Papa Francisko asikitishwa na maafa yaliyosababishwa na mabomu ya kujitoa mhanga nchini Iraq na kusababisha watu 32 kupoteza maisha na wengine 72 kupata majeraha makubwa. Papa Francisko asikitishwa na maafa yaliyosababishwa na mabomu ya kujitoa mhanga nchini Iraq na kusababisha watu 32 kupoteza maisha na wengine 72 kupata majeraha makubwa. 

Mabomu ya Kujitoa Mhanga Iraq: 32 Wamefariki dunia, 75 Majeruhi

Papa Francisko amemtumia salam za rambirambi Rais Barham Salih wa Iraq kuonesha masikitiko yake makubwa kutokana na mauaji ya watu wasiokuwa na hatia. Anasema, anaendelea kusali na kuwaombea wale wote waliopoteza maisha yao pamoja na familia zao, faraja na wagonjwa waweze kupona na kurejea tena katika shughuli zao. Anawaombea wahudumu wa kitengo cha dharura.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.

Mabomu mawili ya watu kujitoa mhanga siku ya Alhamisi, tarehe 21 Januari 2021 huko Baghdad nchini Iraq, yamepelekea watu zaidi ya 32 kupoteza maisha, na wengine zaidi ya 75 kupata majeraha makubwa pamoja na uharibifu wa miundo mbinu. Wachunguzi wa masuala ya ulinzi na usalama wanasema kwamba, hili ni tukio la aina yake kuwahi kutokea katika kipindi cha miaka miwili sasa, tangu Dola la Kiislamu nchini Syria na Iraq, ISIS kupoteza nguvu na mwelekeo nchini Iraq na Siria kunako mwaka 2019. Milipuko hii ni kati ya changamoto kubwa za ulinzi na usalama zinazoendelea kujitokeza tangu majeshi ya Marekani yalipojiondoa nchini Iraq wakati wa utawala wa Rais Donald Trump aliyeng’atuka kutoka madarakani, tarehe 20 Januari 2021. Ni katika muktadha huu, Baba Mtakatifu Francisko amemtumia salam za rambirambi Rais Barham Salih wa Iraq kuonesha masikitiko yake makubwa kutokana na mauaji ya watu wasiokuwa na hatia.

Salam hizi ambazo zimeandikwa kwa niaba yake na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican, Baba Mtakatifu anasema, anaendelea kusali na kuwaombea wale wote waliopoteza maisha yao pamoja na familia zao, faraja na wagonjwa waweze kupona na kurejea tena katika shughuli zao za kawaida. Anawaombea pia wahudumu katika kitengo cha dharura. Ni matumaini ya Baba Mtakatifu Francisko kwamba, wananchi wote wataendelea kujizatiti katika mchakato wa kushinda matumizi ya nguvu na kuanza kujielekeza zaidi katika ujenzi wa udugu wa kibinadamu, mshikamano na amani. Mwishoni, Baba Mtakatifu amewaombea watu wa Mungu nchini Iraq, baraka na neema zitokazo mbinguni. Itakumbukwa kwamba, Baba Mtakatifu kwa mwaka 2021 ametia nia ya kutembelea Iraq, ikiwa kama Mwenyezi Mungu atabariki nia hii njema!

Papa: Iraq

 

22 January 2021, 15:18