Papa Francisko atafungua Wiki ya kuombea Umoja wa Wakristo
Sr. Angela Rwezaula - Vatican
Kwa mara ya kwanza Baba Mtakatifu ataongoza maadhimisho ya masifu ya jioni wakati wa kuanza Wiki ya maombi ya kuombea umoja wa wakristo ambapo kwa kawaida ufungwa tarehe 25 Januari sambamba na Sikukuu ya Uongofu wa Mtakatifu Paulo Mtume wa watu. Siku hiyo Baba Mtakatifu kwa dhati atakuwa huko Panama katika Siku ya XXXIV ya Vijana Duniani, inayoanza tarehe 22 -27 Januari 2019. Ni Wiki ya kushiriki katika juhudi za pamoja kwa ajili ya kuombea Umoja wa Kanisa, hasa kama wajibu kwa Kanisa zima ikiwa ni kwa wabatizwa na wachungaji wake.
Mtazingatia haki tu, ili mpate kuishi na kuimiliki nchi mnayopewa
Ijumaa tarehe 18 Januari 2019 saa 11.30 za jioni, Baba Mtakatifu ataadhimisha masifu ya jioni katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Paulo nje ya Kuta. Mwaka huu Maadhimisho haya yanaongozwa na kauli mbiu “Yaliyo ya haki kabisa ndiyo utakayoyafuata”. Kumb. 16:18-20.maadhimisho hayo yanaongozwa na mada ya Neno la Mungu kutoka katika Kumbukumbu la Torati 16, 18-20, lisemalo “Mtateua waamuzi na maofisa kutoka makabila yenu katika miji yenu ambayo mwenyezi Mungu, Mungu wenu atawapa, nao watatoa hukumu za haki kwa watu.
Msipotoshe haki, msiwe na upendeleo, wala msikubali kupokea rushwa kwa kuwa rushwa hupofusha macho ya watu wenye hekima na kupotosha kesi ya mtu mwadilifu. Mtazingatia haki tu, ili mpate kuishi na kuimiliki nchi mnayopewa na Mwenyezi Mungu, Mungu wenu". Ratiba elekezi ya kila mwaka ni kwamba watu wa Nyumba Kuu ya Kipapa husafiri kwa Bus likiwa limesimama eneo la Kuingilia Ukumbi wa Paulo mjini Vatican saa10.30 jioni masaa ya Ulaya.