Tafuta

2021.03.10: Katekesi ya Papa Francisko kuhusu ziara yake ya kitume nchini Iraq 2021.03.10: Katekesi ya Papa Francisko kuhusu ziara yake ya kitume nchini Iraq 

Papa Francisko:udugu ni changamoto ya dunia nzima!

Papa amesema undugu ni changamoto kwa ulimwengu wote. Je!Tutaweza kuunda udugu kati yetu?kujenga utamaduni wa udugu au tutaendelea na mantiki iliyoanzishwa na Kaini:vita.Udugu,undugu.Watu wa Iraq wanayo haki ya kuishi kwa amani.Ni katika tafakari ya Papa Francisko katika Katekesi juu ya ziara yake ya kitume.

Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican.

Katika siku zilizopita Bwana ameniwezesha kutembelea Iraq, kutumiza mpango wa Mtakatifu Yohane Paulo II. Hakuna Papa aliyekuwa amewahi kwenda katika ardhi ya Ibrahimu. Neema hiyo imewezesha kutimizwa hilo sasa, kama ishara ya matumaini, baada ya miaka ya vita na ugaidi na wakati mgumu wa janga. Ndivyo Papa Francisko ameanza wakati wa Katekesi yake Asubuhi, Jumatano tarehe 10 Machi 2021, akijikita kuelezea juu ya ziara yake ya kitume iliyoanza mnamo tarehe 5 -8 Machi. Papa Francisko amesema baada ya ziara hiyo moyo wake umejazwa na shukrani. Shukrani kwa Mungu na kwa wale wote ambao wamewezesha,akianzia kuwataja kuwa Rais wa jamhuri na Serikali ya Iraq; Patriaki na Maaskofu wa Nchi, pamoja na wahudumu na waamini wa Makanisa yote; viongozi wakuu wa dini kuanzi na Ayatollah Al-Sistani, ambaye alimtembelea anapoishi Najaf na kufanya mkutano ambao amesema hatasahu.

Nguvu ya toba katika hija ya Papa

Papa Francisko akiendelea kufafanua amesema ni kwa jinsi gani alihisi nguvu ya maana ya toba katika hija hiyo, kwa maana hasingeweza kuwakaribia watu hao walioteseka, Kanisa la kishahidi bila kubeba juu yake  kwa niaba ya Kanisa Katoliki, msalaba ambao wanabeba kwa miaka: msalaba mkubwa kama ule ambao ulikuwa umewekwa mbele ya Qaraqosh. Papa amebainisha alivyohisi kwa namna ya pekee kuona majeraha yaliyo wazi ya uharibifu na zaidi kukutana na kusikiliza ushuhuda wa walionusurika na vurugu, mateso na kukimbia… Na wakati huo huo aliona amezungukwa na furaha ya makaribisho ya mjumbe wa Kristo; Papa amesema alivyoona matumaini ya kujifungulia upendo wa amani na udugu, ambao unafupishwa katika maneno ya Yesu yaliyokuwa kwenye nembo ya ziara ya kitume” Ninyi nyote ni ndugu” ( Mt 23,8).

Matumaini kwa na ushuhuda na ishara

Papa amebainisha kuwa matumaini hayo aliyaona katika hotuba ya Rais wa Jamhuri na kwa salamu nyingi na shuhuda, katika nyimbo na ishara za watu. Alisoma katika nyuso nyingi zinazong’aa za vijana na machoni mwa wazee. Watu walikuwa wanamsubiri Papa kwa masaa matano wakiwa wamesisima hata wanawake na watoto mikononi mwao. Walikuwa wanasubiri na machoni mwao kulikuwa na matumaini. Papa Francisko amesema, watu wa Iraq wanayo haki ya kuishi kwa amani, wana haki ya kupata hadhi ambayo inawastahili. Mizizi yake ya kidini na utamaduni ni wa miaka mingi. Mesopotamia, ni  makao ya utunzaji wa ustaarabu; Baghdad katika historia imekuwa mji wa kwanza muhimu ambao ulikaribisha kwa karne nyingi makumbusho ya vitabu vyenye utajiri mkubwa. Je ni kitu gani kiliuharibu? Vita.

Vita daima ni mnyama hujigeuza na kuendelea kula ubinadamu

Vita daima ni mnyama ambaye, pamoja na umri unaobadilika, hujigeuza na kuendelea kula ubinadamu Na mimi nikajiuliza: ni nani alikuwa akiuza silaha kwa magaidi? Nani leo hii anauza silaha kwa magaidi, ambao wanaua sehemu nyingine; kwa mfano hebu fikiria Afrika. Ni swali ambalo ningependa mtu ajibu”. Papa ameendelea kusema kuwa  “Lakini jibu la vita siyo vita vingine, jibu la silaha siyo silaha nyingine.  Jibu lake ni udugu. Hii ndiyo changamoto kwa ajili ya iraq, lakini si tu hiyo ni changamoto kwa kanda nyingi zenye migogoro na isiyoisha kwa ulimwengu mzima. Undugu ni changamoto kwa ulimwengu wote. Je! Tutaweza kuunda udugu kati yetu? kujenga utamaduni wa udugu? Au tutaendelea na mantiki iliyoanzishwa na Kaini: vita. Undugu, undugu.

Sala ya pamoja ya wakrist,waislamu na dini nyingine

Papa Francisko amesema kuwa walikutana na walisali wakristo na waislamu na wawakilishi wa dini nyingine huko Uru mahali ambapo Ibrahimu alipokea wito wa Mungu karibia miaka elfu nne iliyopita. Ibahimu ni baba katika imani kwa sababu alisikiliza sauti ya Mungu ambayo ilimpa ahadi ya uzao, aliacha kila kitu na kuondoka. Mungu ni mwaminifu kwa ahadi zake na bado leo hii anaongoza hatua zetu kwa amani, anaongoza pamoja chini ya anga lile angavu, anga lile ambalo Baba Yetu Ibrahimu aliona sisi uzao wake, na kwamba siku hiyo wahisi kama vile sentesi ilikuwa yao ya “ ninyi nyote ni ndugu.” Ujumbe wa kidugu ulifika kutoka katika mkutano wa kikanisa katika Kanisa kuu la Kisiria katoliki la Baghdad , mahali ambapo mnamo mwaka 2010 waliuwawa watu 48, miongoni mwao mapadre wawili wakati wanaadhimisha Ibada ya Misa, Papa amefafanua.

Kanisa la Iraq ni la kishahidi

Kanisa la Iraq ni Kanisa moja la kishihidi na katika hekalu lile ambalo kuna muhuri kwenye jiwe linalokumbusha ushihidi huo na ambao uliibua furaha ya kukutana. Mshangao wa Papa anasema, ilikuwa ni kwamba yeye alikuwa katikati yao na kujichanganya na furaha yao ya kuwa na Papa katikati yao. Ujumbe wa Kidugu amezinduliwa huko Mosul na huko Qaraqosh, juu ya mito ya Tigri karibu na uharibifu wa mji wa kizamani wa Ninawi, Papa amesema. Kuvamiwa kwa Issis kulisababisha kukimbia  kwa maelfu na maelfu ya wakazi, miongoni mwao wakiwa ni wakristo wa madhehebu mbali mbali na wengine wachache wanaoteswa, hasa Wayazidi, Papa ameeleza.  Uliharibiwa utambulisho wa mji wa kizamani. Kwa sasa wanatafuta kwa ugumu kuukarabati; waislamu wanawaalika wakristo warudi na kwa pamoja kukarabati makanisa na misikiti.

Wito wa kuendelea kusali ili wapate nguvu ya kuanzakwa upya

Kutokana na hilo ndipo   Papa Francisko ameomba kuendelea kusali kwa ajili ya kaka na dada hao waliojaribiwa, kwa sababu waweze kupata nguvu ya kuanza kwa upya. Kwa kufikiria Wairaq wengi waliohama, Papa amewambia wao kuwa waliacha kila kitu kama Ibrahimu; kama yeye, walinde imani na matumaini na wawe wasukaji wa urafiki na udugu mahali popote walipo. Ujumbe wa udugu umefika kupitia Madhimisho mawili ya Ekaristi. Wa kwanza huko Baghdad, katika ibada ya Kikaldayo na wa pili huko Erbil, mji ambao alikaribishwa na Rais katika Mkoa na Waziri Mkuu, Mamlaka na watu. Matumaini ya Ibrahimu na uzao wake ulitimizwa katika huduma ambayo walisherehekea katika Yesu, Mwana wa Mungu Baba ambaye hakujibakiza, lakini alijtoa kwa wokovu wa wote.

Kama matunda ya mitende izae matumani kwa Iraq,Mashariki ya kati na ulimwengu

Yeye kwa kifo chake na ufufuko alitufungulia njia katika nchi ya ahadi, katika maisha mapya, mahali ambapo machozi yanapanguswa, majeraha yanapona, na ndugu wanapatana. Kwa kuhitimisha katekesi yake katika muktadha wa ziara yake ya kitume nchini Iraq, Papa amesema “tusifu Mungu kwa ajili ya Historia ya Ziara hii na kuendelea kusali kwa ajili ya Nchi ile na kwa ajili ya Nchi za Mashariki ya Kati. Nchini Iraq, licha ya kishindo cha uharibifu na silaha, mitende, ishara ya nchi na matumaini yake, imeendelea kukua na kuzaa matunda. Ndivyo ilivyo kwa udugu: kama matunda ya mitende, haitoi kelele, lakini mtende unazaa na hutukuza. Mungu, ambaye ni amani, aipe  wakati ujao wa udugu nchi ya Iraq, Mashariki ya Kati na ulimwengu wote!

KATEKESI YA PAPA 10 MACHI 2021
10 March 2021, 12:11

Mikutano ya Baba Mtakatifu kwa siku za hivi karibuni

Soma yote >