Yesu hakuja kuhukumu.Anatoa fursa ya kujipyaisha maisha yetu!
Na Sr. Angela Rwezaula - Vatican
Ikiwa ni Dominika ya tano ya Kwaresima na ya mwisho kabla ya kuanza Wiki Kuu, tarehe 7 Aprili 2019, Baba Mtakatifu Francisko ametoa tafakari yake kabla ya sala ya Malaika wa Bwana kwa waamini na mahujaji wote walio unganika katika kiwanja cha Mtakatifu Petro mjini Vatican. Baba Mtakatifu akianza tafakari hiyo anasema: katika Dominika ya tano ya Kwaresima, liturujia inawakilisha tukio la mwanamke mzinzi (Yh 8,1-11). Historia hii inatofautiana kwa mitazamo mawili: ya waandishi na Mafarisayo, na ule wa Yesu upande mwingine. Mtazamo wa kwanza, wao wanataka kumhukumu mwanamke, kwa sababu wanajihisi kuwa walezi na ili kubaki katika kutimiza uaminifu wa Sheria. Badala yake, Yesu anataka kumwokoa, kwa sababu yeye binafsi ni huruma ya Mungu ambaye kwa kusamehe, anamwondolea na kupyaisha kwa njia ya mapatano. Yesu alipokuwa anafundisha tena hekaluni, “Waandishi na Mafarisayo wakamletea mwanamke aliyefumaniwa katika uzinzi, wakamweka katikati. Wakamwambia kama wampige kwa mawe kwa mujibu wa torati ya Musa”.
Yesu alikuja duniani kuokoa na wala si kuhukumu
Mwinjili anathibitisha kabisa kwamba: “walisema neno hilo wakimjaribu, ili wapate sababu ya kumshitaki.”. Baba Mtakatifu anaongeza kusema: tazama ubaya wa watu hawa, iwapo anagesema hapana, ilikuwa ni sababu ya kumhukumu Yesu kwa kukosa utii wa torati ya Musa. Na iwapo angeitikia ndiyo, ilikuwa ni kuwashitaki viongozi wa Kirumi, mbao walikuwa wanahifadhi hukumu na hawakukubali umaarufu. Na Yesu lazima ajibu. Kutokana na hili inaonesha wazi kwamba wapinzani wa Yesu wamefungwa katika vikwazo vilivyo finyu vya sheria na wanataka kumfunga Mwana wa Mungu kwa mtazamo wa shutumu na hukumu. Lakini Yesu hakuja ulimwenguni kama hakimu na kuhukumu, bali kuokoa na kuwapa watu maisha mapya. Baba Mtakatifu anauliza swali, je mbele ya jaribio hili, Yesu anafanya nini? Hawali ya yote, anabaki kidogo kwa kimya, anainama na kuandika kwa kidole chake ardhini na zaidi ni kama kutaka kukumbusha kuwa, aliye mwanasheria peke yake na Hakimu ni Mungu ambaye alikuwa ameandika Sheria juu ya jiwe. Na baadaye alijiinua, akawaambia, “Yeye asiye na dhambi miongoni mwenu na awe wa kwanza wa kumtupia jiwe”. Kwa njia hiyo, Yesu anatoa tamko katika dhamiri ya watu hao. Wao walikuwa wanahisi kuwa “mabingwa wa haki”, lakini yeye anawaalika kuwa na utambuzi wa hali zao za kidhambi za kibinadamu, ambapo hawawezi kujisifu kuwa na haki ya maisha au kifo cha wenzao wanao fanana nao!
Dhamiri inashitaki na wanatawanyika mmoja mmoja kuanzia wazee
Kutokana na hiyo walishitakiwa na dhamiri zao, wakatoka mmoja mmoja, wakianzia tangu wazee hata wa mwisho wao, yaani wale ambao ni wataalam zaidi wa dhambi zao waliondoka wote na kuacha kimpiga mawe mwanamke. Baba Mtakatifua anasema, tukio hili, linamkaribisha kila mmoja wetu kuwa na ufahamu kwamba sisi ni wenye dhambi na lazima kuruhusu mawe yaanguke kutoka mikono mwetu na ili kuacha tabia za kuhamasisha na kuhukumu wengine, tabia za masengenyo na ambayo wakati mwingine tunapenda kuwatupia wengine. Tunapo wasengenya wengine ni kuwatupia mawe na tunafanana na watu hawa! Mwisho walibaki Yesu na mwanamke katikati. Dhambi na huruma anasema Mtakatifu Agostino. Ni Yesu peke yake asiye kuwa na dhambi na mbaye angeweza kutupa jiwe dhidi yake, lakini hakufanya hivyo, kwa sababu Mungu hataki kifo cha mdhambi, bali anaye ongoka na kuishi (taz. Ez 33,11). Yesu anamuaga mwanamke na maneno mazuri sana, Baba Mtakatifu anasema; “Enenda zako; wala usitende dhambi tena”. Na kwa maana hiyo Yesu anafungulia mwanamke mbele, njia mpya, iliyoundwa na huruma, njia ambayo inamtaka awajibike na asitenda dhambi tena. Ni mwaliko ambao unawahusu watu wote, yaani sisi sote! Yesu anapotusamehe anatufungulia daima njia mpya ya kwenda mbele. Katika kipindi hiki cha Kwaresima, tunaitwa kujitambua wadhambi na kuomba msamaha wa Mungu.
Wakati wa kujipatanisha msamaha unaleta amani
Baba Mtakatifu Francisko anathibitisha kwamba wakati wa kujipatanisha kwa mara nyingine tena, msamaha unatupatia amani na kutufanya tuanze historia iliyopyaishwa. Kila uongofu wa kweli ni matazamio ya wakati mpya wa maisha mapya, maisha mazuri na maisha yaliyo huru dhidi ya dhambi na kuwa na maisha ya ukarimu. Hatuna hofu ya kuomba msamaha kwa Yesu, kwa sababu yeye anatufungulia mlango wa maisha mapya. Bikira Maria atusaidie kushuhudia wote upendo wa uhuruma ya Mungu ambaye ni katika Kristo anaye tusamehe na kufanya maisha yetu yawe mapya, akitoa fursa na uwezekano mpya wa kujipyaisha daima!
Mara baada ya sala ya Malaika wa Bwana 7.4.2019
Mara baada ya tafakari na sala ya Malaika wa Bwana, Baba Mtakatifu Francisko amewasalimia waamini na wote mahujaji kutoka pande zote za dunia, zaidi kama vile wanafunzi kutoka nchi ya Austria na Ufaransa. Aidha wanafunzi kutoka Bologna Genova, hata Torino na Vercelli. Wazo limewaendea vijana wa kipaimara kutoka Settignano, Scandicci, na wengine kutoka jimbo la Saluzzo,Italia waliosindikizwa na Askofu wao Cristiano Bodo. Anawataka wote wawe wajasiri katika ushuhuda wa Yesu na Injili. Kwa kupokea kipaimara wanapaswa wakue daima kwa ujasiri na wawe wajasiri. Amewakumbuka vijana wengine wadogo wenye umri wa miaka 14 kutoka Milano, waamini kutoka Pescara, Napoli na Terni. Kwa wote amewatakia Dominika njema na zaidi wasisahau kusali kwa ajili yake.