Jumuiya ya Mt.Egidio:Amani ni jukumu la wote!
Na Sr. Angela Rwezaula-Vatican
Leo ni kilele cha Siku ya Amani Ulimwenguni tarehe 21 Septemba iliyotangazwa na Umoja wa Mataifa kwenye Mkutano wa mwaka 1981. Tangu tarehe 21 Septemba siku ambayo inapaishwa ujumbe wa kusitisha silaha ulimwenguni kwa masaa 24 Jumuiya ya Mtakatifu Egido imeandaa matukio mbali mbali ya elimu kuhusu amani. Mwaka huu Siku ya amani ulimwenguni inaongozwa na mada isemayo “Tuunde amani pamoja”, na hasa kwa kutaka kukazia sana hitaji la utamaduni wa huruma na ushirikiano kati ya watu na mataifa mbele ya tishio la janga hili.
Kujenga amani pamoja kiukweli ni sawa sawa na wito mkubwa wa Jumuiya ya Mtakatifu Egidio na ndiyo njia yake ya kufanya kazi katika uhusiano wa kimataifa, njia ambayo imeunganishwa kwa miaka mingi ya kazi katika utatuzi wa migogoro mingi. Kwa mujibu wa Jumuiya hii inahamasisha kuwa “Amani ni jukumu la ulimwengu wote na kila mtu lazima achangie kwa mawazo yake na kazi, kwa sababu, kama vile Mtakatifu Yohane Paulo II alivyothibitisha Siku ya Maombi ya Amani huko Assisi mnamo tarehe 27 Oktoba 1986 kwamba amani ni karakana ya ujenzi uliowazi kwa wote na siyo tu kwa wataalam, wasomi na wataalamu wa mikakati”.
Jumuiya ya Mtakatifu Egidio kwa maana hii inasasisha jitihada zake za kila siku kujenga utamaduni wa kuishi pamoja, ambayo ni dawa bora ya ile ya adui, kuwekeza katika elimu ya watoto na vijana kupitia Shule za Amani na harakati za Vijana za Amani, kukuza mazungumzo kati ya mataifa na dini na kufanya kazi ya kuwapokea wakimbizi na wahamiaji, suluhisho pekee katika changamoto ya wakati wa uhamiaji, matokeo mabaya ya vita, mabadiliko tabianchi na usambazaji usiofaa wa rasilimali za sayari.