2019.01.07 Watawa wa wa shirika la Moyo safi wa Bikira Maria, Mama wa Kristo (Nigeria) 2019.01.07 Watawa wa wa shirika la Moyo safi wa Bikira Maria, Mama wa Kristo (Nigeria)  

Ujumbe wa Papa,Siku ya Kimisionari 2021:hatuwezi kuacha kunena tuliyoona na kuyasikia

Ujumbe wa Papa kwa Siku ya Kimisionari Ulimwenguni 2021,unaongozwa na mada “Kwa maana hatuwezi kuacha kuyanena mambo tuliyoyaona na kuyasikia”(Mdo 4,20).Katika muktadha wa sasa,kuna haja ya dharura ya umisionari wa matumaini kwa waliowekwa wakfu na Bwana ili wawe na uwezo kinabanii kukumbusha kuwa hakuna anayejiokoa mwenyewe.Leo hii Yesu anahitaji mioyo yenye uwezo wa kuishi wito kama historia ya upendo,unaojikita kwenda pembezoni mwa ulimwengu.

Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican.

Katika ujumbe Papa Francisko wa Siku ya Kimisionari ulimwenguni 2021, uliotolewa Ijumaa tarehe 29 Januari, ambao unaongozwa na kauli mbiu "Hatuwezi kuacha kuyanena mambo tuliyoyaona na kuyasikia”( Mdo 4,20), anasema, tunapofanya uzoefu wa nguvu ya upendo wa Mungu, tunapoweza kutambua uwepo wa Baba katika maisha yetu binafsi na kijumuiya, hatuwezi kuacha kutangaza na kushirikisha kile ambacho tuliona na kusikiliza. Uhusiano na Yesu na wafuasi wake, ubinadamu wake ambao unajifunua katika fumbo la kufanyika mwili, katika Injili yake na katika Pasaka yake vyote hivyo vinatuonesha jinsi gani Mungu anapenda ubinadamu wetu na anafanya kuwa furaha zetu, mateso yetu, shauku zetu na huzuni wetu ni vyake ( taz. Gaudium et spes, 22). Hayo yote kwa Kristo yanatukumbusha kuwa ulimwenguni ambamo tunaishi na hitaji lake la wokovu sio geni na tunaalikwa hata kuhisi kuwa sehemu hai ya utume usemao: “Basi enendeni hata njia panda za barabara, na wote muwaonao waiteni arusini”(Mt 22,9). Hakuna mtu mgeni, hakuna ambaye anaweza kuhisi mgeni au mbali kulingana na upendo huu wa huruma.

Uzoefu wa Mitume: Upendo daima upo katika mzunguko

Historia ya unjilishaji inaanza na utafutaji wa shauku wa Bwana  ambaye anaita na anataka kuudumisha kwa kila mtu, mahali alipo, kuwa na mazungumzo ya urafiki (Yh 15,12-17). Mtume yuko mstari wa mbele kutuelekeza hilo, kutukumbusha hadi siku na saa ambayo walikutana naye: “Nayo ilikuwa yapata saa kumi za jioni”( Yh 1,39). Urafiki na Bwana  uliwafanya kumwona akiwatibu wagonjwa, akila na wadhambi, akiwashibisha wenye njaa, akiwakaribia waliobaguliwa, kuwagusa walio najisi, kujifananisha na wenye kuhitaji, kuwaalika katika heri, kufundisha kwa namna mpya na kwa mamlaka, anaacha alama isiyoweza kufutika, inayoweza kuamsha mshangao na furaha kubwa na ya bure ambayo haiwezi hata kushikika. Kama alivyokuwa akisema nabii Yeremiah, uzoefu huu ni moto unaowaka, wa uwepo wake katika mioyo yetu na ambao unatusukuma kwenda katika utume, licha ya kutoa sadaka na kutoeleweka (Yh 20,7-9). Upendo daima huko katika mzunguko na unatualika kuwa katika mzunguko kwa ajili ya kushirikishana tangazo zuri zaidi na kisima cha matumaini hadi kusema “ tumwemwona Masiha (Yh 1,41). Katika Yesu tumeona, tumemsikiliza na kugusa mambo ambayo yanaweza kuwa tofauti, Papa anabainisha. Yeye amevumbua tayari leo hii  hayo na  nyakati za baadaye akitukumbusha tabia msingi ya kuwa binadamu, na mara nyingi iliyosahulika kwamba “ tuliumbwa kwa ukamilifu ambao unafikiwa kwa njia ya upendo tu (Fratelli tutti 68). Nyakati mpya ambazo zinaamsha imani inayoweza kutoa msukumo katika mipango na kuumba jumuiya, huanzia na wanaume na wanawake ambao wanajifunza kubeba udhaifu binafsi na wa wengine, kuhamasisha udugu na urafiki kijamii (Ft 67).

Upendeleo wa pendo wa Bwana, unatushangaza kwa maumbile yake

Jumuiya ya kikanisa inaonesha uzuri wake kila mara inapofanya kumbu kumbu kwa shukrani kuwa Bwana ametuita akiwa wa kwanza (Yh 4,19).  Upendeleo wa pendo wa Bwana, unatushangaza na mshangao, kwa maumbile yake, hauwezi kumilikiwa au kuwekwa na sisi. […] Ni kwa njia hiyo tu inawezekana kuchanua miujiza ya bure, zawadi ya bure. Hata kwa ajili ya umisionari ambao hauwezi kupatikana kutokana na kufikiria na kufanya hesabu. Kujiweka katika hali ya kitume ni kielelezo cha kushukuru (Ujumbe wa Papa kwa Matendo ya kimisionari 21 Mei 2020).  Walakini nyakati za kwanza hazikuwa rahisi. Wakristo wa kwanza walianza na maisha yao ya imani katika mazingira ya uhasama na magumu. Historia za kutengwa na kufungwa zilifungamana na upinzani wa ndani na nje, ambao ulionekana kupingana na hata kukataa kile walichokiona na kusikia; lakini hayo badala ya kuwa matatizo au vizingiti ambavyo vingepelekea kujikunjia wao binafsi; viliwasukuma kubadilisha kila kitu, kinyume na matatizo iligeuka kuwa fursa kwa ajili ya utume. Vizingiti na vikwazo viligeuka navyo kuwa  mahali muafaka kwa ajili ya kupata kila kitu na wote kwa Roho wa Bwana. Hakuna na wala yeyote ambaye alikuwa mgeni katika kutangaza uhuru.

Janga limeonesha na kuongeza uchungu, upweke na umaskini

Ushuhuda hai wa hayo yote unapatikana katika Kitabu cha Matendo ya mitume ambamo wafuasi wa kimisionari daima wanacho mikononi mwao. Ni kitabu kinachosimulia jinsi manukato ya Injili yalivyo sambazwa na kusababisha furaha ambayo ni Roho tu anaweza kuitoa. Kitabu cha Matendo ya Mitume kinatufundisha kuishi majaribu, kwa kushikamana na Kristo ili kukomaa kiimani kwamba Mungu anaweza kutenda kwa kila hali hata katikati uwazi wa kushindwa na uhakika kuwa anayejitoa  sadaka na kutoa kwa Mungu kwa upendo hakika atakuwa na matunda (taz. Yh 15,5” na Evangelii gaudium, 279). Kwa njia hiyo hata sisi, katika kipindi hiki cha sasa ambacho kihistoria siyo rahisi. Hali halisi ya janga limeonesha na kuongeza uchungu, upweke, umaskini na ukosefu wa haki ambamo wengi wanateseka na limefunua  wazi hali za uongo wetu wa usalama na mipasuko mingi, migawanyiko na kugawanyika na ambayo hutenganisha kimya kimya. Walio wadhaifu zaidi na wenye mazingira magumu wamefanya uzoefu na bado kuathiriwa zaidi  na udhaifu huo. Papa Francisko amebainisha juu ya uzoefu wa kuishi kwa kukata tamaa, bila mafanikio, ugumu, hadi kufikia hata uchungu wa kufanana, ambao huondoa tumaini, na umeweza kuchukua miliki ya mitazamo yetu. “Kwa maana hiyo hatujihubiri wenyewe, bali Kristo Yesu ya kuwa ni Bwana; na sisi wenyewe kuwa tu watumishi wenu kwa ajili ya Yesu.” (2 Kor 4,5).  Katika hilo tunahisi kualikwa tena ndani ya  jumuiya zetu na katika familia kwa Neno la Maisha linalojiegemeza ndani ya mioyo yetu na linatuambia “ Hayupo hapa, amefufuka (Lk 24,6); Neno la matumaini ambalo linavunja kila aina ya misimamo na kwa wale  wanaoacha waguswe  linawapatia uhuru  na ujasiri muhimu kwa ajili ya kusimama na kutafuta kwa ubunifu wote namna inayowezekana ya kuishi kwa shauku, sakramenti ya ukaribu wa Mungu kwetu ambaye amwachi hata mmoja kingoni mwa barabara.

Dharura ya utume wa huruma wenye uwezo wa kuwa na ukaribu

Papa Francisko  katika ujumbe wake anadika kuwa, katika wakati huu wa janga, na kukabiliwa na jaribu la kuficha na kuhalalisha kutokujali kwa jina la utengamano mzuri wa kijamii ni dharura ya utume wa uhuruma wenye uwezo wa kufanya  katika umbali wa lazima mahali pa mkutano, mahali pa kutunza na kuhamasisha. “Kwa maana sisi hatuwezi kuacha kuyanena mambo tuliyoyaona na kuyasikia” (Mdo 4,20), huruma ambayo imekuwa kwetu, inabadilishwa kwa namna ya kuwa kiongozi, na uaminifu ambao umeturuhusu kupata tena hamu ya kushirikishana kwa ajili ya kuunda jumuiya moja ya ushiriki na mshikamao ambamo tunaweka wakati, jitihada na mali”( Ft, 36). Ni Neno lake ambalo kila siku linatukomboa na kutokoa na zile samahani ambazo zinapelekea tujifungie ndani ya wasiwasi mbaya zaidi  wa kusema “hata hivyo ni sawa hakuna kitakachobadilika. Na mbele ya kujiuliza swali:“Ni sababu gani lazima nijinyime usalama wangu, faraja na raha ikiwa siwezi kuona matokeo yoyote muhimu? Lakini jibu linabaki lile: “Yesu Kristo alishinda dhambi na kifo na ni mwenye nguvu. Yesu Kristo ni hai  kweli kweli” (Evangelii gaudium, 275). Yeye anataka hata sisi tuiishi, udugu na uwezo wa kukaribisha na kushirikisha tumaini hili. Katika mkutadha wa sasa, kuna haja ya dharura ya umisionari wa matumaini ambao kwa walioekwa wakfu na Bwana wawe na uwezo wa kukumbusha kinabii kuwa hakuna anayejiokoa mwenyewe. Kama Mitume na wakristo wa kwanza, hata sisi tusema kwa nguvu zetu zote “Kwa maana sisi hatuwezi kuacha kuyanena mambo tuliyoyaona na kuyasikia” (Mdo 4,20).  Yote ambayo tumepokea, yote ambayo Bwana ametujalia pole pole, alituzawadia ili tuthubutu na kutoa bure kwa wengine. Kama Mitume ambao waliona, walisikia na kugusa wokovu wa Yesu (1 Yh 1,1-4) ndivyo hata sisi leo hii tunaweza kugusa mwili wa mteswa na utukufu wa Kristo katika historia ya kila siku, na kupata ujasiri wa kushirikishana na wote hatima ya tumaini, na ile ambayo bila shaka inazaliwa kutokana kwamba tunatambua kuwa tumesindikizwa na Bwana. Kama Wakristo hatuwezi kumiliki Bwana kwa ajili yetu binafsi, Utume wa uinjilishaji wa Kanisa unaelezea wazi ufungamanishwaji na mabadiliko ya umma katika ulimwengu na katika ulinzi wa kazi ya uumbaji.

Mwaliko wa kila mmoja wetu:Tukumbuke kwa shukrani watu waliotoa ushuhuda 

Mada ya Siku ya Kimisionari Ulimwenguni mwaka huu, ni “Kwa maana sisi hatuwezi kuacha kuyanena mambo tuliyoyaona na kuyasikia” (Mdo 4,20). Ni mwaliko wa kila mmoja wetu kubeba mzigo na kufanya kutambua kile ambacho kimo moyoni. Utume huu daima umekuwa ni utambulisho wa Kanisa kwamba “upo kwa ajili ya kuinjilisha”(Evangelii nuntiandi, 14).  Maisha yetu ya imani yanadhoofika, yanapoteza unabii na uwezo wa kushangaa na shukrani hasa katika upekwe binafsi au kujifungia katika vikundi vidogo. Na kwa maana hiyo katika mwendo wake unahitahi ukuaji wa ufunguzi, wenye uwezo wa kufikia na kuwakumbatia wote. Wakristo wa kwanza katika kuzuia kuangukia katika vishawishi vya kujifungia binafsi na wenye kisomo, walivutiwa na Bwana na maisha ambayo Yeye alikuwa akiyatoa na kwenda katikati  ya watu na kushuhudia kile ambacho walikuwa wamekiona na kusikiliza kwamba  “Ufalme wa Mbingu huko karibu”. Walifanya kwa ukarimu, kwa shukrani na heshima inayofaa kwa wale wanaopanda wakijua kuwa wengine watakula matunda ya kujitolea kwao na sadaka yao. Papa Francisko kwa maana hiyo anapenda kufikiria kwamba hata wadhaifu, wenye vikwazo na majeruhi wanaweza kuwa wamisionari kwa namna yao, kwa sababu lazima na daima kuruhusu kuwa wema hata kama  upo udhaifu mwingi (Christus vivit, 239). Katika Siku ya Kimisionari Ulimwenguni, ambayo inaadhimisha kila mwaka, na kwa maana hiyo katika Dominika ya tarehe 24 Oktoba, Papa Francisko ameandika kuwa tukumbuke kwa shukrani watu wote ambao kwa ushuhuda wao wa maisha, wanatusaidia kupyaisha juhudi zetu za ubatizo, wa kuwa mitume wakarimu na wenye furaha ya Injili. Tukumbuke hasa wale ambao wamekuwa na uwezo wa kujikita katika safari, kuacha ardhi na familia zao ili Injili iweze kufika haraka bila kuchelewa na bila hofu katika kila kona za watu  na miji ambayo maisha mengi wanajikuta wana kiu ya baraka.

Bwana wa mavuno awatume wafanyakazi katika shamba lake

Kwa kutafakari ushuhuda wao wa kimisionari, unatuhimiza kuwa wajasiri na kusali bila kuchoka kwa “Bwana wa mavuno ili awatume wafanyakazi katika shamba lake”( Lk 10,2)” ; na hii ni kwa sababu tunao utambuzi kuwa wito wa kimisionari siyo jambo la wakati uliopita au kumbu kumbu ya kimapenzi  ya wakati mwingine. Leo hii Yesu anahitaji mioyo ambayo ina uwezo wa kushi wito kama historia ya kweli ya upendo, ambao unafanya kwenda pembezoni mwa ulimwengu na kuwa wajumbe na vyombo vya huruma. Huo ndiyo mwaliko ambao anawapatia kila mmoja japokuwa si mtindo ule ule. Tukumbuke kuwa kuna pembezoni zilizo karibu nasi, katikati ya mji au katika familia binafsi, Papa amebainisha. Kuna hata mantiki ya ufunguzi wa ulimwengu wa upendo ambao siyo wa kijografia bali wa maisha. Daima lakini hasa katika janga hili la corona ni muhimu kujongea na uwezo kila siku wa kupanua mzunguko wetu na kuwafikia wale ambao kwa haraka hatuhisi kuwa sehemu moja ya ulimwengu wetu japokuwa wanaishi karibu nasi( Ft 97). Kuishi utume ni kujitahidi kukuza hisia zile zile za Kristo Yesu na kuamini na Yeye ambaye yuko karibu nami  na ndiye kaka yangu na dada yangu.  Kwa kuhitimisha Papa Francisko anaomba kuwa upendo wa huruma uamshe hata ndani ya mioyo yetu na kutufanya kuwa wafuasi wa kimisionari. Maria Mfuasi wa kwanza wa kimisionari, atufanye tukuze sisi sote wabatizwa ile shauku ya kuwa chumbo na nuru ya dunia yetu” Mt 5,13-14).

UJUMBE WA PAPA SIKU YA KIMISIONARI 2021
29 January 2021, 12:00