KENYA#coronavirus:Ask.Mkuu Muheria:Msitumie hisani kwa madhumuni
Na Sr. Angela Rwezaula- Vatican
Matendo ya hisani na mshikamano hasa katika kipindi hiki cha janga la corona hayatakiwi kutumika kwa malengo na faida binafsi, badala yake ni kwa ajili ya ustawi wa wote. Ndilo tamko na ushauri uliotolewa kwa viongozi wa kisiasa, kutoka kwa Askofu Mkuu Anthony Muheria, wa Jimbo Kuu Katoliki la Nyeri na Ris wa Tume ya Uchungaji na Utume wa Walei ya Baraza la Maaskofu Nchini Kenya.
Kila mtu ahisi kuwa familia moja ya mshikamano
Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa kwenye blog ya Amecea, Askofu Mkuu anabainisha kuwa mshikamano ni msingi kwa ajili ya wema wa wote hasa ndugu kaka na dada walio katika matatizo na kwa maana hiyo hisani hizo hazipaswi kuchukuliwa kama kifaa cha kupatia umaarufu na faida za kibinafsi”. Janga la Covid-19, anasisitiza tena Askofu Mkuu Muheria, “linaleta wasiwasi mkubwa kwa watu wetu. Kwa hili, ninawaalika kila mtu katika umoja, ili kuhisi kama familia moja katika mshikamano”. Kwa namna ya pekee Askofu Mkuu anawaomba viongozi wa kisiasa “kuwa mfano bora kwa kudumisha uhusiano mzuri na wapinzani wao, kwa lengo la heshima hiyo ambayo inaunganisha na inatoa matumaini”.
Siasa zinapaswa kutendwa kwa furaha na amani
Askofu Mkuu wa Nyeri amethibitisha kwamba “Kiukweli, siasa zinapaswa kufanywa kwa furaha na amani, siyo kwa chuki. Mungu anawategemea ninyi, na kuongeza kuwa “Hakikisha kwamba Bwana yuko katika vitendo vyenu, ili muweze kutenda kwa uwajibikaji na busara na muwe watu wa upendo na umoja”, amehitimisha Askofu Mkuu Muheria. Itakumbukwa kwamba, wa mujibu wa takwimu zilizosasishwa hadi Mei 31, zimethibitishwa kesi za Covid-19 nchini Kenya 1,848, na watu 464 wamepona wakati huo huo watu 63 wamekufa.