Papa atuma baraka katika Sinodi ya wa Waldesi
Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican.
Wawakilishi wa Kanisa la Waldesi wanafanya Sinodi yao ya mwaka huko Kaskazini mwa Italia kwenye mji wa Torre Pellice tangu tarehe 22-25 Agosti 2021. Wachungaji wa viongozi wa makanisa mahalia wanakutana kuzungumzia uhusiano wao na Serikali ya Italia na muhimili wa kiekumena, na wakati huo huo hata masuala mengine kuhusu miundo ya kiliturujia na utawala na kuimarisha masuala yao ya kichungaji.
Katika fursa ya maandalizi ya kukutana, hata hivyo Papa Francisko aliwatumia ujumbe wa kindugu siku ya Jumamosi tarehe 21 Agosti 2021, kupitia telegram iliyotiwa saini na Kardinali Pietro Parolin, Katibu wa Vatican. Papa alielezea furaha yake ya utambuzi ambao unaongeza uhusiano kati ya wa Waldesi na Wakatoliki.
Papa Francisko vile vile aliwahakikisha sala zake kwa wote waliokusanyika huko Torre Pellice kwa ajili ya sinodi hiyo. “Naomba Wakristo wote wajitahidi kuendelea kwa ukarimu katika njia ya muungano kamili, wakishuhudia furaha ya Injili na kukuza maadili ya haki, amani, na mshikamano, hasa kwa umakini maalum kwa wale ambao ni wanyonge au waliotupwa”, Papa amesesema. Kwa kumalizia, ameomba baraka ya Mungu juu ya kazi ya Sinodi ya Waldesi.