Papa Francisko:Zawadi ya Mungu kwa ubinadamu ni kumtoa mwanaye
Na Sr. Angela Rwezaula- Vatican.
Ni Dominika ya furaha ambayo Liturujia inatualika kufurahi. Amekumbusha hayo Papa Francisko hata katika tafakari yake kabla ya Sala ya Malaika wa Bwana tarehe 14 Machi 2021, kwa waamini waliokusanyika katika uwanja wa Mtakatifu Petro Vatican. Papa Francisko amesisitizia juu ya sababu ya furaha ya mkristo, iliyoelekezwa na Injili hasa ya Yohane (Yh 3, 16) iliyopendekezwa kwa siku hiyo. Mungu alimtoa Mwanae kwetu sisi sote…. Upendo wa Mungu umepata kilele chake katika zawadi ya Mwana kwa wanadamu dhaifu na wenye dhambi. Papa amerudia tena mazungumzo ya usiku kati ya Yesu na Nikodemu, ambaye alimngojea Masiha akimtambulisha kama mtu hodari ambaye angeuhukumu ulimwengu kwa nguvu. Yesu anamweka katika mashaka ya matarajio haya akiwakilisha hali hiyo katika mantiki tatu: ile ya Mwana wa Mtu aliyeinuliwa msalabani; ya Mwana wa Mungu aliyetumwa ulimwenguni kwa ajili ya wokovu; na ya nuru inayotofautisha wale wanaofuata ukweli na wale wanaofuata uwongo.
Mambo matatu ya utu wa Yesu
Kuanzia hapo Papa Francisko ameonesha mambo matatu ya utu wa Yesu. Akinukuu kifungu kinachoelezea juu ya nyoka wa shaba aliyeinuliwa na Musa jangwani, na kwamba kila aliyekuwa akimtazama nyoka huyo angeweza kupona, Papa ameelezea jinsi, mfano huo ulivyo sawa na Yesu, Mwana wa mwanadamu, na yeye analeta uponyaji. Kazi ya wokovu ya Mungu kwa wanadamu ina usemi wake wa hali ya juu katika kumtoa Mwanae. Kwa maana hiyo, Mungu Baba anapenda watu wake kiasi cha kumtoa Mwanae; alimtoa katika mwili na akamtoa katika kifo.
Kusudi la zawadi ya Mungu ni uzima wa milele wa wanadamu
Mungu kiukweli anamtuma Mwanae ulimwenguni sio kumhukumu, lakini ili ulimwengu uokolewe kupitia Yesu. Utume wa Yesu ni ujumbe wa wokovu, kwa wote, Papa amesisitiza. Nuru ni jina la tatu ambalo Yesu anajipatia mwenyewe. Nuru ambayo imekuja ulimwenguni na ambayo inajumuisha uchaguzi kwa upande wa mwanadamu. Chaguo, ni kati ya kuchukua njia ya nuru au kinyume chake yaani, ya giza. Yeyote atakayechagua giza anakabiliwa na hukumu ya hukumu, yeyote atakaye chagua nuru atapata hukumu ya wokovu. Hukumu daima ni matokeo ya chaguo la bure la kila mtu: yeyote anayefanya uovu hutafuta giza, uovu hujificha kila wakati, na hujifunika. Yeyote anayefanya ukweli, anafanya mema, na mema hayo uonekana katika nuru ambayo inaangazia njia za uzima. Yeyote anayetembea katika nuru, yeyote anayekaribia nuru, hawezi kufanya chochote isipokuwa matendo mema.
Fungua mioyo kwa upendo wa mungu usio na kipimo
Papa Francisko kwa maana hiyo ametoa mwaliko wa kufungua mioyo kwa upendo wa Mungu usio na kipimo, kwa huruma yake iliyojaa upole na wema. Naametoa mwaliki wa kujitoa zaidi wakati wa Kwaresima, kuikaribisha nuru ya Kristo katika dhamiri za kila mmoja. Papa Francisko amesema kuwa “msisahau kwamba Mungu husamehe kila wakati, kila wakati ikiwa, kwa unyenyekevu, tunaomba msamaha. Omba msamaha tu, naye anasamehe. Kwa hiyo hiyo tutapata furaha ya kweli na kuweza kufurahi katika msamaha wa Mungu ambao huzaa upya na kutoa uzima”. Papapa amehitimisha kwa kujikabidhi kwa Maria ili tubapte kuwa hurudhi dhidi ya woga wa kujiruhusu kuchangamotishwa na Yesu. Ni mgogoro mzuri, kwa ajili ya kupona kwetu; ili furaha yetu iweze kuwa kamili.