Waamini na mahujaji wakisikiliza tafakari ya Papa Francisko wakati wa sala ya Malaika wa Bwana tarehe 15  Agosti 2018 Waamini na mahujaji wakisikiliza tafakari ya Papa Francisko wakati wa sala ya Malaika wa Bwana tarehe 15 Agosti 2018 

Muungano wa Yesu na Maria ulianza tangu alipopashwa habari!

Kupalizwa kwake mbinguni roho na mwili ni tunu ya kimungu iliyokuwa imeahidiwa kwa Mama yake Mungu kwa sababu ya namna ya kipekee ya muungano na Yesu. Huo ni muungano wa mwili na roho ulioanza tangu alipopashwa habari Mama Maria na kuzidi kukua katika maisha yake yote.

Sr Angela Rwezaula –Vatican

Katika sikukuu ya leo ya Kupalizwa Bikira Maria Mbinguni, watu waamini wa Mungu wanajieleza kwa furaha kubwa, heshima yake Bikira Maria. Wanafanya hivyo katika Liturujia ya pamoja, hata katika mitindo mbalimbali ya huruma; kwa maana hiyo inatimizwa unabii wa wa Bikira Maria mwenyewe kuwa: Kwa kuwa amemwangalia kwa huruma mtumishi wake mnyenyekevu . Hivyo tangu sasa watu wote wataniita mwenye heri ( Lk 1:48).

Kupalizwa kwake mbinguni  roho na mwili ni tunu ya kimungu iliyokuwa imeahidiwa  kwa Mama yake Mungu kwa sababu ya jinsi yake ya kipekee ya muungano na Yesu. Huo ni muungano wa mwili na roho ulioanza tangu alipopashwa habari na kuzidi kukua katika maisha yake yote ya Maria …. Maria daima alikuwa anatembea na Mwanae, alikuwa anatembea nyuma ya Yesu na kwa njia hiyo sisi tunasema alikuwa mfuasi wake wa kwanza…

Huo ni utangulizi wa tafakari ya Baba Mtakatifu Francisko Jumatano tarehe 15 Agosti 2018   wakati wa sala ya Malaika wa Bwana kwa mahujaji na waamini wote kwenye viwanja vya Mtakatifu Petro mjini Vatican  wakati Mama Kanisa anaadhimisha Kikukuu kubwa ya Kupalizwa kwa Bikira Maria mbinguni.

Akiendelea na tafakari hiyo, Baba Mtakatifu amesema, uvumilivu wa Mama Maria uliejionesha kama ule wa mwanamke wa kawaida kwa wakati ue, kwani alikuwa akisali, akitunza familia na nyumba na  alikuwa akiudhuria katika hekalu. Lakini kila tendo lake la kila siku alilokuwa akijikita, lilikuwa katika muungano wa dhati na Yesu. Kwa kutazama juu ya mlima wa Kalvario, muungano huo ulijionesha wa hali ya juu, kwa upendo na huruma pia mateso makuu ya moyo.  Kwa maana hiyo Mungu alimzawadia ushiriki wa dhati hata katika ufufuko wa Yesu. Mwili wa Mama Mtakatifu ulitunzwa bila kuharibiwa kama ule wa Mtoto wake. Kanisa leo hii linaalika kutafakati fumbo hili. Hiyo ni kwasababu tendo hilo linaonesha kuwa, Mungu anataka kumkomboa mwanadamu kamili, yaani kuokoa roho na mwili, ndiyo binadamu kamili! Yesu alifufuka na mwili wake aliokuwa amepewa na Maria na alipaa kwa Baba na ubinadamu wake uliobadilishwa. Alikuwa na mwili kama mwili wetu, japokuwa uliobadilishwa.

Kupalizwa kwa Bikira Maria, kiumbe aliye binadamu ni uthibitisho kwetu sisi ya kwamba, ndiyo utakuwa mwisho wetu wenye utukufu. Mwili wetu uliobadilishwa utakuwa pale pale na huo ni ufufuko wa mwili,  ni kiungo cha dhati kinacho jionesha ukristo na kipeo cha imani yetu, Papa Francisko anathibitisha!

Akitoa mfano mfano amesema: Wanafalsafa wa kigiriki, walikuwa tayari wametambua hilo ya kuwa matarajio ya roho ya binadamu ni furaha baada ya kifo. Wao walikuwa wanatambua tu kile cha roho, lakini pamoja na hayo walikuwa wakidharau mwili na kuufikiria kuwa umefungwa ndani ya roho; walikuwa hawatambui kwamba Mungu, aliweka uwezo wa mwili wa binadamu kuungana na roho katika heri za mbinguni. Ukweli wa kushangazana kufurahisha wa Kupalizwa kwa Bikira Maria ni maonesho na kuthibitisha ya umoja wa binadamu uliopo na kukumbusha kuwa, wote tunaalikwa kuhudumia na kumtukuza Mungu kwa jinsi tulivyo, yaani  roho na mwili!

Utukufu wa Mungu ni binadamu anayeishi.

Kuhudumia Mungu kwa mwili tu  Baba Mtakatifu anaongeza, inaweza kuwa tendo la utumwa; kuhudumia kwa roho tu pia  inawezekana kuwa kinyume na asili ya binadamu.  Baba mmoja wa Kanisa kwenye miaka ya 220, Mtakatifu Ireneo, alithibitisha kuwa “utukufu wa Mungu ni binadamu anaye ishi na maisha ya binadamu yanategemea maono ya Muungu  ( Rejea barua ya kuthibiti waasi wa  Mungu, IV, 20,7)

Na iwapo tutaishi namna hii, katika kutoa huduma ya furaha kwa Mungu, inayojieleza hata kwa ukarimu wa huduma kwa ndugu, mwisho wetu katika siku ya ufufuko itakuwa inafanana na ile ya Mama wa Mbinguni. Kwa maana hiyo itatimizwakwa dhati  ule Wosia wa kitume wa Mtakatifu Paulo, asemaye, kwa hiyo itumieni  miili yenu kwa ajili ya kumtukuza Mungu ( 1Kor 6,20) na tutamtukuza daima mbinguni.

Papa Francisko amehimitimisha na kusema kwamba, tumwombe Mama Maria, ili kwa njia ya maombezi yake ya umama aweze kutusaidia tuishi safari yetu ya kila siku kwa matumaini na kuwajibika na ili hatimaye tuweza siku moja kuwa na watakatifu wote na wapendwa wetu wote huko mbinguni.

15 August 2018, 15:11