Tafuta

Katika sikukuu ya Mtakatifu Yohane Paulo II, Papa Francisko amekwenda katika Kaburi lake na kusali kitambo Katika sikukuu ya Mtakatifu Yohane Paulo II, Papa Francisko amekwenda katika Kaburi lake na kusali kitambo 

Papa amesali katika Kaburi la Mtakatifu Yohane Paulo II

Papa Yohane Paulo II alizaliwa kunako tarehe 18 Mei 1920 na mauti yakamfika kunako tarehe 2 Aprili 2005. Alitangazwa mwenyeheri tarehe 1 Mei 2011. Papa Fransisko akamtangaza Mtakatifu tarehe 27 Aprili 2014. Tarehe 22 Oktoba Papa amekwenda katika kaburi lake kusali kitambo

Sr. Angela Rwezaula - Vatican

Kanisa Mama likiwa linamkubuka Mtakatifu Yohane Paulo II, kila ifikapo tarehe 22 ya Oktoba, Baba Mtakatifu Franciko Jumatatu 22 Oktoba, amekwenda katika Kaburi lake ndani ya Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro na kusali kwa kitambo.

Historia ya Mtakatifu Yohane Paulo II

Papa Yohane Paulo II alizaliwa kunako  tarehe18 Mei 1920 na mauti yakamfika kunako tarehe 2 Aprili 2005. Jina lake la kuzaliwa lilikuwa Karol Józef Wojtyła. Na alikuwa papa wa 264 kuanzia 16 Oktoba 1978 hadi kifo chake akidumu katika huduma hiyo kwa muda mrefu kuliko mapapa wengine wote, isipokuwa Mtume Petro na Papa Pius IX. Yeye alimfuata Papa Yohane Paulo I akiwa Papa wa kwanza asiye kuwa mwitalia tangu miaka 455 iliyopita, wakati wa Mholanzi Papa Adrian VI (1522 - 1523), tena papa wa kwanza kutoka Poland (na makabila yoyote ya Waslavi) katika historia yote ya Kanisa. Baada ya yeye alifuatia  Papa mstaafu Benedikto XVI. Na kwa sasa tunaye Papa Francisko.

Mtakatifu Yohane Paulo II watu wengi, wanamhesabu kati ya watu walioathiriwa zaidi karne ya 20, hasa kwa sababu tangu mwanzo wa upapa wake alipambana na Ukomunisti uliotesa nchi yake asili na nyinginezo, akachangia kwa kiasi kikubwa hadi kufikia  ukomo wake. Vilevile alilaumu ubepari wa nchi za magharib na kudai haki katika jamii zote, akitetea hasa uhai wa binadamu na uhuru wa dini. Kwa upande wa dini, aliboresha uhusiano kati ya Kanisa Katoliki na madhehebu mengine ya Ukristo pamoja na ule na dini mbalimbali, kuanzia Uyahudi, Ubudha, Uislamu na madhehebu mengine. Kwani pia utakumbukwa mkutano wa kwanza wa kuhisitoa wa madhehubu ya dini uliofanyika katika mji wa Asisi.

Ziara zake duniani na Italia

Mtakatifu Yohane Paulo II alifanya Ziara zake 104 kati nchi 129 ulimwenguni kote, mbali na 146 nchini Italia na 317 katika parokia za Roma,  na katika mikutano hiyo ilikusanya mara nyingi umati mkubwa (hadi zaidi ya milioni 4 mfano huko huko Manila, Ufilipino), na kumfanya asafiri kuliko jumla ya mapapa wote waliomtangulia, akiwa mmojawapo kati ya viongozi wa dunia waliosafiri zaidi. Papa Wojtyła alitangaza wenye heri 1,340 na watakatifu 483, ili kuwapa Wakristo wa leo vielelezo mbalimbali kwa maisha yao ili walenge utakatifu walioitiwa na Mungu.

Idadi hiyo ni kubwa kuliko ile ya waliotangazwa na jumla ya Mapapa wote waliomtangulia walau katika karne tano za mwisho. Alikuwa anaongea lugha mbalimbali, zikiwemo za Kipoland, Kiitalia, Kifaransa, Kijerumani, Kiingereza, Kihispania, Kireno, Kiukraina, Kirusi, Kikroati, Kiesperanto, Kilatini na Kigiriki cha kale, na alipendelea kuzungumza lugha mahalia kila alipokuwa akifanya ziara yake. Mtakatifu Yohane Paulo II ametangazwa na mwandamizi wake Papa Benedikto XVI kuwa mwenye heri tarehe 1 Mei 2011, na baadaye Papa Fransisko akamtangaza mtakatifu tarehe 27 Aprili 2014. Tangu siku hiyo Sikukuu yake ikaanza kuadhimishwa kila mwaka tarehe 22 Oktoba, kulingana na siku yake ya  kwanza rasmi huduma yake ya Kipapa kama khalifa wa Mtume Petro.

22 Oktoba 1978 alianza rasmi kama kharifa wa mtume Petro

Nembo yake yenye msalaba na chini yake herufi M kumaanisha Bikira Maria, mama wa Yesu aliyemheshimu sana. Mnamo Agosti 1978, Wojtyła alishiriki uchaguzi wa Papa Yohane Paulo I, aliyefariki baada ya siku 33 tu. Uchaguzi wa pili wa mwaka huo 1978 ulianza tarehe 14 Oktoba na Wojtyła akashinda walipopiga kura mara ya nane. Hapo alijichaguliwa jina la Yohane Paulo II, kwa heshima ya watangulizi wake wa mwisho. Akiwa na miaka 58 tu, alikuwa kijana kuliko Mapapa wote waliochaguliwa baada ya Papa Pius IX mwaka 1846, aliyekuwa na miaka 5. Misa kuu takatifu ya  kuanza  rasmi shughuli ya kuwa kharifa wa mtume Petro ilifanyika tarehe 22 Oktoba 1978.

Mafundisho yake na hati  zake kwa Kanisa

Kama Papa, moja kati ya kazi zake muhimu ilikuwa kufundisha imani na maadili. Hakuna Papa aliyewahi kuwahubiria watu wengi zaidi. Katika kupokea watu siku 1160 za kila Jumatano ya kateksi walifikia watu 17,600,000. Na kati ya katekesi zake alizowapatia waamini na mahijaji wengi , maarufu zaidi ni zile juu ya “Taalimungu ya Mwili.

Mbali na na hati  5, aliandika pia hati 85.  Katika waraka wa Novo Millennio Ineunte alisisitiza umuhimu wa kuanza upya na Kristo katika  mwanzo wa milenia ya tatu: “Hatutaokolewa na tamko, bali na Nafsi hai.” Katika Veritatis Splendor alisisitiza umuhimu wa kujua ukweli ili kufikia uhuru, badala ya kukubali dhana ya kuwa binadamu anaweza kuwa na rai tu. Katika Fides et Ratio alionyesha haja ya imani na akili kushirikiana ili kujua ukweli. Kadhalika Hati nyingine zinahusu Injili ya Uhai (Evangelium Vitae) na Ekumeni (Ut Unum Sint). Mtakatiu Yohane Paulo II alitoa mafundisho mengi kuhusu jamii pia, akitetea heshima ya watu wote, kuanzia wanawake, na umuhimu wa familia: Jinsi familia inavyokwenda,ndivyo taifa linavyokwenda na ndivyo ulimwengu tunamoishi unavyokwenda.

22 October 2018, 15:43