Hija ya Papa Francisko Morocco: Achonga na waandishi wa habari
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.
Baba Mtakatifu Francisko akiwa njiani kuelekea nchini Morocco, Jumamosi, tarehe 30 Machi 2019 amepata nafasi ya “kuchonga” kidogo na waandishi wa habari 69 walioko kwenye msafara wake kwa kuwatakia heri na nafaka katika kazi yao. Akimkaribisha Baba Mtakatifu Francisko kuzungumza na waandishi wa habari Dr. Alessandro Gisotti, Msemaji mkuu wa mpito mjini Vatica amekumbushia Hati ya Udugu wa Kibinadamu iliyotiwa mkwaju kati yake na Dr. Ahmad Al-Tayyib, Imam Mkuu wa Msikiti wa Al- Azhar, ulioko Kairo, nchini Misri, Jumatatu, tarehe 4 Februari 2019.
Hati hii ni kama nguzo ya majadiliano ya kidini, ili kudumisha amani duniani na kama sehemu ya utekelezaji wa maamuzi ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican. Baba Mtakatifu amesema, hii ni safari fupi lakini ambayo imesheheni mambo msingi katika maisha na utume wa Kanisa. Amewataka heri na baraka, waandishi wawili waliokuwa wanakumbukia siku zao za kuzaliwa hawa ni Gerard O’Connel, mwandishi wa habari za Vatican kutoka Marekani pamoja na Philip Pullella, mwandishi wa habari za Vatican kutoka Shirika la Habari za Kimataifa Reuters.
Baba Mtakatifu, baadaye amesalimiana na kila mmoja wao. Kuhusu Kongamano la Familia huko Verona, Baba Mtakatifu amesikika akisema, hakuna cha kuongeza zaidi ya kile ambacho Kardinali Pietro Parolin alisema wakati wa maadhimisho ya Jubilei ya Miaka 150 ya Hospitali ya Bambino Gesù inayoendeshwa na kumilikiwa na Vatican.