Papa ameonya dhidi ya,ubinafsi, mashindano na majivuno!
Na Sr. Angela Rwezaula - Vatican
Mashindano na majivuno vinaharibu kwa kina jumuiya na kupanda mbegu za migawanyo na migogoro. Ndiyo msisitizo mkuu wa Papa Francisko wakati wa kutoa mahubiri yake katika Misa ya Asubuhi katika Kanisa la Mtakatifu Marta Mjini Vatican, tarehe 5 Novemba 2018. Katika mahubiri yake ameongozwa na Injili ya Siku ya Mtakatifu( Lk 14,12-14) na pia somo la pili la Mtakatifu Paulo kwa (Flp. 2:1- 4), ambapo Papa anahukumu vikali suala la ubinafsi na kujijali kwa kutafuta faida binafsi, badala yeke anasema kuwa kutoa bure kama Yesu alivyokuwa akihubiri haina maana ya kuchagua!
Kutoa bure ni ishara ya ulimwengu wote na si kuchagua
Mafundisho ya Yesu yako wazi, Baba Mtakatifu anasema, siyo kufanya mambo bila kuwa na sababu, si kuchagua marafiki binafsi yaani kwa mujibu wa dhamiri nafsi. Na suala la kufikiria juu ya msingi wa kujithamini tu, kwa dhati ni aina ya ubinafsi, ubaguzi na maslahi binafsi, wakati, ujumbe wa Yesu unakwenda kinyume kabisa kwa maana, kujitoa bure hupanua maisha, huongeza upeo, kwa sababu ni mantiki ya kutazama ulimwengu mzima. Watu wanaochagua ni kwa mantiki ya migawanyo na ambayo haisaidii katika ubinadamu. Hiyo ndiyo ambayo Mtakatifu Paulo ameandika katika Barua ya kwanza kwa Wafilipi. Papa amebainisha na kwamba yapo mambo mawili dhidi ya ubinadamu ambayo ni kushinda na majivuno.
Papa ameongeza kusema kuwa masengenyo pia, yanatokana na mashindano kwa sababu watu wengi uhisi kujiweka wa hali ya juu na kuwashusha wengine chini, kwa njia ya masengenyo. Na kwa namna hiyo ni kumwaribu mtu, ndiyo maana Paulo anasema katika jumuiya kuwa pasiwepo mashindano. Mashindano ni mapambano dhidi ya kumsema mwingine. Ni jambo baya, hata lifanyike kwa namna wazi au likiwa limefunikwa kitambaa cheupe, lakini daima linaharibu mwingine na kujiinua binafsi. Sababu ya kufanya hivyo, Papa amefafanua ni kutokana na kwamba: “siwezi kuwa na karama nzuri ya mtu kama huyo na kuwa mwema hivyo, basi ninaamua kumpunguza mwingine, na ili mimi ninabaki daima kuwa wa hali ya juu. Mashindano ni njia ya kutenda hivyo kwa sababu ya kutafuta faida binafsi”.
Majivuno yanaharibu jumuiya, familia na hata sehemu za kazi
Kadhalika Papa Francisko amekijita kulezea juu ya majivuno ambayo ni sawa sawa na mashindano, kwa maana, ni yule anayejiona kuwa bora zaidi ya wengine. Hiyo inaharibu jumuiya, inaharibu familia pia. Baba Mtakatifu anatoa mfano, kwamba, fikiria mashindano kati ya ndugu kwa ajili ya urithi wa baba yao, sauala ambalo linatokea kila siku … Fikirieni majivuno ya wale wanaojidai kuwa bora ya wengine pia!
Maisha ya kikristo yanazaliwa kutokana na Yesu kujitoa bure
Mkristo lazima atafute mfano wa Mwana wa Mungu kwa kukuza ile hali ya kujitoa bure na kufanya wema kwa ajili ya wangine bila kuhangaikia kama wangine nao wanafanya vile vile. Hiyo ni katika kupanua moyo wa ukarimu na kwa kupinga ushindani au majivuno. Kujenga amani kwa njia ya ishara ndogo ndogo, maana yake ni kuunganisha safari ya mapatano katika dunia, Baba Mtakatifu amethibitisha.
Akimalizia aidha amesema tunaposoma habari za vita, tunafikiria habari za njaa ya watoto wa Yemen, ambalo ni tunda la vita tunasema, huko ni mbali, maskini watoto… lakini je kwa nini hawana chakula? Lakini vile vile vita pia vinafanyika katika nyumba zetu, taasisi zetu kwa njia ya mashindano haya. Ndipo vita vinaanzia! Kwa maana hiyo, amani lazima ianzie pale pale ndani ya familia,katika jumuiya, katika taasisi, nafasi za kazi kwa kutafuta daima kuwa na roho moja na mapatano bila kutafuta faida binafsi.