Tafuta

2020.02.27 Mtakatifu  Gabrieli wa Mateso 2020.02.27 Mtakatifu Gabrieli wa Mateso  

Papa Francisko:Vijana igeni mfano wa Gabrieli ili kupata utimilifu katika Kristo

Ushuhuda wa kikristo wa Mtakatifu Gabrieli ulikuwa wa aina yake hadi kufikia kuwa mfano wa Kanisa hasa kwa ajili ya kizazi kipya.Ndivyo Papa anaandika katika barua aliyomtumia Askofu wa Jimbo la Teramo-Atri,katika fursa ya uzinduzi mwaka wa Jubilei tangu kutangazwa Mtakatifu mnamo 1862 na Papa Benedikto XVI.Ni mwaliko kwa vijana wagundue tena maisha ya kijana huyo aliyeaacha dunia akapata utimilifu katika Kristo.

Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican.

Papa Francisko  ametuma ujumbe wake kwa Askofu Lorenzo Leuzzi wa Jimbo katoliki la Teramo-Atri, Italia  ambao Jumamosi tarehe 27 Februari 2021 wamefungua mwaka wa  Jubilei  ya miaka 100 tangu kutangazwa mtakatifu kijana Gabrieli  wa Mateso. Katika  ujumbe huo Papa anaandika: “katika fursa ya ufunguzi wa mwaka wa Jubilei tangu kutangazwa kwa Mtakatifu Gabrieli wa Mateso imepita miaka 100 tangu mtangulizi wangu Benedikto XV alipotangaza Mtakatifu Gabrieli wa Mateso, aliyefariki katika kisiwa cha Gran Sasso mnamo tarehe 27 Februari 1862 akiwa na umri wa miaka 24”. Papa Fracisko  anaendelea kusema kuwa “tukio hili lilionesha kuwa ushuhuda wake wa kikristo ulikuwa namna hii maalum na wa kipekee hadi kufikia kuwa mfano  wa kuigwa  kwa ajili ya Kanisa hasa kwa ajili ya kizazi kipya.”

Papa katika kukumbuka na maana ya  maadhimisho hayo anapenda “kuungana kiroho na Jimbo hilo, Mapadre wa shirika la Mateso, Jumuiya ya Kikristo ya Abruzo na Molise na kwa wale wote ambao wanashiriki mpango wa maandalizi ya ufunguzi wa mwaka wa Mtakatifu katika Madhabahu ya Mtakatifu huyo na msimamizi wa vijana. Ni matumaini yake kwamba mpango huo wa maandalizi kwa ajili ya miaka miamoja unaweza kuwa muafaka wa kuwaleta katika ibada  kuu wale wote ambao wanamwona Mtakatifu huyo mpendwa kama mfano wa ushuhuda wa Injili na kwa maombezi yake kwa Mungu. Gabrieli alikuwa ni kijana wa wakati wake, aliyejaa maisha na shauku, kwa kuongoza na shauku ya utimilifu ambao ulikuwa ukimsukuma zaidi ya hali halisi ya ulimwengu na mambo yake huku akijificha ndani ya Kristo, Papa anandika. Hata leo, anawaalika vijana kutambua ndani mwao hamu ya maisha na utimilifu, ambao hauwezi kutenganishwa na utafutaji wa Mungu, kutokana  na kukutana na Neno lake ambalo linatia nguvu ya  uwepo wao, kuanzia katika  huduma na kuilekeza kwa ndugu, hasa walio wa dhaifu zaidi, amesisitiza Papa.

Maisha yake mafupi lakini ya kina yaliacha nyayo ambayo inadumu maisha yake yote kwa dhati. Papa Francisko amesema kwa mfano huo uweze kuigwa na kuwa kwa vijana watawa wa Mateso, nguvu ya amani, uthabiti katika matumaini na shauku katika upendo, kwa kuongozwa  na safari ya  watawa, na waamini walei katika umakini wa upendo kuelekea kwa Mungu na kuelekea jirani. Hasa katika kipindi hiki cha dharura ya kiafya na matokeo ya udhaifu wa kiuchumi na kijamii Papa amesema ni lazima kwamba wafuasi wa Bwana wageuke kuwa  mfano zaidi na chombo cha  muungano na udugu kwa kuupanua kwa wengine ule  upendo wa Kiristo na kuwaangazia kwa matendo ya dhati ya ukaribu, upole na jitihada. Kwa kihitimsha, Papa Francisko ansema, kwa wote ambao wanashiriki katika mipango mbalimbali ya kuhamasisha kuishi sala na upendo katika mwaka huu wa maana ya Jubilei, anawatakia waweze kujigundua kwa Bwana, wakiweza kutambua uso wa kila kaka na dada ambao wanahitaji faraja na matumaini. Kwa hisia hizo wakati akiomba wamwombee naye kwa moyo wote amewapa baraka yake ya kitume.

Rehema kamili kwa wale wanaosherehekea Jubilei ya Mtakatifu Gabrieli

Idara ya Toba ya Kitume imetoa rehema kamili hadi  27  Februari  2022, mara moja kwa siku kwa ajili ya mtu binafsi, au kwa ajili ya kuombea roho za marehemu, kwa mahujaji wanaotembelea  madhabahu ya Mtakatifu  Gabrieli wa Mateso na kushiriki katika sherehe ya Jubilei au  kutumia muda vizuri  mbele sanduku  la Mtakatifu Gabrieli, na kuhitimisha kwa sala ya Baba yetu na kanuni ya Imani, na kwa maombi yaliyoelekezwa kwa Bikira Maria na kwa Mtakatifu Gabrieli  ikiwa ni pamoja na (kuungama, kupokea ekaristi, na maombi kwa wa nia za Papa). Wazee, wagonjwa na wale ambao kwa sababu kubwa hawawezi kutoka nyumbani, wataweza kupokea rehema  kamili baada ya kuamua kujitenga na dhambi zote na kwa nia ya kutimiza masharti matatu ya kawaida haraka iwezekanavyo, wakiwa mbele ya picha fulani ya mtakatifu na kuungana kiroho kwa yule anayeadhimisha Jubilei  huku wakimtolea Bwana sala na mateso yao.

27 February 2021, 14:15