Tafuta

Kanisa kama Mama na Mwalimu lina dhamana na wajibu wa kuwalinda watoto wadogo! Kanisa kama Mama na Mwalimu lina dhamana na wajibu wa kuwalinda watoto wadogo! 

Mkutano wa Kanisa Kuhusu Ulinzi wa Watoto: Mama na Mwalimu

Dr. Ghison amezungumza kama “Mama” kielelezo cha “Umama wa Kanisa”. Amegusia kwa uchungu kabisa madonda ya Kanisa kuhusu kashfa ya nyanyaso za kijinsia na kulitaka Kanisa kusimama kidete na kupiga moyo konde, ili liweze kuzishughulikia kashfa hizi kwa toba, unyenyekevu na wongofu wa ndani. Hii ndiyo hatua inayopaswa kuchukuliwa na Kanisa katika ujumla wake!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.

Mama Kanisa katika kukabiliana na kashfa ya nyanyaso za kijinsia anapaswa kutambua na kuheshimu utu na heshima ya waathirika wa nyanyaso za kijinsia; kusikiliza kwa makini shuhuda zinazotolewa na waamini walei; ili hatimaye, kutubu na kumwongokea Mwenyezi Mungu, mwingi wa huruma na mapendo. Kanisa, familia ya Mungu inapaswa kuwa makini katika ulinzi wa watoto wadogo. Huu ndio mkazo uliotolewa na Dr. Linda Ghisoni, Katibu mkuu msaidizi, Idara ya Walei, Baraza la Kipapa la Walei, Familia na Maisha katika hotuba yake elekezi wakati wa Mkutano wa Kanisa Kuhusu Ulinzi wa Watoto Wadogo, Ijumaa, tarehe 22 Februari 2019.

Dr. Ghison amehimiza sana kuhusu “Umoja na umuhimu wa kutenda kwa pamoja” ili kulinda na kudumisha utu na heshima ya watoto; kwa kusikiliza na kujibu nyanyaso za kijinsia, ili kuguswa na madonda ya waathirika; kwa toba na unyenyekevu wa ndani. Amekazia umuhimu wa kuwajibika kwa pamoja, jambo ambalo linawezekana kabisa; kwa kushirikiana kwani Kanisa ni Sakramenti katika Kristo; Ukuhani wa waamini pamoja na utekelezaji wake! Hii ni hotuba iliyomfanya Baba Mtakatifu Francisko, kusimama na kuchangia hoja, kwa kumshukuru Dr. Ghison aliyezungumza kama “Mama” kielelezo cha “Umama wa Kanisa”. Amegusia kwa uchungu kabisa madonda ya Kanisa kuhusu kashfa ya nyanyaso za kijinsia na kulitaka Kanisa kusimama kidete na kupiga moyo konde, ili liweze kuzishughulikia kashfa hizi kwa toba, unyenyekevu na wongofu wa ndani.

Baba Mtakatifu anakaza kusema, hii ndiyo hatua inayopaswa kuchukuliwa na Kanisa katika ujumla wake. Kanisa linajipambanua kama “Mama na Mwalimu”, na kwamba ni “Mchumba mwaminifu wa Kristo Yesu”. Kwa njia hii, dhana ya watu wa Mungu imejadiliwa kikamilifu katika mada iliyotolewa na Dr. Linda Ghisoni! Waamini walei wanashiriki: Ukuhani, Unabii na Ufalme wa Kristo kwa njia ya Sakramenti ya Ubatizo. Baba Mtakatifu anaendelea kufafanua kwamba, Dr. Linda amezungumza kama “Mama mzazi” na amewakilisha vyema dhana ya “Kanisa kama Mama”. Mwishoni, Baba Mtakatifu amemshukuru kwa dhati kabisa Dr. Linda Ghisoni kwa ushuhuda wake kama “Mama na Dada”.

Papa: Kanisa ni Mama

 

 

 

 

23 February 2019, 12:24