Tafuta

Papa Francisko katika Misa amaekumbusha kuwa: Yesu alisema, ombeni na mtapewa Papa Francisko katika Misa amaekumbusha kuwa: Yesu alisema, ombeni na mtapewa  (Vatican Media)

Papa Francisko: Yesu anatufundisha tusali bila kuchoka!

Lazima kuwa wajasiri wakati tunapo omba jambo lolote Bwana. Amesema hayo Papa Francisko wakati wa mahubiri yake asubuhi, tarehe 11 Oktoba 2018, katika Kanisa la Mtakatifu Marta Vatican. “Mungu ni rafiki na ambaye anaweza kutupatia kila tunachohitaji”

Sr. Angela Rwezaula – Vatican

Injili ya Siku, imemsadia Baba Mtakatifu kujikita katika  kutafakari  la Neno la Mungu katika Misa ya asubuhi tarehe 11 Oktoba 2018, ambapo amekabiliana na mada ya sala na jinsi gani sisi tunatakiwa kusali. Bwana anawasimulia kwa dhati mitume wake juu ya historia ya mtu aliyefika usiku wa manane akibisha hodi nyumbani kwa rafiki yake na kuomba chochote cha kula. Rafiki yake alijibu, siyo muda mwafaka, kwa maana alikuwa tayari amelala. Lakini baadaye aliamka na kumpatia kile alichokihitaji.

Kusali bila kuchoka

Baba Mtakatifu katika kufafanua juu ya sala, amesisitiza mambo makuu matatu: mtu mwenye kuhitaji, rafiki na mkate kidogo. Ni ziara ya kushitukiza ya rafiki mwenye kuhitaji na maombi yake hakuchoka kamwe, kwa maana alikuwa na imani kwa rafiki yake kwa kile alicho hitaji. Kusali kwa namna hiyo, ndiyo mtindo ambao Bwana anataka kutufundisha kusali, Papa anasisitiza. “Na hiyo ni kusali kwa ujasiri, kwa sababu tunaposali tunahitaji na kwa kawaida ni mahitaji yaliyo muhimu. Rafiki ni Mungu, ni rafiki tajiri mwenye kuwa na mkate, ambao sisi sote tunahitaji. Kama vile Yesu anasema “Katika sala muwe waingiliaji. Msichoke” Lakini je kuchoka kwa ajili ya kitu gani” je ni kitu gani cha kuomba. “Yeye anasema “ ombeni na mtapewa”.

Sala siyo fimbo ya mazingaombwe

Sala siyo fimbo ya mazingaombwe, na si kwamba tunapomaliza kuomba tunapata haraka. Haina maana ya kusema maneno mawili ya “Baba Yetu” alafu unaondoka zako. Sala ni kazi. Kazi ambayo inataka utashi, inataka usichoke na inakutaka kuwa na msimamo, bila kuwa na aibu. Kwa nini? kwa sababu, mimi niko nabisha hodi katika mlango wa rafiki. Mungu ni rafiki na katika rafiki mimi ninaweza kufanya hivyo. Sala ambayo haikatiki lakini pia ya kuingilia kati.  Baba Mtakatifu ametoa mfano wa Mtakatifu Monika, kwamba ni miaka mingapi alisali, hata kwa machozi, kwa ajili ya uongofu wa mwanae ( Agostino).Lakini hatimaye Bwana alimfungulia mlango. Amebainisha Papa.

Kupambana na Bwana ili kupata

Papa Francisko ametoa mfano wa pili akisimulia tukio la uhakika ambalo lilitukia huko Buenos Aires nchini Argentina. Mtu mmoja mfanyakazi alikuwa na mtoto msichana karibu ya kufa, na madaktari hawakuwa na matumaini ya mtoto huyo kuishi. Baba huyo, alitembea kilometa 70 hadi katika Madhabahu ya Bikira Maria wa Lujan. Alifika usiku na Madhabahu hiyo ilikuwa imefungwa, lakini yeye alibaki nje na kusali usiku mzima akimwomba Bikira Maria: “Ninataka mwanangu, mimi ninataka mwanangu. Na wewe unaweza kunipatia”. Kesho yake asubuhi aliporudi katika hospitali, mke wake alimwambia, “ unajua , madaktari wamempleka mtoto kumpima lakini wamesema, hawajuhi ni kitu gani kwa maana mtoto amezinduka na kuamka, akiomba chakula, kwa sasa yeye hajambo . Baba Mtakatifu ameongeza, “Yule baba alitambua ni nini kwa maana alikuwa amesali”.

Vilio vya watoto watukutu lakini wanapatiwa wanachotaka

Hata hivyo Papa, amewaalika waumini kutafakari hata watoto ambao ni watukutu, wanapokuwa wanataka kitu fulani, wanalia, sana, wanapiga mayowe wakisema, ninataka! Ninataka! Na mwisho wake, wazazi wanakubali.  Lakini mmojawapo anaweza kuuliza: je Mungu hawezi kukasirika iwapo nitafanya hivyo? Na Yesu mwenyewe Papa anathibitisha, kwa matazamio ya jambo hilo, alisema: “Iwapo ninyi mlio wakatili, mnatambua kuwapa vilivyo vyema watoto wenu, jinsi gani Baba wenu aliye mbinguni atawapatia Roho Mtakatifu kwa wale wanao mwomba”.

Papa Francisko akihitimisha tafakari, amesisitiza kwamba, ni rafiki ambaye daima anatoa mema. Anatoa zaidi kwa yule anayeomba ili kutatua matatizo pia kutoa hata Roho Mtakatifu. Tafakarini kidogo: je ninasali namna gani? Kama kasuku? Ninasali kwa moyo wote kweli? Ninapambana na Mungu katika sala ili anipatie kile ninacho hitaji hasa kinachostahili? Tujifunze vema sehemu hiyo ya Injili jinsi gani ya kusali.

11 October 2018, 15:36
Soma yote >