Papa Francisko:Yesu anajionesha kuwa ni mkate wa uzima
Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican.
Katika Injili ya leo kutoka Yh 6,41-51, Yesu anajionesha kwetu kama mkate wa uzima. Hii ni kwa sababu ni Yeye peke yake anayemwilisha roho, ni Yeye peke yake anayetufanya tuhisi tunapendwa, hata kama walio wengi wanamkatisha tamaa. Ni Yeye tu anayetupatia nguvu za kupenda na kusemehe, na ni Yeye anatupatia maisha milele.
Huo ndiyo ujumbe mfupi wa Papa Francisko kwa njia ya mitandao uliotolewa Jumapili tarehe 8 Agosti 2021, ukiangazia kwa dhati Injili ya siku ambapo Yesu anaeleza akionesha uwazi wake kwamba Yeye ni nani na amekuja kufanya nini katika ulimwengu huu na ametumwa na nani. Tunaona hata madharau yaliyo jitokeza kwa wale waliokuwa wanamsikiliza wakisema: " Je huyu siye Yesu, tunayemjua na familia yake? Sasa anasemaje huyu, Nimeshuka kutoka mbinguni? (Yh 6, 41-42).
Papa Francisko katika tafakari ya siku hata hivyo kuhusiana na suala hili ametilia mkazo kuwa “Hata sisi labda tunanung’unika kama wao. Tunasema kuwa ingekuwa vizuri Mungu akae mbinguni bila kujichanganya katika maisha yetu, wakati sisi tunaendelea na mambo yetu hapa duniani. Badala yake, Mungu alijifanya mtu ili aingie kwa dhati ulimwenguni, aingie kwetu kwa dhati, Mungu alijifanya mtu kwa ajili yangu, kwa ajili yako na kwa ajili yetu sisi sote ili awe katika maisha yetu. Na kila kitu katika maisha yetu, vinamhusu”.