Papa Francisko amesali kwa ajili ya watu waliopoteza ajira zao katika kipindi cha janga!
Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican
Papa Francisko Jumatatu ya Wiki ya tano ya Pasaka, tarehe 11 Mei 2020 ameadhimisha Ibada ya Misa katika kikanisa cha Mtakatifu Marta Vatican, ambapo katika utangulizi amekumbuka maadhimisho ya kumbukumbu ya miaka 75 tangu kupatikana kwa Mwili wa Mtakatifu Timotheo katika Kanisa Kuu la Termoli, Italia wakati wa ukarabati wa kanisa hilo kunako mwaka 1945. Mawazo yake pia amesali kwa ajili ya watu wengi ambao katika nyakati hizi za janga la corona wanateseka sana kutokana na kupoteza ajira zao. “Tuungane pamoja na waamini wa Termoli katika siku kuu ya kupatikana kwa mwili wa Mtakatifu Timotheo leo. Katika siku hii watu wengi wamepoteza kazi hawakupata ajira tena, wengine walikuwa wanafanya kazi isiyo ya kuajiriwa… Tusali kwa ajili ya hawa kaka na dada zetu ambao wanateseka na ukosefu huu wa kazi”.
Ahadi ya Roho Mtakatifu inaishi ndani mwetu
Papa katika mahubiri yake ameongozwa na Injili ya siku mahali ambapo Yesu anawambia mitume wake “ ikiwa kila ampendaye atazishika amri zake na Baba atampenda halafu Yeye na Baba watakuja kwa huyu mtu”. Mtu asiyenipenda, yeye hayashiki maneno yangu; nalo neno mnalolisikia silo langu, ila ni lake Baba aliyenipeleka. Hayo ndiyo niliyowaambia wakati nilipokuwa nikikaa kwenu. Lakini huyo Msaidizi, Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaambia” (Yh 14, 21-26) Kwa kurudia kifungu hicho Papa ameongeza kusema ni ahadi ya Roho Mtakatifu ambayo inaishi ndani mwetu, ambayo Baba na Mwanaye wanatuma ili kutusindikiza katika maisha, na Yeye anaitwa Msaidizi, kwa maana anatuimarisha tuwe imara na tusianguke. Bwana alituahidi msaada huo ambao ni Mungu mwenyewe!
Roho Mtakatifu anatufundisha kuingia katika fumbo
Roho Mtakatifu anatufundisha kuingia katika fumbo la imani, anatusaidia kujua mafumbo, mafundisho ya Yesu na kuyakuza katika imani yetu bila kukosea. Haya ni mafundisho ambayo yanakuwa katika ukuu wake, japokuwa daima katika mwelekeo huo huo, anatusadia kulewa zaidi kile anachosema. Mafundisho hayo kamwe hayasimami bali yanakua, anathibitisha Papa Francisko. Roho Mtakatifu anazuia mafundisho haya yasisimame bila kukua ndani mwetu. Yanakuza ndani mwetu ule ufahamu wa kile ambacho Yesu anafundisha. Roho Mtakatifu anatufanya tukumbuke kile ambacho Yesu alisema. Ni kama kumbu kumbu inayotuamsha, na kutufanya tubaki bila kusinzia mbele ya mambo ya Bwana; aidha anatufanya tukumbuke maisha yetu tunapokutana na Bwana au tunapomwacha Bwana.
Roho Mtakatifu anatusaidia kufanya uamuzi sahihi
Roho Mtakatifu anatupeleka katika kumbu kumbu ya wokovu, kumbu kumbu ya mchakato wa safari ya maisha; anatuongoza ili kung’amua nini tunatakiwa kufanya sasa, na ni njia gani ya kweli na isiyo sahihi. Roho Mtakatifu anatusaidia kufanya uamuzi sahihi, uwe mdogo au mkubwa wa kila siku. Anatufundisha kila kitu, anatuongoza kuingia katika mafumbo, anatufanya tukumbuke na kutufanya tuweze kung’amua. Roho huyo Mtakatifu ni Zawadi ya Mungu kama asemavyo kuwa: “ sitaawacha peke yenu, nitawatumia Msaidizi” na Bwana atusaidia kuitunza zawadi hii ambayo tuliipokea wakati wa ubatizo” amehitimisha Papa Francisko. Kama kawaida ya Papa Francisko kwa wakati huu baada ya misa imefuatia Ibada ya kuabudu na kubariki kwa Ekaristi. Kabla ya kuacha Kikanisa cha Mtakatifu Marta, wimbo wa Maria umeimbwa wa Kilatino:Malkia wa Mbingu
Regína caeli laetáre, allelúia.
Quia quem merúisti portáre, allelúia.
Resurréxit, sicut dixit, allelúia.
Ora pro nobis Deum, allelúia.