Virusi vya Corona: Vatican yasitisha shughuli za Mahakama
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.
Baba Mtakatifu Francisko kwa kusoma alama za nyakati sanjari na kuzingatia hali halisi ya mlipuko wa Virusi vya Corona, COVID-19 na athari zake katika jamii, ameamua kuanzia tarehe 18 Machi 2020, kusimamisha shughuli zote za Mahakama za Vatican, hadi hapo tarehe 3 Aprili 2020. Tahadhari hii imekwisha kuchukuliwa pia na Serikali ya Italia. Lakini, shughuli za uchunguzi wa makosa mbali mbali zitaendelea kama kawaida. Pamoja na kuzingatia kanuni, masharti na itifaki ya kupambana na Virusi vya Corona, COVID-19, shughuli za dharura Kimahakama zinaweza kuendelea kwa ruhusa ya Rais wa Mahakama, kwa kuratibu muda wa kuingia na kutoka.
Agizo hili kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko, limetolewa na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican kwa vyombo vya mawasiliano ya jamii. Virusi vya Corona, COVID-19 vinaendelea kusababisha majanga makubwa pamoja na kugumisha maisha ya watu wengi duniani!