Tafuta

Baba Mtakatifu Francisko wakati wa katekesi yake amethibitisha kuwa Sikukuu ya Kuzaliwa kwa Bwana inaleta mabadiliko ya maisha yasiyo tarajiwa Baba Mtakatifu Francisko wakati wa katekesi yake amethibitisha kuwa Sikukuu ya Kuzaliwa kwa Bwana inaleta mabadiliko ya maisha yasiyo tarajiwa 

Tujifungulie mshangao ambao Mungu anapendelea!

Katika mwanzo wa katekesi ya Baba Mtakatifu Francisko,ambayo imejikita kutazama sikukuu ya kuzaliwa kwa Bwana amesema na kusema,miti,mapambo na mwanga kila mahali vinatukumbusha kuwa hata mwaka huu ipo sikukuu. Matangazo mengi yanatualika kutoa zawadi mpya ili kufanya mshangao. Iwapo tunataka kuishi sikukuu hii, lazima kufungua moyo kupokea mishangao

Sr. Angela Rwezaula – Vatican

Siku sita zijazo ni Sikukuu ya Kuzaliwa kwa Bwana. Miti, mapambo na mwanga kila mahali vinatukumbusha kuwa hata mwaka huu ipo sikukuu. Vyombo vya matangazo vinatualika kutoa zawadi na daima mpya ili kufanya mshangao. Lakini nauliza, hii ndiyo sikukuu ambayo Mungu anapenda? Je ni Sikukuu gani angependelea Yeye, ni zawadi gani, na ni mshango gani? Ndiyo mwanzo wa tafakari ya Katekesi ya Baba Mtakatifu Francisko tarehe 19 Desemba 2018, kwa mahujaji na waamini wote waliofika katika Ukumbi wa Paulo VI mjini Vatican kusikiliza katekesi yake ambapo tafakari hiyo imejikita kutazama Sikukuu ya Kuzaliwa kwa Bwana ambayo inakaribia.

Kwa kutazama Sikukuu ya kwanza ya Noeli ili kugundua haki za Mungu

Baba Mtakatifu akiendelea na tafakari hiyo anasema: “tutazame Sikukuu ya kwanza ya Kuzaliwa kwa Bwana katika historia ili tuweze kukugunda haki za Mungu. Sikukuu ya kwanza ya historia, ilikuwa imejaa mishangao. Kwa kuanza na Maria ambaye alikuwa ni mchumba wa Yosefu na akafika Malaika na kubadili maisha. Kutoka Bikira na kuwa mama!  Baba Mtakatifu akiendelea kutazama mshangao mwingine anasema: ni kutazama Yosefu ambaye ameitwa kuwa Baba wa mtoto wakati hakumzaa. Mtoto wa kiajabu anawadia kipindi ambacho hakuwa anasubiriwa, kwa maana ilikuwa ni kipindi ambacho Maria na Yosefu walikuwa ni wachumba na kwa mujibu wa sheria, wao wawili kama wachumba wasingeweza kuishi pamoja. Mbele ya jambo hili ilikuwa ni kashfa na kwa maana hiyo, katika kipindi hicho, Yosefu alikuwa analazimika kumwacha Maria na kujikosha jina lake, lakini Yeye pamoja na kuwa na haki ya kufanya hivyo, anashangaza! Baba Mtakatifu anafafanua kuwa, ili kutoweza kumdhuru Maria, alifikiri kumwacha kisiri, hata kwa ghaharama ya kupoteza sifa yake binafsi.

Lakini baadaye, ndipo mshango mwingine unatokea. Mungu katika ndoto anabadili mipango yake na kumwomba amchukue Maria mchumba wake. Aidha mara baada ya kuzaliwa kwa Yesu na wakati tayari anafanya mipango ya kifamilia, kwa mara nyingine tena katika ndoto akaambiwa adamke na kwenda katika nchini Misri. Kutokana na hiyo Baba Mtakatifu anasema: kwa ujumla Sikukuu ya Kuzaliwa kwa Bwana inaleta mabadiliko ya maisha yasiyo tarajiwa. Na iwapo tunataka kuishi sikukuu hii lazima kufungua moyo na kuwa tayari kupokea mishangao hasa ya kubadili maisha yasiyotarajiwa.

Ni wakati wa usiku wa Sikukuu ya Noeli unatokea mshangao mkubwa

Akiendelea na ufafanuzi juu ya mshangao anasema: ni wakati wa usiku wa kuzaliwa kwa Bwana ndipo mshangao mkubwa unatokea, yaani Mtukufu ni mtoto mchanga. Neno la Mungu ni mtoto, akiwa na maana kwamba ni mtoto asiyekuwa na uwezo wa kuzungumza. Na neno la Mungu likawa asiyeweza kuzungumza. Na katika walio mpokea Mwokozi hapakuwapo na viongozi wakuu wa wakati ule au wa maeneo hayo au  mabalozi. Hapana bali walikuwa ni watu rahisi, wachungaji ambao walishangazwa na malaika wakati wanafanya kazi usiku na wakakimbia upesi bila kusimama. Baba Mtakatifu anauliza, “Nani angeweza kutarajia hilo? Krismasi ni kusherehekea Mungu asiyeweza kuelezeka, au tuseme vema ni kuadhimisha Mungu asiyeweza kuelezeka na ambaye anabadili mantiki zetu na matarajio yetu.

Kwa kufanya sikukuu ya kuzaliwa kwa Bwana ni kukaribisha duniani mshangao wa Mbinguni

Kufanya sikukuu ya Kuzaliwa kwa Bwana, basi ni kukaribisha duniani mshangao wa mbingu, Baba Mtakatifu Francisko anasisitiza, siyo rahisi kuishi hivi hivi katika ardhi hii, wakati mbingu ilileta mapya yake duniani. Siku ya Kuzaliwa kwa Bwana ni matashi mema ya zama mpya, mahali ambamo uhai haupangwi, bali hujitoa, mahali ambamo si kuishi kibinafsi, kulingana na ladha binafsi, bali kwa ajili ya Mungu na Mungu, kwa sababu, Sikukuu ya Mungu ni Mungu pamoja nasi ambaye anaishi nasi na anatembea nasi.

Krismasi ni ushindi wa unyenyekevu juu ya kiburi, dhidi ya umimi

Kuishi na kufanya sikukuu ya kuzaliwa kwa Bwana ni kuacha utikiswe na mshangao wa mapya. Sikukuu ya Kuzaliwa kwa Yesu siyo kutoa uhakika wa joto kubwa jikoni, bali ni msisimko wa Mungu ambao unatikisa historia. Kuzaliwa kwa Bwana ni ushindi wa unyenyekevu dhidi ya kiburi, ni  urahisi na  wingi wa kimya dhidi ya kelele nyingi; ni ushindi wa sala dhidi ya wakati wangu, ni ushindi wa Mungu dhidi ya umimi. Kufanya Sikukuu ya Kuzaliwa kwa Bwana ni kufanya kama Yesu aliyekuja kwa ajili yetu wahitaji; ni kushuka kwa wale ambao wanahitaji zaidi yetu. Ni kutenda kama Maria ambaye alijikabidhi kwa Mungu na upole hata bila kujua nini alikuwa anatakiwa kufanya.

Kufanya sikukuu ya Kuzaliwa kwa Bwana ni kufanya kama Yosefu ambaye aliamka ili kutimiza kile ambacho Mungu alikuwa anataka hata kama haikuwa kwa mujibu wa mipango yetu. Mtakatifu Yosefu ni mtu wa mshangao, kwani katika Injili yeye hazungumzi kamwe. Hakuna neno la Yosefu katika Injili; ni Bwana anazungumza naye katika ukimya, akiwa katika usingizi. Sikukuu ya kuzaliwa kwa Bwana inapendelea sauti ya kimya ya Mungu dhidi ya kelele nyingi na kutumia hovyo. Baba Mtakatifu Francisko anashauri kuwa: iwapo tutakuwa na utambuzi wa kukaa kimya mbele ya pango, sikukuu hiyo itakuwa kwetu mshangao na siyo kitu ambacho kilishonekana. Kukaa kimya mbele ya pango, ndiyo wito kwa ajili ya Sikukuu ya Kuzaliwa kwa Bwana. Tafuta muda kidogo, nenda mbele ya pango na kaa kimya. Utahisi, utaona mshangao, Baba Mtakatifu amehimiza! 

Kwa bahati mbaya unaweza kukosea sikukuu

Kwa bahati mbaya lakini inawezekana kukosea sikukuu, Baba Mtakatifu amebainisha na kwamba na kupendelea mapya ya Mbingu, mambo ya kawaida ya dunia. Iwapo Sikukuu ya Kuzaliwa kwa Bwana inabaki kuwa sikukuu nzuri tu ya kiutamaduni, mahali ambapo tunajiweka sisi katikati badala yake, hiyo itakuwa ni fursa iliyopotea Baba Mtakatifu amesisitiza. Kwa maana hiyo ameomba kuwa, sikukuu ya kuzaliwa kwa Bwana isiwe ya kidunia! Tusimweke pembeni anayesheherekewa kama enzi zile kwamba: “Alikuja kwake, wala walio wake hawakumpokea”  (Yh1,11). Tangu mwanzo wa Injili ya Majilio ya Bwana, Baba Mtakatifu anasema tumeombwa  kuwa mioyo yetu isiwe migumu na kusumbukia maisha: “Basi, jiangalieni, mioyo yenu isije ikalemewa na ulafi, na ulevi, na masumbufu ya maisha haya; siku ile ikawajia ghafula, kama mtego unasavyo (Lk 21,34).

Kwa kusisitiza zaidi Baba Mtakatifu pia amonesha kuwa kwa siku hizi ni kukimbizana labda zaidi ya kipindi chote cha mwaka. Lakini wanafanya kinyume na yale ambayo Yesu anataka. Wakati huo ni kutoa lawama mambo mengi ambayo yanajaza siku katika dunia ambayo inakwenda haraka. Licha ya hayo Yesu hakulaumu dunia alituombea ili sisi tusisongwe ndani ya dunia hiyo badala yake tukeshe tukiomba kila wakati (Lk 21,36)

Na tazama itakuwa Sikukuu ya kuzaliwa kwa Bwana iwapo tutakuwa kama Yosefu katika kutoa nafasi ya ukimya

Baba Mtakatifu akihitimisha Katekesi yake amesema: tazama basi itakuwa Sikukuu ya Kuzaliwa kwa Bwana iwapo tutakuwa kama Yosefu, kwa kutoa nafasi ya ukimya; iwapo tutakuwa kama Maria kwa kuitikia Mungu,“ tazama mimi hapa; tutakuwa kama Yesu iwapo tutakuwa karibu na wale walio pekee yake; itakuwa ni sikukuu iwapo tutakuwa kama wachungaji kwa kuondoka katika zizi binafsi ili kwenda kukaa na Yesu. Itakuwa ni sikukuu ya kuzaliwa kwa Bwana, iwapo tutapata mwanga katika groto ya maskini huko Bethlehemu.

Onyo: Baba Mtakatifu anathibitisha, “haitakuwa ni Sikukuu ya Kuzaliwa kwa Bwana, iwapo tutatafuta mianga ya mikuu inayofumba macho ya ulimwengu, iwapo tutajazwa na zawadi, vyakula vya mchana na jioni bila kuwasaidia hata mmoja wa maskini, ambaye anafanana na Mungu, kwa sababu, sikukuu ya kuzaliwa kwa Mungu imekuja ikiwa maskini”. “Ninawatakia Sikukuu njema ya Kuzaliwa kwa Bwana, yenye utajiri mkuu wa sikukuu na mshangao wa Yesu! Inawezekana kuwa mshangao usio kuwa na tija, lakini ndiyo ladha ya Mungu. Iwapo tutajikita ndani mwake, itakuwa mchango wa ajabu kwetu sisi. Kila mmoja wetu ameficha ndani ya moyo wake uwezo wa kushangaza. Tujiachie katika mshangao wa Yesu katika Sikukuu ya Kuzaliwa.

19 December 2018, 13:20