Tafuta

Papa Francisko: Vita ni mama wa majanga makubwa ya binadamu! Papa Francisko: Vita ni mama wa majanga makubwa ya binadamu! 

Papa Francisko kushiriki ufunguzi wa mkutano wa 42 wa IFAD, 2019

Ni wakati wa kuwekeza katika mchakato wa sera na mikakati ya maendeleo endelevu na fungamani kwa ajili ya ustawi na mafao ya wengi, kwa kuhakikisha kwamba: biashara haramu ya silaha duniani pamoja na vita vinakoma. Baba Mtakatifu anasikitika kusema kwamba, vita ni mama wa majanga makubwa ya binadamu!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.

Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kushiriki katika mkutano wa arobaini na mbili wa Baraza kuu la Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo, (IFAD) utakaofanyika mjini Roma, tarehe 14 Februari 2019. Taarifa hii imethibitishwa na Dr. Greg Burke, Msemaji mkuu wa Vatican. Baba Mtakatifu Francisko anasema, baa la njaa duniani linapaswa kushughulikiwa kwa vitendo zaidi kwani maskini na akina yakhe pangu pakavu tia mchuzi wanaendelea kuteseka kila kukicha!

Ni wakati wa kuwekeza katika mchakato wa sera na mikakati ya maendeleo endelevu na fungamani kwa ajili ya ustawi na mafao ya wengi, kwa kuhakikisha kwamba, biashara haramu ya silaha duniani pamoja na vita vinakoma, kwani vita ni mama wa majanga makubwa ya binadamu! Takwimu zinazotolewa na Jumuiya ya Kimataifa zinaonesha kwamba, kuna ongezeko kubwa la watu wanaoendelea kupekenywa na baa la njaa duniani, lakini jambo la kusikitisha ni kuona kwamba, umoja, upendo na mshikamano katika mapambano dhidi ya baa la njaa unazidi kumong’onyoka kila kukicha.

Umefika wakati wa kutekeleza kwa vitendo sera na mikakati inayopania kufutilia mbali baa la njaa na umaskini duniani badala ya kuendelea kuendekeza mtindo wa sasa wa kufanya mikutano na makongamano yasiyokuwa na tija katika mchakato wa mapambano ya baa la njaa na umaskini duniani! Ni wakati wa kuwekeza katika mchakato wa sera na mikakati ya maendeleo endelevu na fungamani kwa ajili ya ustawi na mafao ya wengi, kwa kuhakikisha kwamba, biashara haramu ya silaha duniani pamoja na vita vinakoma. Baba Mtakatifu anasikitika kusema kwamba, vita ni mama wa majanga makubwa ya binadamu! Kwa muhtasari huu ndio ujumbe wa Baba Mtakatifu Francisko aliomwandikia Professa Josè Graziano da Silva, Mkurugenzi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa, FAO, kwa ajili ya maadhimisho ya Siku ya Chakula Duniani, tarehe 16 Oktoba 2018.

Wakati huo huo, Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD), umetoa wito kwa nchi za Kiafrika wa kuwekeza zaidi katika sekta ya kilimo kwa ajili ya kupambana na wimbi kumbwa na wahamiaji sanjari na kuwa na uhakika wa usalama wa chakula duniani katika ujumla wake. Taarifa iliyotolewa na mfuko huo imeutaka Umoja wa Afrika na Umoja wa Ulaya kuwekeza zaidi katika sekta ya kilimo barani Afrika na kwamba hiyo itasaidia kupunguza wimbi la uhamiaji kuelekea Ulaya.

Mkurugenzi wa Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo, Kanayo F. Nwanze amesema kuwa, wakazi wa maeneo ya vijijini wanaamua kuondoka maeneo hayo kuelekea mijini au barani Ulaya kutokana kwamba hawawezi kumudu gharama za maisha yao na familia zao. Amebainisha kwamba, kwa mwaka mmoja Afrika huwa inatenga bajeti ya kiasi cha dola bilioni 35 kwa ajili ya kuagiza bidhaa za chakula na kuwa sasa umefika wakati ajira na uwekezaji katika sekta ya kilimo vipewe nafasi ya pekee na viongozi wa Serikali Barani Afrika.

Papa: IFAD 2019

 

27 November 2018, 14:32