Ukiona sanamu ya mtoto Yesu aliyefungua mikono yake, ina maana kwamba Mungu alikuja kwa ajili ya kukumbatia ubinadamu wote Ukiona sanamu ya mtoto Yesu aliyefungua mikono yake, ina maana kwamba Mungu alikuja kwa ajili ya kukumbatia ubinadamu wote 

Baba Mtakatifu:Pango ni picha ya ufundi wa amani ni vema kuitengeneza nyumbani!

Baba Mtakatifu Francisko wakati wa katekesi tarehe 18 Desemba 2019 kwa mahujaji na waamini waliounganika katika ukumbi wa Paulo VI amewakumbusha kuwa iwapo maisha yetu yanazaliwa kwa upya ndiyo sikukuu ya Kuzaliwa kwa Bwana kweli.Kwa maana hiyo ni muhimu kutengeneza Pango ndani ya nyumba ili kugundua kwa tafakari ya kuwa Mungu anaishi karibu nasi na siyo kwamba haonekani!

Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican

Baada ya wiki moja itakuwa ni sikukuu ya kuzaliwa kwa Bwana. Katika siku hizi  wakati wa kufanya maandalizi ya sikukuu, tunaweza kujiuliza: je ninajiandaa namna gani kwa ajili ya sikukuu ya kuzaliwa? Ni kwa nmna rahisi lakini ya dhati ya kujiandaa  hasa ni kutengeneza pango. Hata mimi mwaka huu nimefuata njia hii. Nimekwenda Greccio, mahali ambapo Mtakatifu Francisko wa Assisi alifanya Pango la kwanza na watu wa sehemu hiyo. Na niliandika barua kwa ajili ya kukumbusha maana ya utamaduni huu, nini maana ya pango katika kipindi cha Siku Kuu ya kuzaliwa kwa Bwana. Ndiyo mwanzo wa tafakari ya Baba Mtakatifu Francisko wakati wa katekesi yake kwa waamini na mahujaji waliofika katika uwanja wa Mtakatifu Petro Jumatano tarehe 18 Desemba 2019. Kabla ya kuanza katekesi yake, imesoma Injili ya Mtakatifu Luka 2, 15-16 isemayo kwamba “Ikawa, malaika hao walipoondoka kwenda zao mbinguni, wale wachungaji waliambiana, Haya,na twendeni mpaka Bethlehemu, tukalione hilo lililofanyika, alilotujulisha Bwana. Wakaenda kwa haraka wakamkuta Mariamu na Yusufu, na yule mtoto mchanga amelala horini.

Peleka Injili katika maeneo yote:shuleni,magerezani, mahospitalini na viwanjani

Baba Mtakatifu Francisko akiendelea na tafakari yake amesema kuwa hori kwa hakika ni kama Injili hai (Rej barua ya Admirabile signum, 1). Peleka Injili katika maeneo ambayo wanaishi. Katika nyumba shuleni, katika maneeo ya kazi na makutano, katika mahospitali na katika nyumba za utunzaji, katika magereza na katika uwanja mbalimbali. Na mahali pale tunapoishi inatukumbusha jambo moja msingi kwamba Mungu hakubaki bila kuonekana mbinguni, lakini alikuja duniani na kujifanya mtu, mtoto. Kutengeneza pango ni kuadhimisha ule ukaribu wa Mungu. Mungu daima amekuwa karibu na watu wake lakini hasa alipojifanya mtu na kuzaliwa alikuwa karibu sana. Kutengeneza pango ni kuadhimisha ukaribu wa Mungu ni kugundua kwa upya kuwa Mungu ni wa kweli na wa thati, anaishi na mapigo ya moyo wake.  Mungu siyo wa mbali sana au kama hakimu aliye mbali, lakini ni upendo mnyenyekevu, aliyeshuka hadi kwetu akatufikia. Mtoto horini anatuonesha huruma yake.

Baadhi ya sanamu zinazo mwonesha mtoto na mikono iliyofunguliwa ni kwa ajili ya kutueleza kuwa Mungu amekuja kukumbatia ubinadamu wetu. Kwa maana hiyo ni vema kukaa mbele ya pango na kumkabidhi Bwana maisha yetu na  kumwelezea juu ya watu na hali halisi tulizo nazo ndani ya mioyo yetu aidha  kufanya naye tathmini za mwaka ambao tunakaribia kuumaliza, kushirikishana matarajio na wasiwasi.  Kandoni mwa Yesu Baba Mtakatifu Francisko amesema, “tunamwoana Mama Maria na Mtakatifu Yosefu. Tunaweza kufikiria mawazo na hisia walizokuwa nazo wakati Mtoto anazaliwa katika umaskini, bila shaka ilikuwa ni furaha  lakini pia na mshangao mkubwa. Lakini pia  Baba Mtakatifu Francisko amethibitisha kwamba, “tunaweza  hata kuwaalika Familia Takatifu kuwa nyumbani mwetu, mahali ambapo kuna furaha na mashaka, mahali ambapo kila siku tunaamka, tunakula na tuko karibu na watu wapendwa zaidi.

Pango ni Injili hai ya nyumbani na ni la wakati wa sasa katika familia

Baba Mtakatifu Francisko akiendelea na tafakari yake amethibitisha kwamba hori au pango ni Injili hai ya nyumbani. Neno pango kwa kuelezea maana yake ni horini, wakati mji wa pango, Bethlehemu maana yake  ni “nyumba ya mkate”. Horini na nyumba ya Mkate, ni pango tunalofanya nyumbani mahali ambapo tunashirikishana chakula na upendo, vyote hivyo vinatukumbusha kuwa Yesu ni chakula, mkate wa maisha ( Yh 6,34). Ni yeye anayerutubisha upendo wetu; ni Yeye anatoa nguvu za kwenda mbele na kusamehe katika familia zetu. Pango linatoa fursa nyingine ya mafundisho ya maisha, anathibtisha Baba Mtakatifu. Katika ukawaida wa maisha yetu ya kukimbizana leo hii, huu ni mwaliko wa kutafakari kwa kina. Pango linatukumbusha umuhimu wa kusimama. Na hii ni kutokana na kwamba tutakapo tambua tu  kujiundia nafasi ya kusimama, tutaweza kupokea kile kile chenye maana katika maisha yetu.  Ni kwa njia ya kuacha nje ya nyumba na kelele za dunia hii tu ili kujifungulia katika usikivu wa Mungu ambaye anazungumza nasi katika ukimya. Pango ni la wakati wa sasa, ni la la wakati wa sasa katika kila familia. Baba Mtakatifu Francisko amesisitiza na kuendelea kusema kuwa tarehe 17 Desemba amezawadiwa picha ya pango maalum iliyo ndogo, inayoitwa “ Tumwache mama apumzike”.  Picha hii ilikuwa inaonesha mama aliye lala na Yosefu akiwa na mtoto hapo hapi  akiwa anambeleleza alale.  Baba Mtakatifu Francisko ameuliza swali: “ je ni wangapi kati yenu wanapaswa kushirikishana usiku kati ya mme na mke kwa ajili ya mtoto kike au kiume anayelia lia sana”. “Tumwache mama apumzuke ndiyo huruma ya familia, na ya ndoa”, Baba Mtakatifu amesisitiza!

Pangoni anaonekana fundi wa amani na hivyo ni Injili iliyo hai

Baba Mtakatifu Francisko katika  tafakari yake amesema kwamba pango  ni muhimu sana katika nyakati za sasa, wakati kila siku duniani wanaendelea kutengeneza silaha nyingi na sura nyingi za vurugu, zinazonguka katika macho  na ndani ya mioyo yetu. Kinyumbe na Pango ni kwamba inajionesha picha ya fundi wa amani. Kwa maana hiyo ni Injili hai na katika  kuanzia horini, ndipo tunaweza kupokea hatimaye mafundisho kuhusu maana hiyo hiyo ya maisha! Tunaona kila siku matukio mbalimbali katika hori. Wachungaji wakiwa na kondoo, wahunzi ambao wanachoma vyuma vyao, wanaosaga unga kwa ajili ya kutengeneza mkate,  na wakati mwingine katika pango wanaweka hata maeneo mbalimbali kuonesha hali halisi zinazowazunguka katika eneo mahalia. Ni haki kufanya hivyo kwa sababu pango linatukumbusha kuwa Yesu anakuja katika maisha yetu halisi.

Hiyo ni muhimu anasisitiza Baba Mtakatifu! Kutengeneza pango dogo nyumbani  ni muhimu  daima kwa sababu linakumbusha kuwa Mungu alikuja kwetu na anazaliwa kwetu, anatusindikiza katika maisha, ni mtu kama sisi alijifanya mtu kama sisi. Katika maisha yetu ya kila siku sisi siyo peke yetu, Yeye anaishi nasi. Yeye habadilishi vitu kama mazingaombwe, lakini iwapo tunampokea kila kitu kinaweza kubadilika. Baba Mtakatifu Francisko amehitimisha kwa kuwatakia matashi mema ya kutengeneza pango na kwamba iwe fursa kwa ajili ya kumkaribisha Yesu katika maisha.  Tunapotengeneza pango nyubani ni kama kufungua mlango na kusema “ Yesu ingia” ni kufangua ukaribu hai  wa dhati na ndiyo mwaliko wa Yesu  ili aweze kuja katika maisha yetu. Kwa sababu iwapo yeye anaishi katika maisha, maisha hayo yanazaliwa kwa upya. Iwapo maisha yanazaliwa kwa upya kiukweli ndiyo siku kukuu ya kuzaliwa kwa Bwana. Ninawawatakia Sikukuu ya kuzaliwa kwa Bwana ninyi nyote!

Shukrani nyingi kutoka kwa Papa kwa ajili ya wote waliomtakia matashi mema ya Jibilei ya miaka 50 ya upadre na siku ya  kuzaliwa kwake

Baba Mtakatifu Francisko amewashukuru sana kwa wale wote waliomtakia matashi meme kutoka duniani nzima, waliotuma pia ujumbe kwa ajili ya jubilei ya miaka 50 tangu apatiwe daraja takatifu la upadre. Hayo yote ameeleza mara baada ya kumaliza katekesi yake ya kila jumatano. Hata hivyo katika ukumbi wa Paulo wa VI amekaribishwa kwa vigelegele na shangwe kubwa kwa watu elfu saba walio kuwa kwenye ukumbu huo wakati akiwapungia mikono na salam na kuwabusu watoto wadogo wengi!

18 December 2019, 12:22