Baba Mtakatifu Francisko amesikitishwa sana na mauaji ya kinyama yaliyotokea mjini Kabul na kusababisha watu 50 kupoteza maisha yao wengi wao wakiwa ni wanafunzi. Baba Mtakatifu Francisko amesikitishwa sana na mauaji ya kinyama yaliyotokea mjini Kabul na kusababisha watu 50 kupoteza maisha yao wengi wao wakiwa ni wanafunzi. 

Papa Francisko Asikitishwa na Mauaji ya Kinyama ya Wanafunzi

Watu zaidi ya 50 wamepoteza maisha na wengine zaidi ya 100 wamejeruhiwa. Shambulizi hili la kigaidi limetokea karibu na shule ya Sekondari ya Sayed Ul-Shuhada, huko Kabul. idadi ya wanafunzi waliojeruhiwa wengi wao wakiwa ni wasichana inaweza uongezeka maradufu. Papa Francisko anasema, vitendo hivi ni kinyume kabisa cha utu, heshima na haki msingi za binadamu.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.  – Vatican.

Baba Mtakatifu Francisko mara baada ya Sala ya Malkia wa Mbingu, Jumapili tarehe 9 Mei 2021 ameonesha masikitiko yake makubwa kutokana na vitendo vya kigaidi vilivyotokea Jumamosi tarehe 8 Mei 2021 huko Kabul nchini Afghanstan. Watu zaidi ya 50 wamepoteza maisha na wengine zaidi ya 100 wamejeruhiwa. Shambulizi hili la kigaidi limetokea karibu na shule ya Sekondari ya Sayed Ul-Shuhada, huko Kabul. Serikali ya Afghanstan inasema, idadi ya wanafunzi waliojeruhiwa wengi wao wakiwa ni wasichana inaweza uongezeka maradufu.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, vitendo hivi ni kinyume kabisa cha utu, heshima na haki msingi za binadamu. Baba Mtakatifu ametumia fursa hii kwa ajili ya kusali na kuwaombea wanafunzi waliofariki dunia ili waweze kupokelewa na Mwenyezi Mungu mwingi wa huruma na mapendo kwenye Makao yake ya milele. Mungu awafariji pia wazazi, ndugu na jamaa wanao omboleza kutokana na vifo hivi. Baba Mtakatifu anamwomba Mwenyezi Mungu aweze kuikirimia Afghanstan amani ya kudumu. Wakati huo huo, Baba Mtakatifu Francisko ameonesha wasiwasi kutokana na machafuko ya kisiasa yanayoendelea kutimua vumbi nchini Colombia.

Takwimu zinaonesha kwamba, zaidi ya watu 24 wamefariki dunia kutokana na ghasia hizi, wakati ambapo watu 89 hawajulikani mahali walipo. Wachunguzi wa mambo wanasema, ghasia hizi ni matokeo ya kuporomoka kwa uchumi nchini Colombia. Kumekuwepo na ongezeko kubwa la umaskini na kwamba, asilimia 42.5% ya idadi ya wananchi wote wa Colombia “wanasiginwa” na umaskini mkubwa, unaodhalilisha utu, heshima na haki msingi za binadamu. Yote haya yanachangiwa pia na janga kubwa la maambukukizi ya Ugonjwa wa Virusi vya Korona, UVIKO-19 pamoja na jitihada za serikali kutangaza mabadiliko ya ongezeko la kodi inayolipwa Serikalini. Wananchi wanataka kuona maboresho makubwa katika mfumo wa pensheni, huduma ya afya pamoja na elimu. Mabadiliko ya kodi mpya kwa sasa yamesitishwa kutokana na kuzuka kwa maandamano makubwa kupinga ongezeko hili. Jumuiya ya Kimataifa inaishutumu Serikali ya Colombia kwa kutumia nguvu nyingi za kijeshi kupita kiasi.

Mauaji ya Kinyama Kabul

 

 

10 May 2021, 15:00