Tafuta

Papa Francisko ataadhimisha Ibada ya Misa katika fursa ya Siku kuu ya Mwili na Damu ya Yesu Jumapili 14 Juni 2020 katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro. Papa Francisko ataadhimisha Ibada ya Misa katika fursa ya Siku kuu ya Mwili na Damu ya Yesu Jumapili 14 Juni 2020 katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro. 

Papa Francisko:Maadhimisho ya Corpus Domini tarehe 14 Juni 2020!

Jumapili tarehe 14 Juni 2020, Papa Francisko anatarajia kuongoza ibada ya Misa Takatifu katika fursa ya maadhimisho ya Siku Kuu ya Mwili na Damu ya Yesu ‘Corpus Domini” katika Altare ya Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Karibia waamini 50 watashiriki katika maadhimisho hayo yatakayofanyika kuanzia saa 3.45 asubuhi majira ya Ulaya na kuhitimishwa kwa ibada ya kuabudu Ekaristi Takatifu na mwisho atabariki kwa Ekaristi hiyo.

Sr. Angela Rwezaula – Vatican

Papa Francisko anatarajia kuongoza ibada ya Misa Takatifu katika fursa ya maadhimisho ya Siku Kuu ya Mwili na Damu ya Yesu  au ‘Corpus Domini” katika Altare ya Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, tarehe 14 Juni 2020. Kwa mujibu wa msemaji mkuu wa masuala ya kiliturujia anasema karibia waamini 50 watashiriki katika maadhimisho hayo yatakayofanyika kuanzia saa 3.45 asubuhi majira ya Ulaya na kuhitimishwa kwa ibada ya kuabudu Ekaristi Takatifu na mwisho atabariki kwa Ekaristi hiyo. Ni tendo ambalo litarudia kama alivyokuwa akifanya kila siku kwenye Misa za Mtakatifu Marta, zilizokuwa  zinatangazwa moja kwa moja tangu tarehe 9 Machi hadi 17 Mei 2020, wakati wa kipindi ambacho nchini Italia na kwingineko hapakuwapo na uwezekano wa kuadhimisha misa na waamini kwa sababu ya janga la virusi vya corona.

Maadhimisho ya Papa Francisko

Mwaka jana Papa Francisko aliadhimisha Siku  kuu ya Mwili na Damu ya Yesu katika Uwanja wa Mtakatifu Maria Consolata kwenye mtaa wa Casal Bertone  Roma na kunako mwaka 2018 katika Parokia moja ya Mtakatifu Monika huko Ostia, Roma. Tangu 2013 hadi 2017 maadhimisho ya Misa yalikuwa yanafanyika katika Uwanja wa Mtakatifu Yohane Laterano na baadaye kufuata maandamano ya Ekaristi hadi katika Kanisa Kuu la Maria Mkuu Roma.

Asili ya Siku kuu hii

Mzizi wa Sherehe ya Sikukuu ya Mwili na Damu ya Yesu au Corpus Domini, inaanzia mbali katika karne ya XIII. Kunako mwaka 1215 Mtaguso wa IV wa Laterano ulithibitisha ukweli wa uwepo wa Kristo katika Ekaristi, na baadaye katika Mtaguso wa  Trento kunako 1551 ukadhihirisha kabisa  kwamba  kwa kubariki  mkate na divai ubadilishwa kabisa ule mkate kuwa Mwili wa Kristo na  divai kuwa kweli  Damu yake. Huko Ubelgiji, baada ya kufuatia uzoefu wa ajabu wa Mtakatifu Juliana wa Cornillon, sherehe hii ilianzishwa kunako 1247 katika sikukuu mahalia kwenye mji wa Liègi. Baada ya miaka michache, kunako mwaka 1263, Padre  mmoja wa  Bohemia ambaye alifika Bolsena akiwa anasumbuliwa na shaka juu ya uwepo halisi wa Yesu, wakati wa kuadhimisha Misa yake na hasa alipofikia  wakati wa matoleo ya kumega mkate, aliona  matone machache ya damu yakitoka katika Ostia hiyo. Baada ya tukio hilo, Papa Urban IV aliamua kunako mwaka 1264 kulipanua tukio hili la maadhimisho  katika Kanisa lote ulimwenguni katika Siku kuu ya Mwili na Damu ya Yesu au ‘Corpus Domini’ katika luhja ya kilatino.

08 June 2020, 15:02