Ufilippino-Maskofu: msiogope mabaharia kwani Kanisa liko upande wenu!
Na Sr. Angela Rwezaula-Vatican
Katika Siku ya Mabaharia Kimataifa, Maaskofu nchini Ufillipino wanasema“ msiongope kwani Kanisa liko upande wenu”. Hata hivyo katika kilele cha siku hiyo kunako tarehe 25 Juni 2020, Jumuiya ya Umoja wa Mataifa imesema kuwa mabaharia pamoja na wavuvi ni kati ya wafanyakazi mashuhuri, wanaosaidia kusongesha mbele gurudumu la maendeleo fungamani duniani. Kwa mujibu wa Maaskofu wa Ufillipino wanasema “kufikia lengo, kuwasiliana na kuendeleza jitihada za kujifunza, ndiyo njia muhimu kwao. Maisha yana mambo mengi ambayo upiga chini na juu kama vile maji baharini,. wanaandika Maaskofu katika barua iliyotiwa saini na Askofu Ruperto Cruz Santos, mhusika wa kitengo cha Utume wa Baharini wa Baraza la Maaskofu Ufilippino na ambaye anatazama muktadha huo kuwa mgumu hasa uliochangiwa na janga la Covid-19.
Shukrani kwa jitihada za mabaharia kwa jitihada
Katika ushauri wa Askofu lakini anasema, "kumbukeni hata ikiwa mawimbi yapo juu na upepo ni mkali, inabidi kuinua matanga na kufunga milango kwa utambuzi ya kwamba Kanisa liko tayari kuwaunga mkono na kuwasaidia". “Hamko peke yenu, kwani tuko pamoja nanyi, tunafanya kazi na tunawakaribisha kwenye vikanisa vyetu vidogo.” Kutokana na hii ndipo wanatoa wito kwa waamini wote kutokuwa na ubaguzi dhidi ya mabaharia na kusema “Ni mashujaa wa siku zetu. Hawawezi kubandikwa majina ya uwongo kama wabebaji wa Covid-19; badala yake, lazima wakaribishwe, wasaidiwe na wenyeji ”. “Ni wanadamu, ni wafanyakazi walioko mstari wa mbele na kwa sababu ya kujitoa katika huduma yao kwamba, sisi sote tunaweka chakula katika meza na kupokea dawa na vifaa". Kwa maana hiyo barua hiyo ya kichungaji inaongeza kwamba, ni muhimu kuonyesha kwamba hatujasahau au kuachana nao.
Mabaharia wawasiliane zaidi na wapendwa wao
Pili, maaskofu wa Ufilipino wanawahimiza mabaharia kuwasiliana zaidi na wapendwa wao, ili waweze kushirikisha katika maisha ya baharini. “Msiruhusu mazungumzo yenu yajikite tu katika mambo ya kifedha, mahitaji ya vifaa au bajeti isiyokamilika badala yake jaribuni kuruhusu mawasiliano yenu yawe ya dhati, yaliyojaa tumaini na daima yategemee kumbukumbu nzuri, ambao ni pumzi nafuu na kutiwa nguvu.” Wanaandika maaskofu.
Mafunzo zaidi na bidii ya uwajibikaji
Pendekezo la tatu ni kuendelea na njia ya mafunzo kila wakati kwa kufanya bidii zaidi, katika utendaji wa uwajibikaji na kujitoa kwenye majukumu waliyokabidhiwa. "Wakati mnapokuwa mkielekea katika fukwe na bandari zilizo mbali kwa hakika mtakabiliwa na shida ambazo zitaweka majaribu ya dhamira zenu, kanuni zenu na msimamo wenu. Lakini mbele ya haya yote, kuweni waminifu na tunzeni mwenendo wenu huo huo. Msiteleleke na kumbukeni maneno ya Yesu ambaye alisema: 'Msiogope' (Mt 14: 27). Hatimaye katika barua hiyo ya kichungaji, Mtume wa Bahari kwa ajili ya Kanisa nchini Ufilipino anawahakikishia mabaharia sala zake na kuwashukuru kwa huduma inayotolewa nchini humo. "Ninyi ni mashujaa wetu na tumaini letu”.