Morocco-Kard.L.Romero:Jitihada za kimisionari na kusali Rosari
Na Sr.Angela Rwezaula-Vatican
Utakuwa ni mwezi wa aina yake wenye utajiri wa mipango kadhaa yaani Mwezi Oktoba katika Jimbo Kuu katoliki la Rabat nchini Morocco. Amekumbusha hayo katika barua yake ya kila wakati kwa waamini wake, Askofu Mkuu wa Jimbo, Kardinali Cristóbal López Romero na ambaye amekumbusha kutangazwa kwa Waraka wa Papa Francisko wa ‘Fratelli tutti’ na kuwaalika watazame kwa shukrani ya kumbu kumbu ya Mtakatifu Francis wa Assis, tarehe 4 Okotba 2020 na kuwatia moyo wa kufanya jitihada kwa ajili ya nyumba yetu ya pamoja.
Kardinali Lopez kwa maana hiyo amewashauri waamini wake kusali Rosari Takatifu, hasa katika sikukuu ya Bikira Maria wa Rosari, tarehe 7 Oktoba ili kugundua na kuzindua wito kwa upya wa kimisionari na kushirikiana kwa ajili ya utume wa kimisionari. Kwa kuelezea kwa ufupi, juu ya mkutano wa Baraza la Makuhani, uliofanyika hivi karibuni mwanzoni mwa mwaka mpya wa kichungaji, Askofu Mkuu wa Rabat amesema kuwa makuhani wa jimbo wametafakari kwa namna ya pekee juu ya dharura ya virusi vya corona ambavyo bado vinaendelea kugusa na kuyumbisha ulimwengu mzima na juu ya karantini za miezi iliyopita, huku wakishirikishana uzoefu na mafundisho muhimu waliyopata wakati wa kipindi hicho kigumu.
Baraza la Makuhani vile vile wamejadiliana kuhusiana na athari za janga la gonjwa la corona hasa kwa maisha ya wakristo na kichungaji na walitathimini uwezekano wa kuitisha sinodi ya kijimbo. Hata hivyo fursa ya mkutano huo pia ilikuwa ni kufanya mazungumzo kuhusu maandalizi ya miaka 100 ya Kanisa Kuu la Mtakatfìifu Petro la Rabat, ambapo watasheherekea mwaka kesho, vile vile shughuli za Caritas na maandalizi ya jimbo kuu kwa ajili ya kutangazwa Mtakatifu Charles de Foucauld. Hatimaye katika Barua kwa waamini Kardinali López Romero anawachangamotisha waamini wote kuanza kwa upya shughuli za kichungaji katika maparokia yote.