Tafuta

2023.01.24 Kundi la Kikao cha Pili cha kazi kwa ajili ya awamu ya kibara,Afrika huko Nairobi-Kenya, kuanzia 23 -25 Januari 2023. 2023.01.24 Kundi la Kikao cha Pili cha kazi kwa ajili ya awamu ya kibara,Afrika huko Nairobi-Kenya, kuanzia 23 -25 Januari 2023. 

SECAM:Kundi la wataalam katika kikao cha II cha kazi ya Sinodi kibara!

Katika Maadhimisho ya Awamu ya Pili ya Sinodi kwa ngazi ya Kimabara,kikao cha pili cha Bara la Afrika kimefunguliwa tarehe 23 na kitahitimishwa tarehe 25 Januari, huko Nairobi Kenya.Kabla ya kikao hicho kilitanguliwa na mkutano kwa njia ya mtandao wa Makatibu wakuu kutoka mabaraza ya Maaskofu wa Kanda mbali mbali za mashirikisho la Mabaraza ya Maaskofu yanayounda SECAM.

Na Angella Rwezaula; - Vatican.

Katibu wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu wa Afrika na Madagascar(SECAM), kwa kushirikiana na Initiative for African Synodality (ASI), yaani Mpango wa Sinodi kwa ajili ya Afrika, wanayo furaha kuwatangaza  wote juu ya mkutano wa kundi la wataalam kutoka bara la Afrika kwa ajili ya kikao  cha kazi ya pili ya Sinodi ya kibara kuhusu Sinodi, inayofanyika kuanzia tarehe 23 Januari hadi 25 Januari 2023 katika Jumba la AFRICAMA, jijini Nairobi, Kenya. Mkutano huo unafuatiwa  na sehemu ya kikao cha kwanza kilichofanyika mjini Accra, nchini Ghana kuanzia tarehe 6 hadi 9 Desemba 2022, ambapo timu ya Bara ilitafakari kuhusu Hati ya Hatua ya Mabara (DTC) iliyoandaliwa na Sekretarieti kuu ya Sinodi ya Vatican. Kutokana na mktadaha huo katika kikao cha kwanza, timu ya bara iliithamini hati hiyo (DTC) katika muktadha wa masuala yaliyojitokeza kutoka katika makanisa kwenye  ripoti za kikanda na kufafanuliwa rasimu ya waraka wa kisinodi wa bara la Afrika. Kikao hicho cha Pili kwa maana hiyo  ni njia ya kusikilizana na ya Roho Mtakatifu, ambayo itashuhudia timu ikijitolea katika: kufafanua upya hati ya sinodi ya bara la Afrika na ufahamu mpya unaotoka katika Makanisa mahalia; na kujadili mpango unaowezekana wa mkutano wa Sinodi ya Bara la Afrika uliopangwa kufanyika Juma la kwanza la mwezi Machi 2023 huko Addis Ababa, nchini Ethiopia.

Wajumbe wa Mikao cha Pili cha Kazi kwa ajili ya Awamu ya Kibara ya Sinodi, Barani Afrika
Wajumbe wa Mikao cha Pili cha Kazi kwa ajili ya Awamu ya Kibara ya Sinodi, Barani Afrika

Hata hivyo kabla ya  mkutano huo, kilifanyika  kikao kwa njia ya mtandao ambacho kiliwaleta pamoja Makatibu wakuu kutoka mabaraza ya Maaskofu wa Kanda mbali mbali za mashirikisho ya Mabaraza ya Maaskofu ambayo yanaunda Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu wa Afrika na Madagascar (SECAM). Viongozi wa Kanisa  walishirikishana  baadhi ya changamoto na matokeo yaliyopatikana katika Afrika kwenye mchakato wa sinodi. Wakati wa hatua ya pili ya mchakato wa sinodi, Kanisa  hata hivyo linawaalika mabara mbalimbali kuendelea kupambanua na kusikiliza sauti ya Roho kwa kutumia Hati ya kitendea Kazi kwa ajili ya Hatua ya Kibara. Akizungumza wakati wa kikao mtandaoni ambacho kilikubaliwa na sekretarieti kuu ya Roma na SECAM, Askofu Luis Marín de San Martín, wa Shirika la Mtakatifu Augustino(OSA), ambaye ni Katibu Msaidizi wa Sekretarieti Kuu ya Sinodi alibainisha kwamba kanda ya Afrika inapaswa kutambua kipengele cha tofauti za kiutamaduni katika mchakato wa sinodi  hasa wanaposikilizana wao kwa wao kwa njia ya Roho Mtakatifu. Na hii kwa kuongeza  alisema na  kama vile Neno la Mungu lilivyo jikita ndani yake katika historia, hivyo hivyo hata mchakato wa Sinodi unahitaji hatimaye kuchukua maamuzi ambayo yanatambua na kurutubishwa na tofauti za kiutamaduni za Afrika na mabara mengine. Na utofauti huo wa kiutamaduni utalitajirisha Kanisa la ulimwengu wote.

Kikao cha Pili cha kazi kwa ajili ya Awamu ya kibara Afrika 23-25 Januari 2023
Kikao cha Pili cha kazi kwa ajili ya Awamu ya kibara Afrika 23-25 Januari 2023

Katika kuwasilisha kwa waandishi wa habari juu ya  tafakari ya kwanza ya awamu ya mwisho ya hatua ya bara kwa  Makatibu wakuu wa Sinodi ya Afrika,  walieleza changamoto  ambazo karibu zinazofanana kwa bara zima. Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Shirikisho  la  Mabaraza ya Maaskofu wa Afrika Mashariki (AMECEA), Padre Anthony Makunde, kuhani wa Tanzania, alisema kuwa: “Mchakato wa usikilizaji unafanyika katika mazingira ya mchanganyiko wa jamii, hivyo eneo hilo halina mazingira ambapo hata kama Wakatoliki ni wengi lakini kuna mchanganyiko wa madhehebu”. Akitaja maeneo mengine yenye changamoto,  Padre Makunde  alisema imani za kijadi bado ziko hai katika nchi mbalimbali, hivyo kuwashawishi wasikilizaji, na idadi kubwa ya nchi zina migogoro ya kisiasa inayoambatana na misimamo mikali ya kidini ambayo imekithiri katika mabaraza mbalimbali. Zaidi ya hayo, Padre Makunde alibainisha kwamba: “Kanisa linapaswa kufanya zaidi kuimarisha dhana ya Kanisa kama familia ya Mungu kwa kurejea kwenye misingi ya ndoa na maisha ya familia,  kwamba kuna wasiwasi juu ya hali ya kuishi pamoja na kuwa na uhusiano wa kimapenzi bila kuoana, kuoa mapema, ndoa za mitala na  kulazimishwa na ndoa za utotoni.”

Wakati wa mkutano na waandishi wa habari mnamo Jumanne, tarehe 17 Januari 2023,  walibainisha kwamba Kanisa Barani Afrika liliweka nuru  juu ya utume na uinjilishaji na juu ya uhusiano na mashirika ya kiraia, hasa na utamaduni, siasa na haki na hitimisho lilionesha hitaji la kuwasindikiza watu ili kwamba  Kanisa linaweza kuchangia maendeleo ya jamii. Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mikutano baina ya Kanda za Maaskofu wa Kusini mwa Afrika (IMBISA), Padre  Rafael Baciano Sapato alisisitizia juu ya kuimarisha sura ya familia barani Afrika na juu ya utamaduni wa kiafrika. Kwa mujibu wake alisema kuwa: “sura tuliyo nayo katika eneo letu bado ni Kanisa kama familia. Tuna matumaini kwamba mchakato huu utaimarisha sura ya familia, kwa kuwa kila mtu anazingatia sinodi.  Kwa maana hiyo “tunahitaji kwenda  mbele katika suala la utamaduni. Hadi sasa tunatambua kwamba elimu ya kiutamaduni inahusiana zaidi na liturujia, lakini kuna mambo mengine ya imani yetu ambayo yamejikita katika utamaduni wetu,"aliongeza kusema kuhani wa  Jimbo la Lichinga nchini  Msumbiji.

Wakati wa Kikao cha Kwanza huko Accra Ghana Desemba 2022
Wakati wa Kikao cha Kwanza huko Accra Ghana Desemba 2022

Katika kikao hicho kwa njia ya mtandao kilitanguliwa na  mkutano wa kwanza wa bara ambao ulifanyika jijini Accra, Ghana kabla ya ule wa pili ambao unaendelea nchini Kenya kuanzia tarehe 23-25 Januari 2023 na hatimaye Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar, SECAM, litaadhimisha Sinodi kwa Kanisa la Bara la Afrika kuanzia tarehe 1 hadi 7 Machi 2023 huko mjini Addis Ababa, nchini Ethiopia. Mkutano wa mwisho wa Sinodi ya Bara la Afrika na Madagascar (SECAM) utajumuisha wajumbe 155: wanawake walei 27, wanaume26, wasichana 16, wavulana 16, waseminari 5, wanovisi 5, mabruda 8, watawa 12, mapadre 18, maaskofu 15 na makadinali 7.

Katika hilo Awamu ya Pili ni muhimu sana katika mchakato wa utambuzi wa dhana ya Sinodi, jinsi ambavyo Kanisa linatembea katika umoja na  kudadvua avipaumbele vya Makanisa mahalia, ili hatimaye, kuweza kupata mang’amuzi ya pamoja na kuendelea kuimarisha ushirikishano na mshikamano wa udugu kati ya watu wa Mungu. Katika milenia ya tatu, Kanisa litambua vema juu ya uwepo wa shida, changamoto na mivutano inayosimikwa mizizi yake katika tamaduni pamoja na historia za watu mahalia. Na ikumbukwe Maadhimisho ya Awamu ya Pili ya Sinodi katika ngazi ya Kimabara ilianzia  mwezi Septemba 2022 ambayo itahitimishwa kabla ya tarehe 31 Machi 2023.

Sinodi:kikao cha pili katika Awamu ya Pili ya Sinodi Kibara 23-25 Januari 2023 ,Nairobi Kenya
24 January 2023, 13:05