Wayahudi huko  Pittsburgh Marekani katika maombi kufuatia na shambulio la kinyama lilitokea 27 Oktoba  Wayahudi huko Pittsburgh Marekani katika maombi kufuatia na shambulio la kinyama lilitokea 27 Oktoba  

Katika shambulio la Pittsburgh, Papa anasema ni tukio lisilo la kibinadamu!

Papa Francisko ameonesha ukaribu wake na sala kwa ajili ya mji wa Pittsburgh nchini Marekani, kwa namna ya pekee jumuiya ya wayahudi walioshambuliwa tarehe 27 Oktoba katika Sinagogi na kusababisha vifo vya watu kadhaa

Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican

Mara baada ya tafakari na sala ya Malaika wa Bwana, tarehe 28 Oktoba 2018, Baba Mtakatifu Francisko  ameelezea na kuonesha ukaribu wake wa sala kwa mji wa Pittsburgh nchini Marekani, kwa namna ya pekee Jumuiya ya Wayahudi waliopatwa na mkasa wa shambulio la kutisha katika Sinagogi.  Papa amesema: “Mwenyezi Mungu awapokee marehemu wote katika amani yake na kuwapa faraja familia zao, na nguvu  kwa wote waliojeruhiwa.

Hata hivyo kuhusiana na tukio hilo Baba Mtakatifu ameongeza kusema, "wote kwa hakika tumejeruhiwa kwa tendo lisilo la kibinadamu. na hivyo  Bwana asaidie kuzima moto wa chuki ambao unazidi kuongezeka katika jamii zetu na ili  kukuza maana ya ubinadamu, heshima ya maisha, thamani ya kimaadili na kiraia na uchaji wa Mungu ambaye ni upendo na Baba wa wote”.

Kutangazwa wenyeheri Jose Tullio Maruzzo na  Luis Obdulio Arroyo Navarro

Kadhalika akiendelea amesema: Jumamosi 27 Oktoba, huko Marales nchini Guatemala, alitangazwa Mwenyeheri Jose Tullio Maruzzo, mtawa wa ndugu wadogo wafransiskani na Luis Obdulio Arroyo Navarro, waliouwawa kwa chuki, wakitetea imani yao katika karne iliyopita, wakati wa mateso dhidi ya Kanisa, katika jitihada za kuhamasisha haki na amani. Baba Mtakatifu anaongeza kusema: "Tumshukuru Bwana na kuwakabidhi hao maombi kwa ajili ya Kanisa la Guatemala, ndugu kaka na dada, ambao kwa bahati mbaya hata leo hii katika sehemu mbalimbali za dunia wanateseka kwa sababu ya kushuhudia Injili. Na kwa wenyeheri wapya tuwapigie makofi…

Bwana wa miujiza (Señor de los Milagros)

Kadhalika amekumbuka Papa. “ leo hii ni sikukuu ya Bwana wa miujiza (Señor de los Milagros), siku ambayo inajulikana huko Lima na nchi yote ya Peru: kwa wote amewatakia matashi mema,  watu wote wa Peru na jumuiya ya watu wa Peru wanaoishi mjini Roma. Ameongeza kusema, “ Jumapili iliyopita mlikuwa hapa na picha ya Bwana wa Miujiza,  lakini mimi sikujua". Ninawatakia matashi mema katika Sikukuu hii!

Kadhalika amewasalimia hata jumuiya ya Venezuelea wanaoishi Italia ambao wameunganika pamoja wakiwa na picha ya Mama wa  Chiquinquirá, Chinita.

        

28 October 2018, 16:01