Papa atuma salamu za rambirambi kufuatia na kifo cha rais mstaafu Chirac wa Ufaransa
Na Sr. Angela Rwezaula - Vatican
Baba Mtakatifu Francisko katika salam za rambi rambi kufuatia kifo cha aliyekuwa Rais wa Ufransa Bwana Jacques Chirac kilichotokea tarehe 26 Septemba 2019, anaonesha masikitiko makubwa na kumpa pole Rais Macron, serikali yake na watu wote wa Ufaransa. Anasali kwa Mungu ili ampokee katika hali ya amani, wakati huo huo anawapa faraja na matumaini wale wote ambao wamejaribiwa na wanaomboleza kifo chake, hasa mke wake na familia nzima. Bwana abariki Ufaransa na raia wote wa Ufaransa.
Salam za rambi rambi kutoka kwa maaskofu wa ufaransa
Katika ujumbe wa salamu za rambi rambi uliotumwa kwa Bi Chirac na familia yake, maaskofu wa Ufaransa wanaandika kuwa, Rais mstaafu Bwana Jacques Chirac ameacha alama ya mkakati wake kwa watu wa Ufaransa, mtindo wake wa kukutana kibinadamu na uwezo wake wa kukabiliana na matatizo. Mbali na hotuba zake za kisiasa, katika mchakato wa shughuli yake ya muda mrefu, amekumbana na changamoto zilizosababishwa na uchumi, mabadiliko ya dunia kabla na baada ya mwaka 1989 Ulaya na mabara mengine, uchaguzi wa maisha binafsi kijamii na ulazima wa maendeleo ya kiteknolojia. Baraza la maaskofu katoliki wa Ufaransa hata hivyo wataungana wote katika Misa ya mazishi ya Rais Mstaafu Chirac, kuweza kukaa karibu na familia yake na raia wote wa ufaransa, ili kukumbuka huduma ya ukarimu wake kwa nchi na kumkabidhi marehemu Chirac katika mwanga wa Mungu wa huruma ambaye anaona kwa kina ndani ya mioyo.