TANZANIA#coronavirus:Viongozi wa dini waomba uwazi juu ya Covid-19 katika nchi!
Na Sr. Angela Rwezaula- Vatican
Hivi karibuni, viongozi wa Baraza la Maaskofu (TEC), Baraza la Ushauri wa Wakristo (CCT) na Baraza la Waislam (BAKWATA) nchini Tanzania katika ujumbe wao wa tarehe 28 Mei 2020 wameomba uwazi juu ya maambukizi wa covid 19 nchini humo. Hii ni baada ya Mkutano uliofanyika katika Kituo cha Mafunzo ya Wanawake cha Baraza la Ushauri wa Wakristo (CCT ) mkoani Morogoro, ambao wameiomba serikali kutoa taarifa za wazi kwa watu juu ya takwimu zinazohusiana na kuanea kwa maambukizi ya Covid-19 nchini Tanzania ili iwezekane kujibu ipasavyo na kushiriki katika mapambano dhidi ya virusi hivyo. Zaidi walitoa ushauri kwa hospitali za nchi na vituo vya afya kutoa huduma ya bure kwa watu wenye ugonjwa wa homa ya mapafu kutokana na virusi vya corona bila kujali bima ya afya.
Covid-19 ni tishio kubwa kwa nchi na ulimwengu
Kikundi hiki cha kidini kimebainisha Covid-19 ni janga na kiukweli ni tishio kubwa kwa nchi na ulimwengu mzima, na kusisitiza kwa waamini wake juu ya umuhimu wa kuendelea kufuata hatua za kinga zilizoamriwa na wahudumu wa afya na kuwa na imani yao kwa Mungu ambaye anashinda kila uovu. Wakati wa mkutano wao, wahudumu wa afya kutoka taasisi mbali mbali na katika hospitali za TEC, CCT na BAKWATA, waliwasilisha ripoti kadhaa, wakionesha woga ulioenea kati ya wagonjwa, ukosefu wa vifaa vya utambuzi wa Covid-19 na ukosefu wa vifaa vya kinga kwa madaktari na wauguzi.
Wafanyakazi katika vituo vya afya wako hatarini kuambukizwa
Kwa mujibu wa taarifa ziliko kwenye blog ya Amecea, Mkurugenzi wa Tume ya Kikristo ya huduma za kijamii (CSSC), Dk. Josephine Balati, ameelezea juu ya uchunguzi uliofanywa na Tume katika sehemu mbali mbali za nchi, kwamba katika hospitali nyingi na vituo vya afya, kutokana na vifaa vya kinga binafsi kukosekana kwa wafanyakazi, wanaonekana kuwa na hatari ya kupata maambukizi kutoka kwa wagonjwa. “Kile wanachofanya ni kupokea wagonjwa na kuwapa chumba maalum kwa wale wanaoonyesha dalili zinazohusiana na virusi vya corona”.
Kuna hitaji la kutoa taarifa kwa umma na ushauri wa kiafya
Naye Dk. Rahma Omar, wa Mpango wa kiafya wa BAKWATA, alisisitizia umuhimu wa sala na kwa upande wa viongozi wa kidini, lakini pia hitaji la kutoa habari kwa umma na ushauri mzuri wa kiafya. Viongozi hao kwa ujumla katika kuzingatia maazimio hayo, wameomba serikali kusambaza vifaa vya kinga binafsi (PPE)kwa hospitali na vituo vyote vya afya, iwe ni katika vituo vya umma, binafsi au vya kidini. Na zaidi walipendekeza ununuzi wa vifaa vya utambuzi kwa Covid -19 na mashine za kupumulia katika mikoa mbali mbali ya nchi, na hiyo ni pamoja na kuweka uwazi zaidi juu ya kuenea kwa virusi, ili kuwaruhusu watu waweze kujua kinachotokea na kushinda hofu ambayo kwa sasa inaendelea kukua.