Tafuta

Papa Francisko: Kwaresima ni kipindi cha kufunga, kusamahe na kufanya matendo ya huruma: kiroho na kimwili! Papa Francisko: Kwaresima ni kipindi cha kufunga, kusamahe na kufanya matendo ya huruma: kiroho na kimwili!  (Vatican Media)

Kwaresima ni muda wa: kufunga, kusamehe na matendo ya huruma!

Baba Mtakatifu anawataka waamini kujivika huruma ya Mungu, tayari kusamehe hata mambo makubwa zaidi! Mwenyezi Mungu ni mwingi wa huruma na mapendo, kwa wale wote wanaotubu na kumwongokea, yuko tayari kuwasamehe na kuwakirimia tena neema ya kuanza upya safari ya maisha yao hapa duniani! Mkazo: Kufunga, kusamahe na matendo ya huruma kwa maskini zaidi!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.

Baba Mtakatifu Francisko katika mahubiri aliyotoa kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha, kilichoko mjini Vatican, Jumatatu, tarehe 18 Machi 2019 amekazia kuhusu umuhimu wa kuiga huruma ya Mungu katika maisha pamoja na kutoa ushauri wa jinsi ya kuishi kikamilifu Kipindi cha Kwaresima! Baba Mtakatifu anawataka waamini kujivika huruma ya Mungu, tayari kusamehe hata mambo makubwa zaidi! Mwenyezi Mungu ni mwingi wa huruma na mapendo, kwa wale wote wanaotubu na kumwongokea, yuko tayari kuwasamehe na kuwakirimia tena neema ya kuanza upya safari ya maisha yao hapa duniani!

Baba Mtakatifu anasema, kujinyonga ni dhambi ya mauti, lakini hata katika dhambi hii, bado kuna huruma ya Mungu isiyokuwa na mipaka, kumbe, waamini wasijikatie tamaa wala kukatishwa tamaa, bali wawe na ujasiri wa kukimbilia huruma ya Mungu! Ushauri wa bure katika kipindi hiki cha Kwaresima: Mosi, usihukumu kwani hii ni tabia mbaya sana katika maisha ya kiroho. Pili, ni kusamehe na kusahau, ingawa si rahisi sana kutokana na udhaifu wa kibinadamu. Lakini, waamini wakumbuke kwamba, watasamehewa kwa kipimo kile kile walichotumia kuwasamehe jirani zao.

Tatu, waamini waoneshe moyo wa upendo na ukarimu, kwa kuondokana na kishawishi cha kutaka “kupika majungu”, kwa kuwahukumu watu! Waamini wawe na ujasiri wa kuwasaidia wengine na kwa jinsi hii wataweza pia kupata neema na baraka kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Ukarimu ni nguzo msingi dhidi ya majungu! Kwaresima, kiwe ni kipindi cha kumwilisha matendo ya huruma: kiroho na kimwili kwa wahitaji zaidi!

Papa: Mahubiri
18 March 2019, 14:34
Soma yote >