Papa Fancisko amewaomba vijana wasali Rosari kwa ajili ya amani na kusoma wosia "Christus vivit"
Na Sr Angela Rwezaula - Vatican
Tarehe 14 Aprili 2019 Baba Mtakatifu Francisko mara baada ya maadhimisho ya Jumapili ya Matawi, ikiwa ni mwanzo wa maadhimisho ya Juma Kuu Takatifu, Kanisa linapofanya kumbu kumbu ya Mateso, kifo na Ufufuko wa Kristo na siku ambayo inakwenda sambamba na Maadhimisho ya XXXIV ya Vijana Duniani na ambayo imeadhimishwa kijimbo, Baba Mtakatifu Francisko amewasalimia wote wanaoshiriki katika maadhimisho hayo, lakini pia hata waliokuwa wakifuata kwa njia ya vyombo mbalimbali vya mawasiliano. Baba Mtakatifu amewafikiria hata vijana wote wakiwa karibu na maaskofu wao katika majimbo wakiadhisha Siku ya vijana katika kila jimbo duniani kote.
Vijana someni Wosia wa Christus vivit
Baba Mtakatifu Fancisko akiwageukia vijana katika maadhimisho hayo anawaalika waishi kila siku kwa mujibu wa maelekezo ya Wosia wa hivi karibuni wa kitume Christus vivit yaani Kristo anaishi, na kwamba ni tunda la Sinodi ambayo iliwahusisha hata vijana wenzao. Katika waraka huo kila mmoja anaweza kupata neno lenye kuzaa katika maisha binafsi na kwa ajili ya kukua katika safari ya imani na huduma kwa ndugu.
Zawadi ya Rosari
Kwa mantiki ya Jumapili hiyo Baba Mtakatifu ametoa zawadi kwa wote waliofikia katika uwanja wa Mtakatifu Petro, Rosari ya mti wa mizeituni ambazo zilitengenezwa katika nchi Takatifu, wakati wafursa ya Mkutano wa Vijana duniani huko Panama mwezi Januari na kwa ajili ya Siku ya hii. Na kwa maana hiyo Baba Mtakatifu amependa kupyaisha “wito” wake kwa vijana kusali Rosari, kwa ajili ya amani, kwa namna ya pekee, amani katika Nchi Takatifu na nchi zote za Mashariki. Amehitimisha akiomba wote wamwelekee Bikira Maria ili aweze kusaida kuishi vema Juma Takatifu.