Watawa wamisionari wa upendo Watawa wamisionari wa upendo 

Pwani ya Pembe:Mwezi wa kimisionari waunganisha vyombo vya habari mahalia!

Maandalizi ya Maadhimisho ya Mwezi wa Kimisionari,Oktoba nchini Pwani ya Pembe inajumuisha vyombo vyote vya habari mahalia ili kuweza kutangaza vema Injili kwa watu wote.

Na Sr. Angela Rwezaula-Vatican

Mkurugenzi wa kitaifa wa kazi ya kimisionari (PMS) nchini Pwani ya Pembe  (Ivory Coast), Padre Jean Noel Gossou katika kulekea kuadhimisha mwezi wa kimisionari Oktoba ndani ya Kanisa, amewataka washiriki wa mkutano ulioandaliwa kwa ajili ya  mwezi wa kimisionari ambao uliofunguliwa tarehe 16 Sptemba katika makao makuu Altopiano Abidjan, kutumia vyombo vya habari katika uinjilishaji.

Padre Gossou akifafanua mada yenye kaulimbiu   “Mimi hapa nitume” ametoa mwaliko wa kutumia njia muafaka za uenezaji wa injili katika utume wa kimisionari. Aidha ameonesha hata maamuzi hayo yaliyotolewa katika mkutano wa kiulimwengu kwa wakurugenzi wa kitaifa.  Mkutano wa umoja wa wakurugenzi hao wa kitaifa, uliotangazwa na vyombo vya habari  kwa malengo ya kukuza moyo wa uinjilishaji umejikita katika umuhimu wa kukuza miito mitakatifu kama nyenzo za uinjilishaji. Katika mkutano huo kadhalika, kumekuwepo na mpango mkakati wa kurusha matangazo ya utume wa kimisionari kwa njia ya  Televisheni ya kanisa( Ecclesi TV), Radio Katoliki, Sauti ya Injili (La Voix de l’Evangile), Radio Espoir, na Radio za Jimbo la Grand-Bassam ili kuwezesha usambazaji mzuri wa Injili.

Mikakati mbalimbali ya kimisionari imewekwa kwa ajili ya  uchambuzi wa kauli mbiu “niko hapa nitume mimi” (Is 6:8) na kutoa pia fursa ya kukutana kwa wajumbe wa kamati ya kitaifa iliyowaweza kujadili mafaa yanayozikumba Idara za kimisionari zinazosaidia katika uongozi na katika kuhuisha moyo wa kimisionari. Kwa kunukuu katika ujumbe wa Papa Francisko uliotolewa kwa mataifa yote unaowakumbusha watu kuwa bado wako kwenye janga la gonjwa la Corona linaloathiri hali ya kiuchumi, kisiasa, kiutamaduni na kijamii, Padre Gossou amewaalika wakristo kudumu katika matumaini kama ujumbe wa ukombozi unavyodai.

Padre Gossou hatimaye katika hotuba yake  ameiuganisha kauli mbiu ya mwezi wa kimisionari na mazingira ya uchaguzi wa Rais utakaofanyika kunako tarehe 31 oktoba 2020 nchini humo.  Wakati jamii ikiwa katika hofu ya ugonjwa wa Corona, amesema mkristo anaitwa na kutumwa katika utume ili kupeleka ujumbe wa matumaini, na amani, ushirikiano wa kijamii na hivyo kila mkristo anapaswa kuitika “tazama mimi nipo hapa” na kuitika huku ni kupokea sauti ya Kristo na kuubeba ujumbe wa wokovu kwa watu wote.

24 September 2020, 15:32