Tafuta

Sala ya Malaika wa Bwana Sala ya Malaika wa Bwana 

Papa:Kanisa halihukumu wanandoa bali ni lenye huruma na upendo!

Wakati wa sala ya Malaika wa Bwana, Papa amekumbusha kuwa upendo wa kujitoa moja kwa moja unasindikizwa na Kristo, anayewafanya wanandoa waungane, wakati utafutaji binafsi wa kujitosheleza, unagawanya. Kanisa halitoi hukumu, bali linaalikwa kuwapeleka kwa Mungu waliojeruhiwa mioyo yao au mahangaiko, na anayeishi uzoefu wa uhusiano

Sr. Angela Rwezaula - Vatican

“Injili ya Domenika hii (Mc 10,2-16) inatoa fursa ya Neno la Yesu juu ya ndoa. Simulizi linafunguliwa na wafalisayo ambao wanauliza Yesu kama ni halali mwanaume kumpa talaka mke wake, kama ilivyokuwa inaonesha kanuni ya  sheria ya Musa (Mk 10,2-4). Yesu awali ya yote kwa hekima yake na mamlaka itokayo kwa Baba, anapunguza ukuu wa maelezo ya sheria ya Musa kwa kusema: “Kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu aliwaandikia amri hii”. Hii ilikuwa inawasaidia kwa muda mfupi kutokana na ubinafsi wetu, lakini haikuwa inaendana na lengo asili la Muumba.

Huo ni mwanzo wa tafakari ya Baba Matakatifu wakati wa Sala ya malaika wa Bwana, Jumapili 7 Oktoba 2018, katika kiwanja cha Mtakatifu Petro mjini Vatican, kwa waamini na mahujaji waliofika kusali naye. Baba Mtakatifu akiendelea na tafakari hiyo anasema:”Hapa Yesu ananukuu katika Kitabu cha Mwanzo na kusema: “Tangu mwanzo wa kuumbwa ulimwengu Mungu aliwaumba mume na mke; Kwa sababu hiyo mtu atamwacha baba na mamaye; ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja, (Mk 10:6-7). Na anahitimisha kwa kusema: “Basi alichokiunganisha Mungu mwanadamu asikitengenishe”.

“Katika mpango wa asili wa muumbaji hakuna mume anayeoa mke na wakati huo huo kama mambo yanakwenda vibaya anampatia talaka. Hapana Baba Mtakatifu anabainisha, badala yake mme na mke wanaitwa kutambuana,kukamilishana na kusaidiana kwa pamoja katika ndoa”.

Uaminifu katika ndoa na kuvumilia wakati wa mateso na uchungu

Mafundisho haya ya Yesu yako wazi na yanalinda hadhi ya ndoa, kama muungano wa upendo ambao unahitaji uaminifu. Kile kiinachowawezesha wanandoa kubaki wameungana katika ndoa yao ni upendo wa kujitoa binafsi moja kwa moja kwa mwingine kwa neema ya Kristo. Iwapo katika ndoa inataliwa na upendeleo binafsi, na wa kutaka kujitosheleza, basi kwa maana hiyo muungano wao hauwezi kudumu”.

Na ndiyo sura ya Injili inayokumbusha ukubwa wa hali halisi ambayo mme na mke wanaalikwa kuishi uzoefu wa uhusiano na upendo ambao inawezekana kutokea hata uchungu  na mateso kutokana na ishara za kipeo. Yesu hakubali chochote kile ambacho kinaweza kuleta hatari katika mahusiano. Anafanya hivyo wakati anathibitisha ishara ya Mungu, mahali panatoka nguvu na uzuri wa mahusiano ya kibinadamu. Baba Mtakatifu amesema.

Kanisa kusindiza familia

Kanisa kwa upande mwengine halichoki kuthibitisha uzuri wa familia kama ilivyokabidhiwa na Maandiko Matakatifu na utamaduni; wakati huo huo inajitahidi kusikika kwa dhati katika ukaribu wa umama kwa wale wote wanaoishi uzoefu wa uhusiano uliogawanyika au unakwenda mbele kwa njia ya mateso na matatizo.

Kanisa halihukumu bali ni  huruma na upendo

“Namna ya kutenda kwa Yesu mwenyewe kwa watu wake wasio waaminifu, yaani sisi, Baba Mtakatifu anasema, unatufundisha kuwa upendo uliojeruhiwa unaweza kuponywa na Mungu kwa njia ya huruma na msamaha. Kwa maana hiyo Kanisa, katika hali hiyo haiulizi na wala kuhukumu. Kinyume chake mbele ya machungu mengi ya ndoa zilizoshindwa, Kanisa linasikia kuitwa  na kuishi katika uwepo wake kwa upendo, na huruma, ili kuwapeleka kwa Mungu majeruhi na wanaohangaika. Baba Mtakatifu amemalizia akiomba Bikira Maria ili asaidie wanandoa kuishi na kupyaisha daima muungano wao kuanzia na zawadi ya asili ya Mungu.

08 October 2018, 09:09