Kongamano la Ekaristi Kimataifa Budapest 13-20 Septemba 2020!
Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican
Mara baada ya tafakari ya Neno la Mungu na sala ya Malaika wa Bwana, Jumapili tarehe 15 Desemba 2019, kwa mahujaji na waamini waliounganika katika kiwanja cha Mtakatifu Petro, Baba Mtakatifu Francisko amewasalimia watu waMungu wote ikiwa ni familia nyingi, makundi ya maparokia, vyama mbalimbali waliofika kutoka Italia na sehemu mbalimbali ya dunia. Baba Mtakatifu amesema kwamba wakati wanajiandaa na matukio ya sherehe za Kuzaliwa kwa Bwana wote wanaalikwa kujiandaa vema hasa katika safari ya unyenyekevu wa Yesu, Mungu aliyefanya mtu ili kuweza kukutana na kila mmoja wetu. Na kwa kufanya hivyo ni kupata kugundua kuwa Yeye anatupenda na kuungana nasi kwa sababu hili ili na sisi tuweze kuungana na Yeye(Waraka wa Admirabile signum,1).
Kongamano la Ekaristi Kimataifa huko Budapest, 13-20 Septemba 2020
Aidha Baba Mtakatifu ametangaza kwamba kuanzia tarehe 13 hadi 20 Septemba 2020, wataadhimisha jijini Budapest nchini Romania “Kongamano la 52 la Ekaristi Takatifu Kimataifa”. Kongamano la Ekaristi linafanyika sasa zaidi ya nusu karne hasa ikiwa na maana ya kukumbusha kuwa katika kiini cha maisha ya Kanisa ipo Ekaristi! Kaulimbiu inayoongoza Kongamano hilo itakuwa ni “Chanzo chetu ni kwako kutoka katika kifungu cha (Zab 87,7). Kwa maana hiyo Baba Mtakatifu Francisko ameomba kwamba: “tusali kwa ajili ya tukio hili la Ekaristi huko Budapest ili liweze kusaidia Jumuiya za kikristo katika mchakato wa upyaisho. » (Hotuba ya Papa kwa Kamati ya Maandalizi ya Kongamano la Ekaristi Kimataifa,10 Novemba 2018). Na kwa wote amewatakia Domika njema na Novena njema ya Kuzaliwa kwa Bwana. Watoto wote wapeleke mtoto Yesu katika pango na wasisahau kusali kwa ajili yake.