Papa Francisko: likizo ni wakati wa kufurahia pamoja na familia!
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.
Hija ya Kanisa; Utayari na Maamuzi ya busara ni mambo msingi katika maisha, kama njia ya kuwa mfuasi amini wa Kristo Yesu. Hivi ndivyo alivyokazia Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Jumapili tarehe 30 Juni 2019. Mara baada ya Sala ya Malaika wa Bwana, Baba Mtakatifu Francisko amewatakia wafanyakazi wote mapumziko mema ya kipindi cha kiangazi. Iwe ni fursa ya kufurahia pamoja na familia zao.
Baba Mtakatifu amewakumbuka na kuwaombea wale wote ambao katika kipindi hiki cha kiangazi wameathirika kutokana na kuongezeka kwa kiwango cha joto sehemu mbali mbali za dunia. Baba Mtakatifu anawakumbuka wagonjwa, wazee na wafanyakazi ambao wanapaswa kuendelea kutekeleza dhamana na utume wao hata katika mazingira ya joto kali, katika maeneo ya uwazi, ili kwamba, hasiwepo mtu anaye watelekeza au kuwanyonya! Mwishoni, Baba Mtakatifu amewatakia heri waamini na mahujaji wote kutoka ndani na nje ya Italia waliohudhuria kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Wote hawa amewatakia Jumapili njema.