Papa Francisko anamshukuru Prof. Giovanni Maria Vian kwa kazi kubwa aliyolifanyia Kanisa. Papa Francisko anamshukuru Prof. Giovanni Maria Vian kwa kazi kubwa aliyolifanyia Kanisa. 

Papa Francisko anamshukuru Prof. Giovanni Maria Vian!

Baba Mtakatifu anamshukuru na kumpongeza Professa Vian kwa uwepo, ushirikiano na utayari wake hata katika utekelezaji wa mchakato wa mageuzi Vatican. Ameonesha uaminifu katika kutangaza mafundisho ya Khalifa wa Mtakatifu Petro, daima akiwa anajibidisha kuwalisha watu habari zenye ubora sanjari na kuwapatia watu wasiokuwa na sauti jukwaa la kutolea maoni yao.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.

Baba Mtakatifu Francisko amemwandikia Professa Giovanni Maria Vian, Mkurugenzi mstaafu wa Gazeti la L’Osservatore Romano, barua ya kumpongeza na kumshukuru kwa kazi kubwa aliyoifanya wakati akitekeleza dhamana na wajibu wake kwa ajili ya Vatican na Kanisa katika ujumla wake baada ya kuteuliwa na Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto XVI. Katika kipindi chote hiki, Professa Vian ameonesha: weledi, nidhamu, uadilifu na uwajibikaji wa hali ya juu kabisa mintarafu Mafundisho ya Mababa wa Kanisa pamoja na dhamana yake kama Mkristo!

Baba Mtakatifu anamshukuru na kumpongeza Professa Vian kwa uwepo, ushirikiano na utayari wake hata katika utekelezaji wa mchakato wa mageuzi aliyoanzisha kwenye vyombo vya mawasiliano vinavyomilikiwa na kuendeshwa na Vatican. Kwa hakika hapa ameonesha uaminifu katika kutangaza mafundisho ya Khalifa wa Mtakatifu Petro, daima akiwa anajibidisha kuwalisha watu habari zenye ubora sanjari na kuwapatia watu wasiokuwa na sauti jukwaa la kutolea maoni yao.

Baba Mtakatifu anakaza kusema, Professa Vian alijisadaka bila ya kujibakiza katika kutekeleza dhamana na wajibu wake, kiasi kwamba, utume wake ukawa ni chemchemi ya furaha na amani na kwamba, bado anaendelea kutumainia sala na ushauri wake. Mwishoni, Baba Mtakatifu anamtakia kila la heri na baraka kwake na kwa familia yake.

Papa: Prof. Vian
27 December 2018, 13:50