PASAKA YA BWANA 2019:Ukaribu wa kiroho wa Papa kwa waathirika wa Sri Lanka
Na Sr. Angela Rwezaula- Vatican
Mara baada ya Sala ya Malkia wa Mbingu, tarehe 22 Aprili 2019, Baba Mtakatifu kwa upya amerudia kuonesha ukaribu wa kiroho na ubaba kwa watu wa Sri Lanka. Anaeleze ukaribu huo hata kwa Kardinali Malcolm Ranjith Patabendige Don na kwa Kanisa Kuu Katoliki la Colombo. Anasali kwa ajili ya waathirika na majeruhi na kuwaomba watu wote wasisite kutoa msaada muhimu. Na zaidi ni matarajio yake kuwa watu wote waweze kulaani matendo haya ya kigaidi ambayo ni matendo yasiyo ya kibinadamu na hayawezi kabisa kukubaliwa! Na mwisho amesali sala ya Salam Maria kwa ajili yao...
Salam mbalimbali kwa mahujaji wote toka pande za dunia
Baba Mtakatifu Francisko katika hali halisi ya siku ya furaha hiyo anawasalimia kwa upendo familia na makundi yote ya parokia, vyama na mahujaji wote waliofika kutoka Italia na kila kona ya Dunia . Kwa kila mmoja anamtakia mema, kuishi kwa imani kuu katika siku nane za Sikukuu ya Pasaka ambayo inarefushwa kwa kufanya kumbukumbu ya Ufufuko wa Kristo. Amewashauri wachukue fursa hii ya kuwa mashuhuda wa furaha na amani ya Bwana Mfufuka.