Papa:Tusiharibu,tuheshimu maisha na kukuza ikolojia ya haki na upendo
Na Angella Rwezaula; - Vatican.
Katika Liturujia ya leo, inaeleza Heri za Mlimani kwa mujibu wa Injili ya Matayo (Mt 5,1-12). Ya kwanza na muhimu ni “ Heri maskini wa Roho, maana Ufalme wa Mbingu ni wao”. Maskini wa Roho ni akina nani? Ni wale ambao wanajua kuwa hawajitoshelezi wenyewe na kutosheleza, na wanaishi kama omba omba kwa Mungu. Wanajua kuwa wenye kumwitaji Yeye na wanatambua kuwa wema unatoka kwake, kama zawadi na kama neema. Ndivyo Baba Mtakatifu Francisko ameanza tafakari yake akifafanua Injili ya Siku kwa waamini na mahujaji waliokusanyika katika Uwanja wa Mtakatifu Petro mjini Vatican, Dominika tarehe 29 Januari 2023.
Baba Mtakatifu Francisko amesema Aliye maskini katika roho anafanya kuwa tunu kwa kile anachopokea; kwa hiyo anatamani kwamba pasiwepo zawadi yoyote iweze kuharibika. Baba Mtakatifu kwa maana hiyo amependa kujikita katika mantiki ya umaskini wa kiroho kuhusu kutoharibu. Yesu anatuonesha umuhimu wa kutoharibu, kwa mfano baada ya wingi wa mikate na samaki wengi, aliwambia wanafunzi wake wakusanye vipande vyote vilivyobaki, kwa sababu kisipotee kipande cho chote” (Yh 6,12). Kutoharibu kunatuwezesha kufahamu thamani yetu sisi wenyewe, ya watu wengine na vitu vingine. Kwa bahati mbaya, lakini huo ni msingi ambao mara nyingi unasahaulika, hasa katika jamii yenye utajiri. Mahali ambapo panatawala utamaduni wa kutumia hovyo na kubagua. Kwa hiyo Papa Francisko amependekeza changamoto tatu dhidi ya kasumba ya kuharibu au kutumia hovyo.
Changamoto ya kwanza: Usiharibu zawadi ya kile ambacho sisi ni nani. Kila mmoja ni mwema kutegemeana na sifa alizo nazo. Kila mwanamke, kila mwanaume ni tajiri na sio kwa sababu ya talanta lakini kwa hadhi, na kupendwa na Mungu kuna maana ya mwenye thamani. Yesu anatukumbusha kuwa sisi ni wenyeheri sio kwa sababu ya kile tulicho nacho lakini ni kwa kile ambacho sisi tulivyo. Umaskini wa kweli kwa hiyo ni wakati mtu anajiachilia, anatupilia mbali, na anajitoa mwenyewe. Tunapambana kwa msaada wa Mungu dhidi ya vishawishi vya kijizingatia wasiostahili, wakosaji na kujililia.
Baadaye kuna changamoto ya pili ambayo ni “Tusiharibu zawadi tulizo nazo”. Baba Mtakatifu ameongeza kusema kuwa hii imaanisha kwamba katika dunia, kila mwaka, wanaharibu karibu robo tatu ya uzalishaji wa vyakula kwa ujumla. Na hiyo wakati wengi wanakufa kwa njaa! Kwa hiyo “Rasilimali za uumbaji haziwezi kutumiwa namna hiyo; mali zinapaswa kuhifadhiwa na kushirikishwa kwa namna ya kwamba hakuna yeyote anakosa mambo msingi. Tusiharibu kile tulicho nacho, lakini tueneze ikolojia moja ya haki na ya upendo!
Hatimaye Papa Francisko ameelezea changamoto ya tatu ambayo ni kwamba “tusibague watu”. Utamaduni wa kubagua una maana ya kwamba “ninakutumia hadi nitakapokuwa ninahitaji huduma yako: wakati sikuhitaji tena au wewe ni kizingiti, ninakutupilia mbali”. Na hii inatokea hasa hasa kwa watu walio dhaifu zaidi; kama vile watoto ambao hawajazaliwa, (yaani utoaji wa mimba), wazee, wenye kuhitaji na wasio na fursa. Lakini watu hawawezi kutupwa kamwe! Kila mmoja ni zawadi takatifu na ya kipekee kwa kila rika na kwa kila hali. Tuheshimu na kuhamasisha maisha daima!
Baba Mtakatifu ameomba kwa njia hiyo kujiuliza maswali: Awali ya yote je ninaishije umaskini katika roho? Ninajua kutengeneza nafasi kwa Mungu, ninaamini kuwa Yeye ni wema wangu, ukweli wangu na utajiri mkubwa? Ninaamini kuwa Yeye ananipenda au ninajitupa mbali na huzuni, kwa kusahau kuwa mimi ni zawadi? Na baadaye niko makini kutoharibu, ninawajibika katika kutunza mambo na mali? Je nina uwezekano wa kushirikisha na wengine? Hatimaye: ninafikiria walio wadhaifu zaidi kama tunu msingi, ambazo Mungu ananiomba nizihifadhi? Ninawakumbuka maskini, na wale ambao wanakosa mambo ya lazima? Mama Maria atusaidie katika Heri, ili kushuhudia kwa furaha kwamba maisha ni zawadi na uzuri wa kufanya zawadi.