Papa na amani kati ya Korea mbili:Muwe na uvumilivu ili kushinda migawanyiko!

Tarehe 27 Aprili 2019,Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake wakati wa fursa ya kumbu kumbu ya mwaka wa kwanza tangu kutiwa sahini ya Azimio la Panmunjon,anasisitiza amani,matumaini na muungano wa Peninsula ya Korea!

Na Sr. Angela Rwezaula - Vatican

Ikiwa ni mwaka wa kwanza wa kihistoria kuhusu mkutano kati ya viongozi wawili wa Korea ya Kaskazini Bwana, Kim Jong-un na Rais wa Korea ya Kusini Bwana Moon Jae-in, uliofanyika katika kijiji cha Panmunjon,mpakani mwa nchi hizi mbili, Baba Mtakatifu Francisko tarehe 27 Aprili 2019 ametuma ujumbe wake kwa njia ya video akiwapa salama nyingi za upendo na kuwakumbusha juu ya sahini ya Mkataba wa amani, matumaini na muungano wa Peninsula ya Korea.

Mkutano wa Panmunjom kwa ajili ya amani,matumaini na muungano

Katika ujumbe wake kwa njia ya video, Baba Mtakatifu anasema: Marafiki wapendwa, ninayo furaha ya kuwatumia salam za upendo katika mwaka huu wa kwanza wa kutiwa saini ya Mkataba wa Panmunjom kwa ajili ya amani, matumaini na muungano wa Peninsula ya Korea. Hali kadhalika Baba Mtakatifu anahimiza kutafuta maelewano na mapatano kwamba: Maadhimisho haya yanaweza kutoa fursa kwa wote matumaini ambayo yanasimama juu ya umoja, mazungumzo na juu ya mshikamano kidugu ambao uwe halisi na kweli. Kwa njia ya jitihada za uvumilivu na kuhimimili, katika kutafuta maelewano na mapatano, mambo ambayo yanawezesha kushinda migawanyiko na upinzani.

Sala kwa ajili ya azimio hili liweze kuleta wakati mpya

Hatimaye katika ujumbe wake kwa njia ya video Baba Mtakatifu Francisko anasali kwa ajili ya azimio hili kwamba: Ninaomba ili maadhimisho haya ya Azimio la Panmunjom yaweze kuleta wakati mpya wa amani kwa Wakorea wote. Na kwa ajili yenu nyote ninawaombea wingi wa baraka za Mungu.

27 April 2019, 12:40