Ujumbe wa Papa kwa njia ya Video kwa wananchi Morocco!
Na Sr. Angela Rwezaula - Vatican
Kabla ya ziara ya Baba Mtakatifu Francisko ya siku mbili 30-31 Machi kuitembelea nchini Morocco, kama kawaida yake kila mara kabla ya ziara, kwa mara nyingine tena, tarehe 28 Machi 2019 ametuma ujumbe wake kwa njia ya video kwa watu wa Morocco. Ujumbe wake kwa njia ya video unaanza na As-Salamu Alaikum! Amani iwe kwenu na kuendelea kusema kwamba, muda mfupi ataitembelea nchi yao pendwa kwa ziara ya siku mbili. Anamshukuru Mungu kwa kumpatia fursa hiyo. Vile vile anaonesha furaha yake ya kuweza kukutana na Mfalme Mohammed VI ambaye kwa ukarimu wake ametoa mwaliko huo na viongozi wa Morocco kwa ushirikiano wao wa dhati.
Baba Mtakatifu Francisko anasema, kwa kufuata nyayo za mfuasi wake Yohane Paulo II, anakwenda kama mhujaji wa amani na udugu, ambao unahitajika sana katika dunia.Aidha anathibtisha kwamba,kama wakristo na waislam wanaamini katika Mungu mmoja Muumbaji na wa huruma ambaye aliumba watu na kuwapatia dunia ambayo wanaishi ndugu wote, katika kuheshimiana tofauti na kusaidiana katika mahitaji. Yeye aliwakabidhi wao ardhi na nyumba yetu ya pamoja ili kuilinda kwa uwajibikaji na kuitunza kwa ajili ya kizazi kijacho.
Kwa mana hiyo Baba Mtakatifu anaongeza kusema, itakuwa furaha kubwa kwake, pia kushirikishana moja kwa moja misingi hiyo aliyoitaja katika mkutano utakaofanyika huko Rabat. Na zaidi katika safari hii itakuwa kwake fursa kubwa ya kutembelea jumuiya ya kikristo iliyopo nchini Morocco, ili kuwatia moyo katika safari yao. Na kama itakavyo kuwa ile ya kukutana na wahamiaji, ambao anathibitisha, wanawakilisha watu katika kujenga kwa pamoja dunia ya haki na yenye mshikamano. Kwa kuhitimisha, anawashukuru wazalendo wote wa Marocco kwa moyo wote kuanzia sasa kwa ajili ya makaribisho yao wanayo msubiri na zaidi kwa ajili ya sala zao, akiwahakikishia naye kuombea nchi yao pendevu.