Tafuta

Papa Francisko asikitishwa sana na maafa yaliyotokea huko Indonesia kutokana na Tsunami Papa Francisko asikitishwa sana na maafa yaliyotokea huko Indonesia kutokana na Tsunami 

Papa Francisko asikitishwa na maafa ya Tsunami huko Indonesia

Baba Mtakatifu Francisko amewakumbuka wale wote waliofariki dunia, waliopata majeraha na wale ambao kwa sasa hawana tena makazi baada ya nyumba zao kubomolewa na Tsunami. Anawaombea huruma na faraja kutoka kwa Mwenyezi Mungu na ameitaka Jumuiya ya Kimataifa kushirikiana na kushikamana na familia ya Mungu nchini Indonesia katika kipindi hiki kigumu!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.

Kwa mara nyingine tena, Jumamosi, tarehe 22 Desemba 2018 kumetokea Tsunami huko Indonesia na kusababisha zaidi ya watu 200 kupoteza maisha na wengine 800 kupata majeraha makubwa na kwamba, idadi ya vifo na waathirika inaweza kuongezeka maradufu. Sehemu zilizoathirika zaidi ni Jakarta na Kisiwa na Sumatra na kwamba, Shirikisho la Misaada ya Kanisa Katoliki nchini Indonesia kwa kushirikiana na Serikali, wanaendelea kutoa huduma kwa waathirika wa tetemeko hili!

Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana, Jumapili, tarehe 23 Desemba 2018 kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, mjini Vatican, amewakumbuka wale wote waliofariki dunia, waliopata majeraha na wale ambao kwa sasa hawana tena makazi baada ya nyumba zao kubomolewa na Tsunami. Anawaombea huruma na faraja kutoka kwa Mwenyezi Mungu na ameitaka Jumuiya ya Kimataifa kushirikiana na kushikamana na familia ya Mungu nchini Indonesia katika kipindi hiki kigumu!

Baba Mtakatifu anakaza kusema, Noeli ya Mwaka huu 2018, iwe ni fursa ya kumwilisha imani katika matendo; kwa familia, ndugu na jamaa kukutana na kusherehekea Noeli kwa pamoja. Baba Mtakatifu amewakumbuka hata wale ambao wako mbali na nyumba pamoja na familia zao, watambue kwamba, wanakumbukwa na Mwenyezi Mungu na kamwe hawezi kuwaacha. Watu wote waweze kuonja ukarimu wa kidugu ndani ya Kanisa, kwani malango ya Jumuiya ya Kikristo daima yako wazi na Kristo Yesu anazaliwa kwa ajili ya wote na anawakirimia watu wote upendo unaobubujika kutoka kwa Mwenyezi Mungu!

Papa: Tsunami Indonesia

 

23 December 2018, 14:47