Papa Francisko:wabunge mna wajibu&zinahitajika sheria za haraka kuokoa sayari!
Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican.
Katika matazamio ya COP26, ya Mkutano wa Umoja wa Mataifa kuhusu mabadiliko ya tabianchi utakaofanyika kuanzia tarehe 31 Oktoba hadi tarehe 12 Novemba 2021 huko Glasgow nchini Scotland, Papa Francisko ameomba wabunge wa Italia na wa Umoja wa Ulaya ambao wameshiriki Mkutano ulioandaliwa na Bunge katika maadalizi hayo waongozwe katika kazi yao na taa mbili. Ya kwanza ya uwajibikaji na pili mshikamano! Mwanzoni mwa hotuba yake Papa ameeleza kwamba kuna njia inayopaswa kuchukuliwa ambayo viongozi mbali mbali wa dini na wanasayansi tofauti hivi karibuni walitoa ahadi ya pamoja wakati wanatia saini ya wito wa pamoja hasa katika mtazamo wa COP26, kwa kusukumwa na ufahamu wa changamoto kubwa ambazo zinatishia ubinadamu na sayari na hitaji la mshikamano mkubwa mbele ya janga la ulimwengu.
Katika fursa hiyo, iliyohuishwa na roho ya udugu, Papa amethibitisha kuwa waliweza kuhisi muungano wenye nguvu wa sauti zote tofauti katika kuelezea mambo mawili. Kwa upande mmoja, maumivu ya uharibifu mkubwa uliofanywa katika familia ya wanadamu na kwa nyumba yake ya pamoja; kwa upande mwingine, hitaji la haraka la kuanzisha mabadiliko ambayo yanaweza kusonga na uamuzi na kusadikika kutoka katika tamaduni ya kutupa, iliyoenea katika jamii zetu, hadi kufikia utamaduni wa utunzaji. Papa anakiri, kwamba ni suala juu ya mabadiliko makubwa ambayo yanahitajika kufanya uongofu wa kweli na dhamira thabiti, ukianzia na wale ambao wana nafasi za uwajibikaji. Kwa upande wao, kama wawakilishi wa dini, Papa amesema, wamejitolea sana kufanya kazi katika nyanja hiyo kwa njia ya vitendo na mfano hasa kwa kupendelea elimu katika ikolojia, lakini hii haitoshi.
Papa ameongeza kusema katika hotuba yake kuwa "Na wakati huo huo, ombi limefanywa kwa serikali zote ili kuchukua haraka njia ambayo inazuia kuongezeka kwa kiwango cha joto ulimwenguni na kutoa msukumo wa vitendo vya ujasiri na pia kuimarisha ushirikiano wa kimataifa. Hasa, miito imetolewa ili kukuza mchakato wa mpito wa nishati iliyo safi; kufuata matumizi endelevu ya ardhi wakati wa kuhifadhi misitu na bioanuwai; kukuza mifumo ya vyakula inayoheshimu mazingira na tamaduni za watu asili na mahalia; kupeleka mbele mapambano dhidi ya njaa na utapiamlo; kusaidia mitindo endelevu ya maisha, matumizi na uzalishaji".
Kila mtu lazima afanye sehemu yake, Papa amesisitiza, akizingatia mambo mengi ya mpito kuelekea mtindo wa maendeleo muhimu zaidi na fungamani. Na katika haya yote, jukumu la wabunge ni maamuzi mema na vile vile utekelezaji wa maadili ya siasa nzuri: ambayo ni hekima, kuona mbali na hisia ya faida ya pamoja. Papa Francisko ameeleza: “Ninyi wabunge, kama wahusika wakuu wa shughuli za kutunga sheria, mna jukumu la kuongoza tabia kupitia zana mbali mbali zinazotolewa na sheria, ambayo huweka kanuni za mwenendo unaoruhusiwa kulingana na faida ya wote (Laudato si ') na kwa msingi wa kanuni nyingine kuu, kama vile utu wa mwanadamu, mshikamano na ushirikiano. Utunzaji wa nyumba yetu ya pamoja inaingia ndani ya wigo wa kanuni hizi”.
Papa Francisko amesema, ni suala la kuhimiza njia mpya ili kufikia malengo yaliyowekwa na Mkataba wa Paris na kuchangia kufanikiwa kwa COP26. Na kuhitimisha hotuba yake, Papa Fransisko anawasilisha wito mwingine kwa wabunge: Kwa njia hiyo ni matumaini kuwa kazi yenu inayodai jitidha, kwa mtazamo wa COP26, na hata baada yake, itaangazwa na taa mbili muhimu, ya kwanza ni taa ya uwajibikaji na taa ya mshikamano . Tunalo deni kwa vijana, kwa vizazi vijavyo ambao wanastahili kujitolea kwetu wote ili kuweza kuishi na kutumaini. Kwa hili, tunahitaji sheria za haraka, za busara na za haki, ambazo zinashinda uzio mwembamba wa mzaingira mengi ya kisiasa na zinaweza kufikia makubaliano ya kutosha haraka iwezekanavyo na kutumia njia za kuaminika na zilizo uwazi.