Sherehe ya Noeli ya Bwana: Iweni mashuhuda wa matumaini duniani!
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.
Baba Mtakatifu Francisko wakati wa kutoa salam zake kwa mji wa Roma na Ulimwengu katika ujumla wake, “Urbi et Orbi” kwa Noeli ya Mwaka 2019, alikua ameambatana na Kardinali Konrad Krajewski, Mtunza sadaka ya Kipapa pamoja na Kardinali Renato Raffaele Martino, Rais Mstaafu wa Baraza la Kipapa la haki na amani pamoja na Baraza la Kipapa kwa ajili ya shughuli za kichungaji kwa wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum. Baba Mtakatifu ametumia fursa hii kuwatakia watu wote heri na baraka kwa Sherehe ya Noeli ya Bwana. Amewakumbuka hata wale waliokuwa wamejiunga naye kwa njia ya vyombo mbali mbali vya mawasiliano ya jamii.
Hawa ni waamini, mahujaji na wageni kutoka sehemu mbali mbali za dunia waliokuwa kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Baba Mtakatifu amewashukuru na kuwapongeza kwa uwepo na ushiriki wao katika Sherehe hii ya Noeli, siku ya furaha. Watu wote wanaitwa kutoa ushuhuda wa matumaini duniani, kwa kutangaza kwa maneno, lakini zaidi kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao, kwamba, Kristo Yesu ambaye ni amani yao, amezaliwa kati yao. Mwishoni, amewaomba waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kuendelea kumsindikiza kwa sala na sadaka zao katika maisha na utume wake ka Khalifa wa Mtakatifu Petro.