Tafuta

Baba Mtakatifu Francisko anawaalika waamini kujiandaa kikamilifu kwa imani, matumaini na mapendo kumpokea Yesu atakapobisha katika malango ya maisha yao! Baba Mtakatifu Francisko anawaalika waamini kujiandaa kikamilifu kwa imani, matumaini na mapendo kumpokea Yesu atakapobisha katika malango ya maisha yao!  (ANSA)

Papa Francisko: Jiandaeni vyema kumpokea Yesu katika maisha!

Baba Mtakatifu Francisko anawaalika waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema kujiandaa vyema kukabiliana na Fumbo la Kifo. Ili kuweza kufikia hatua hii, kwanza kabisa mwamini anapaswa kuishi kwa imani, matumaini na mapendo thabiti. Mwamini atambue udhaifu na mapungufu yake ya kibinadamu, ajiaminishe na kujikabidhi chini ya uongozi na Kristo Yesu! KIFO!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.

Baba Mtakatifu Francisko, Ijumaa, tarehe 29 Novemba 2019 ameadhimisha Ibada ya Misa takatifu kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha kilichoko mjini Vatican kwa kukazia umuhimu wa kujiandaa vyema ili kukabiliana na Fumbo la Kifo. Ili kuweza kufikia hatua hii, kwanza kabisa mwamini anapaswa kuishi kwa imani, matumaini na mapendo thabiti. Mwamini atambue udhaifu na mapungufu yake ya kibinadamu, ajiaminishe na kujikabidhi chini ya uongozi na Kristo Yesu. Wakati huu, Kanisa linapojiandaa kufunga Mwaka wa Liturujia na kufungua Mwaka Mpya wa Kanisa kwa kuanza kipindi cha Majilio, waamini wanahimizwa kusali, ili kuweza kujiandaa kikamilifu kwa Ujio wa Kristo Yesu katika maisha yao! Baba Mtakatifu anafafanua kwamba, kifo kinamwezesha mwamini kukutana mubashara na Kristo Yesu katika safari yake ya mwisho hapa duniani, inayohitaji maandalizi makini pamoja na waamini kusindikizana kwa sala na sadaka, ili kwa imani, matumaini na mapendo, waweze kuwa tayari kukutana na Kristo Yesu, Hakimu mwenye huruma na haki, wakati makao ya hapa duniani yatakapokuwa yamebomolewa, ili kupata makao ya maisha na uzima wa milele!

Mama Kanisa anawakumbusha watoto wake kwamba, yote yatapita, lakini Neno lake linadumu milele yote. Udhaifu na mapungufu ya binadamu yanawafanya wachungulie kifo. Ni kutokana na muktadha huu, ndio maana watu wanaposongwa na shida mbali mbali wanashauriwa kuonana na daktari au mshauri ili kupata tiba na nasaha. Baba Mtakatifu anawashauri watu wa Mungu kujiandaa vyema kukabiliana na Fumbo la Kifo katika hija ya maisha yao na wala wasikubali matapeli kuwalaghai kwa kutaka kurefusha maisha yao, lakini mwisho wa yote ni kifo! Wala hakuna mtu awaye yote atakayeishi milele, kufa ni lazima kwa binadamu, lakini waamini wanapaswa kujiandaa kwa imani na matumaini ili kukabiliana na Fumbo la kifo, pale Kristo Yesu atakapokuja kuwachukua. Baba Mtakatifu anasisitiza kwamba, hili si tangazo la kifo, bali ni sehemu ya Injili inayosimikwa katika maisha kwa kugusa udhaifu na mapungufu ya binadamu! Jiandaeni kwani iko siku, Kifo kitabisha hodi malangoni penu! Huu ni mwaliko wa kusali na kuombeana, ili kujenga na kuimarisha imani, matumaini na mapendo. Kwa hakika, hakuna mtu anayefahamu ile saa wala siku atakapkutana na kifo, jambo la msingi ni kujiandaa kikamilifu. Fumbo la kifo linapaswa kufumbatwa katika imani, matumaini na mapendo!

Papa: Kifo

 

 

 

 

 

29 November 2019, 17:10
Soma yote >