Papa Francisko:Furaha siyo nadharia ni uzoefu wa kujua kuwa unapendwa katika maisha
Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican.
Papa Francisko akianza na salamu kwa Jumuiya wa Wafilipino wa Roma ambao walikuwa wanawakilisha jumuiya nzima katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro amesema Kanisa ni zuri na la kuvutia ambalo linapenda ulimwengu bila kuhukumu na kwayo linajitoa lenyewe. Ni katika fursa ya maadhimisho ya miaka 500 tangu kuanza uinjilishaji katika nchi yao ya asili ambapo Papa Francisko amewashukuru kwa furaha ya imani wanayopeleka ulimwengu wote na katika jumuiya za kikristo kuanzia na wanapoishi. Amefikiria juu ya uzoefu mwingi mzuri katika familia za Roma, lakini hata katika ulimwengu mzima mahali ambao wafilipino wapo wanafanya kazi na wamtambua kutoa ushuhuda wa imani. Kama mtindo wa Maria na Yosefu: Mungu anapenda kupelekea furaha ya imani kwa huduma ya nyenyekevu na iliyofichika, jasiri na vumilivu.
'Bato balani sa gugma' yaani Sumaku ya upendo
Mwanzoni mwa liturujia Papa amefika kwa maandamamo katika Kanisa Kuu akiongozana na Kardinali Luis Antonio G. Tagle, Rais wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa watu, mwenye asili ya Kifilipino, Kardinali Angelo De Donatis, Makamu wa Papa wa Jimbo la Roma, na makuhani 8 wa Jumuiya ya Kifilipino. Wimbo wa lugha yao uitwao “Bato balani sa gugma”, yaani ‘sumaku ya upendo’ uliongoza, maandamamo hayo, na altareni wamepeleka msalaba wa Magellano na sanamu ndogo inayomwakilisha Mtakatifu Niňo, yaani Mtoto Yesu. Mara baada ya Misa Takatifu , Kardinali Tagle ametoa salamu na shukrani kwa niaba ya wahamiaji wote wakifilipino walioko Roma, huku akikumbuka vipindi vya upekwe hasa wanapofika kwa mara ya kwanza, japokuwa amesema wanapata nguvu katika Yesu ambaye anasafiri na kila mmoja. Aidha amesema hata wanapokosa bibi na babu zao wanakumbuka kuwa wanaye “Lolo Kiko” yaani wanao kupitia kwa Papa Francisko.
Injili siyo fundisho ni Yesu aliyejitoa kwetu
Katika tafakari ya Papa Francisko, kwenye Dominika ya nne ya Kwaresima na ambayo inaitwa Laetare, imejikita juu ya meneno ya Yesu ambaye anamwambia Nikodemu katika Injili ya Yohane iliyopendekezwa katika liturujia kuwa “ Mungu aliupenda ulimwengu hata akamtoa Mwanaye wa pekee. Papa anasema hapa kuna msingi wa furaha yetu. Ni muktadha wa Injili ambayo siyo wazo au fundisho, bali ni Yesu Mwana, ambaye Baba alitupatia kwa sababu hata sisi tuwe na maisha”.
Furaha siyo nadharia ni uzoefu wa kupendwa katika maisha
Msingi wa furaha yetu siyo nadharia nzuri ya jinsi gani tuweze kuwa na furaha, badala yake ni kufanya uzoefu wa kuwa tunasindikizwa na kupendwa katika safari ya maisha. Kutokana na hilo, Papa Francisko amesisitiza juu ya mantiki mbili za sentesi isemayo: “alipenda sana” na “kumtoa. Mungu alipenda sana ni maneno ambayo Yesu alimweleza Nocodemu, mzee myahudi ambaye alitaka kumjua Mwalimu na ambaye anatusaidia kutambua uso wa kweli wa Mungu. Mungu ambaye daima alitutazama kwa upendo na kwa upendo alikuja katikati yetu katika mwili wa Mwana”. Katika Yesu, Papa amebainisha Mungu atamka maneno ya mwisho juu ya maisha yetu: ‘wewe hujapotea, wewe unapendwa’. Inawezekana kusikiliza kwetu Injili na kuiweka katika matendo ya imani yetu, hakutufanyi kutambua ukuu huo wa upendo na labda tunaelekeza katika kutimiza udini, huzuni, na kujifungia binafsi. Ni ishara ambazo tunapaswa kusimama na kusikiliza kwa upya tangazo la habari njema, Papa ameshauri
Ni baba anayependa na kujihusisha na historia yetu
Papa Francisko akiendelea amesema “Mungu anakupenda kwa namna hii hadi kutoa maisha yake yote. Sio Mungu ambaye anatazama tofauti kutoka juu, lakini ni Baba anayependa sana, anayejihusisha na historia yetu; siyo Mungu ambaye anapendwa tu bali ni Baba ayeangaika ili pasiwepo hata mmoja anayepotea; siyo Mungu anayehukumu, bali ni Baba anayetuokoa kwa mkubatio wa baraka ya upendo wake”. Kwa kutazama neno la pili, la Mungu alimtoa Mwanae, Papa Francisko amesisitiza kwamba, kutokana na kwamba anatupenda sana, ndiyo maana Mungu anajitoa mwenyewe na anatupatia maisha yake. Nguvu ya upendo ni kwamba, inavunja ganda la ubinafsi, inavunja mipaka ya usalama uliohesabiwa sana wa kibinadamu, inavunja kuta na kushinda hofu, ili kujifanya zawadi. Wale wanaopenda wanapendelea kujihatarisha kwa kujitoa badala ya kujithamini, kama Mungu anavyofanya, na ambaye anajitoa binafsi kwa sababu alipenda sana. Katika Yesu, aliyeinuliwa msalabani, Mungu mwenyewe alikuja kutuponya kutokana na sumu inayotoa kifo, kama vile nyoka waliowashambulia watu wa Israeli jangwani; alijifanya mdhambi ili kutuokoa na dhambi. Mungu hatupendi kwa maneno tu, amekumbush Papa, kwa sababu anatupatia Mwanae ili kila mtu anayemwangalia na kumwamini apate kuokolewa. Kwa sababu hiyo unapopenda zaidi, ndivyo unavyoweza kutoa.
Ni vizuri kukutana na watu wanaopendana
Papa Francisko akiendelea na tafakari yake amesema:“Ni vizuri kukutana na watu wanaopendana, watu wanaotakiana mema na kushirikishana maisha; tunaweza kusema juu yao kama Mungu: wanapendana sana kiasi kwamba wanatoa maisha yao. Sio tu kuhesabu kile tunachoweza kuzalisha au kupata, kinacho hesabiwa hasa ni upendo ambao sisi tunajua jinsi ya kuutoa. Mungu aliupenda ulimwengu hata akamtoa Mwanawe ndiyo chanzo cha furaha! Papa Francisko ameongeza kusema kwa sababu hiyo leo hii, Kanisa, pamoja na Isaya, linahimiza, juu ya “Dominika Laetare” yaani “Shangilieni na furahini, ninyi mliokuwa katika huzuni”. Na katika hili amerudi nyuma kufikiria safari yake ya Iraq: “Watu walioteswa walifurahi, ashukuriwe Mungu, kwa huruma yake”. Wakati mwingine, “tunatafuta furaha mahali ambapo hakuna”, katika udanganyifu unaopotea”, “ndoto za ukuu wa nafsi yetu ya umimi”, katika usalama wa vitu, au katika ibada ya sura zetu”. “Lakini uzoefu wa maisha unatufundisha kwamba furaha ya kweli ni kujisikia kupendwa bure, kuhisi kusindikizwa, kuwa na mtu ambaye anashiriki ndoto zetu na ambaye, wakati tunazama, anakuja kutusaidia na kutuongoza kwenye bandari salama”, Papa amefafanua.
Tangazo la kikristo lazima lipelekwe kwa wengine
Kwa kuwapongeza jumuiya ya Kifilipino katika uzoefu wao wa imani na furaha katika shughuli zao zote, Papa Francisko amesema wanaionesha na kuifanya kuwa mtindo wa Maria na Yosefu, kwa sababu Mungu anapenda kuleta furaha ya imani na huduma ya unyenyekevu na iliyofichwa, ya ujasiri na ya kudumu. Amewaomba wasiache kuendeleza kazi ya uinjilishaji na ambayo siyo kuigeuza propaganda. Tangazo la Kikristo lililopokelewa daima linapaswa kupelekwa kwa wengine, kutunza wale waliojeruhiwa na wanaoishi pembezoni. Kama Mungu anayejitoa kwetu, Kanisa pia halikutumwa kuhukumu, bali kwa ajili ya kukaribisha; sio kulazimisha, lakini kupanda mbegu; sio kuhukumu bali kupeleka kwake Kristo ambaye ni wokovu. Papa amesema: “Msiogope kutangaza Injili, kutumikia na kupenda. Na kwa furaha yenu mtaweza kuhakikisha kwamba Kanisa pia linasema aliupenda ulimwengu sana. Kanisa linalopenda ulimwengu bila kuhukumu na ambalo linajitoa kwa ajili ya ulimwengu ni zuri na la kuvutia. Na ndiyo iwe hivyo huko Ufilipino na katika kila sehemu ya dunia” amehitimisha Papa Francisko.