Tafuta

Vatican News
Kuweka wakfu wa kikuhani katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro mnamo 12. 05. 2019 Kuweka wakfu wa kikuhani katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro mnamo 12. 05. 2019  (Vatican Media)

Papa Francisko Aprili 25 atatoa daraja la ukuhani kwa vijana 9

Katika Dominika ya IV ya Pasaka,ambayo ni ya Mchungaji mwema,tarehe 25 Aprili saa 3.00,Papa Francisko ataongoza ibada takatifu katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro,Vatican na kuwaweka wakfu wa kikuhani mashemasi 9 wa jimbo la Roma.

Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican.

Papa Francisko kama Askofu wa Roma anarudia kwa mara nyingine tena kutoa daraja la ukuhani katika jimbo lake. Mwaka jana, tukio hilo liliharishwa  kutokana na janga la Covid-19 na kufanywa na Makamu wake Kardinali Angelo De Donatis katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Yohane wa Laterano, Roma. Kwa maana hiyo tarehe 25 Aprili 2021 saa tatu kamili, siku ambayo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika IV ya Kipindi cha  Pasaka na siku ya  Mchungaji mwema, Papa Francisko ataongoza Ibada hiyo katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro, Vatican. Vijana watakaowekwa wakfu wa kikuhani ni tisa na kwa sasa wako katika mafungo ya kiroho kwa kijiandalia vema siku hii muhimu kwao na kwa Kanisa la Roma.

Hata hivyo majiundo yao yamepitia katika seminari tofauti za jimbo. Vijana sita wamesomea katika Seminari Kuu ya Kipapa ya Roma. Hawa ni Georg Marius Bogdan, Salvatore Marco Montone, Manuel Secci, Diego Armando Barrera Parra, Salvatore Lucchesi na Giorgio De Iuri. Wawili wamesomea katika Taasisi ya Redemptoris Mater na  ambao ni Riccardo Cendamo na Samuel Piermarini  na wakati hu huo mmoja  amesomea kwenye Seminari ya Mama wa Mungu Upendo (Madonna del Divino Amore), jina lake ni  Mateus Henrique Ataide da Cruz. Maadhimisho hayo katika Kanisa Kuu  yataanyika kijimbo na kutangazwa moja kwa moja kupitia vyombo vya habari Vatican, Telepace, Tv2000 na kwenye ukurasa wa Facebook wa jimbo.

19 April 2021, 13:24