Uganda:Askofu wa Lira atoa wito kwa waamini kusaidia wahudumu wapya!
Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican.
Msiwaangalie hawa vijana kama nyenzo za kuoa. Hili lilikuwa ni onyo kali lilitolewa na Askofu Sanctus Lino Wanok wa Jimbo katoliki la Lira nchini Uganda kwa waamini na hasa wanawake vijana wakati wa kuwekwa wakfu kwa kuhani mmoja na mashemasi watano katika Kanisa kuu la Mashahidi wa Uganda huko, Lira. Muda mfupi baada ya kuwasilishwa kwa wagombea hao katika daraja la ukuhani na ushemas, Askofu Wanok aliwaonya sana wanawake vijana kuheshimu watumishi wa Mungu na kuacha kuwashawishi waingie kwenye majaribu.
Msiwasumbue makuhani katika utume wao
Askofu Wanok aliendelea kusisitiza kwa wanawake hao akitumia lugha ya mahali hapo: “Anyira wa tima ber”, hii ikimaanisha 'wasichana wadogo': "tafadhali nipeni msaada: wachukulieni wagombea hawa kama kaka zenu na sio vifaa vya kuoa kwa sababu wametengwa kwa ajili ya utume maalum", na kuongeza kusema kuwa "mara nyingi wanawake wamefanya makuhani wengine washindwe kutimiza nadhiri ya useja wao". Askofu pia aliwaonya wazazi wa watahiniwa hao kuacha kuwavuruga wasikumbatie utume wao kwa kuwapa majukumu mazito ya kifamilia kati ya shughuli zingine ambazo zinawahusu.
Pongezi kwa kuhani na mashemasi kwa uvumilivu na mafanikio
Askofu hata hivyo pia aliwapongeza kuhani na mashemasi waliowekwa rasmi ukuhani na ushemasi kwa uvumilivu wao na kufanikiwa kumaliza kozi yao nzuri kwa mafanikio. Walakini, aliwakumbusha kuzingatia kiapo cha utii ili kufanikiwa wakati wanajitahidi kukuza na kuhamasisha Ufalme wa Mungu katika jumuiya zao mahalia. Askofu Sanctus Lino Wanok alikuwa pamoja na Askofu Mstaafu Joseph Franzelli wa Jimbo la Lira na Makuhani pamoja na waamini watu wa Mungu waliona Shemasi Haron Okello akipewa daraja la kuhani na Waseminari: Isaac Ojok kutoka Aloi, Rogers Okello kutoka Omoro, Douglas Ogwal kutoka Teboke, Emmanuel Opio Etam na Moses Edyomo kutoka Dokolo wote wakipewa dara la ushemasi.