Tafuta

Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu wa Afrika na Madagascar (Secam) wanaomba kufutwa kwa madeni kwa nchi barani afrika wakikumbuka kwamba Afrika ni mgodi wa malighafi kwa nchi zilizoendelea. Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu wa Afrika na Madagascar (Secam) wanaomba kufutwa kwa madeni kwa nchi barani afrika wakikumbuka kwamba Afrika ni mgodi wa malighafi kwa nchi zilizoendelea.  

AFRIKA#coronavirus wito wa Secam kwa Afrika:tunahitaji msaada na madeni yafutwe na kuimarisha mshikamano!

Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu wa Afrika na madagascar(Secam)wametoa wito kwa ajili ya Afrika wakiomba kufutwa kwa madeni ya nchi na wakati huo huo kuimarisha mshikamano hasa katika kipindi hiki cha janga na baada ya janga la virusi vya covid-19.

Na Sr. Angela Rwezaula- Vatican

Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu wa Afrika na Madagascar (Secam) limezindua baadhi ya miito kwa ajili ya  bara la Afrika mbele ya kukabiliwa na dharura ya virusi vya corona. Katika taarifa kuhusu Covid-19 na matokeo yake yaliyotiwa sahini tarehe 31 Mei 2020 na, rais wa Shirikisho hilo Kardinali Philippe Ouedraogo, maaskofu wanakazia juu ya ukosefu wa rasilimali katika mapambano dhidi ya janga na misaada kwa wale ambao wametakiwa kusitisha shughuli zao.  “Bila shaka, mipango hiyo ilikuwa tayari  imeanzishwa ili  kudhibiti athari za janga hili, lakini tunapenda kwenda mbali zaidi na tuombe kufutwa kabisa kwa deni la nchi za Kiafrika ili kuruhusu uamsho wa uchumi. Na zaidi tunaomba msaada mkubwa kwa sababu uweze kuunda mifumo bora ya kiafya, kuhamasisha uundaji wa biashara ndogo na za kati ili kupunguza ukosefu wa ajira, na kuhakikisha usalama wa chakula”, wanaandika maaskofu.

Afrika ni chimbuko la mgodi wa malighafi

Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu wa Afrika na Madagascar  (Secam) wanaelekeza ujumbe wao kwa namna ya pekee kwa makampuni ya kimataifa na wafanyabiashara wakubwa, wakikumbuka kwamba Afrika ni mgodi wa malighafi kwa nchi zilizoendelea. Kwa sababu hii, maaskofu wanaomba kampuni kubwa zinazotumia malighafi hizo kuchangia ili nchi mahali wanamotoa malighafi hizo ziweze kuhakikisha zinatoa huduma msingi za kijamii kama vile  hospitali, shule na nyumba zinazofaa. Maaskofu pia wanawahimiza wajasiliamali wakubwa, wafanyabiashara  na makampuni ya dawa kutochukua fursa ya hali ya sasa kufaidika nayo na badala yake kushiriki katika juhudi za kuhakikisha msaada kwa watu walio katika hatari kubwa zaidi. “Janga la kiafya uliosababishwa na Covid-19 linapaswa kutusukuma kutafuta njia zote na njia za kumaliza magonjwa kama vile ugonjwa wa malaria na kifua kikuu, ambayo yanaendelea kutesa katika  bara (...) tunaomba Jumuiya ya Umoja wa Afrika kuhimiza nchi wanachama ili kusaidia kuunda mfuko wa mshikamano utakaotumika kwa  ajili ya afya ya watu”, wanasisitiza Maaskofu hao.

Viongozi wa kisiasa, taasisi na watu wote wenye mapenzi mema 

Viongozi wa kisiasa pia wanaalikwa kuhakikisha kuwa rasilimali ndogo zinazopatikana zinatumika kusaidia wale ambao wanahitaji msaada na siyo mazoea ya ufisadi na kuishia kwenye mifuko mibaya. Hatimaye wito wao ni kwa taasisi zote za kikanisa ili katika utume wao, wabaki kidete na washirikiane na taasisi nyingine katika kuhamasisha wema wa pamoja kwa ajili ya watu wa Afrika na Madagascar.  Kwa wote wenye mapenzi mema, mwaliko huo unawaelekeza ili kwa dhati kuunda tena thamani ya mshikamano, ili kukabiliana vyema na athari za janga na kusaidia wagonjwa wa Covid-19 na wale ambao wamepona.

Janga la covid-19 katika mabara yote matano

Shirikisho la Baraza la Maaskofu wa Afrika na Madagascar, hawakusahau kuelezea mshikamano na watu wote wa Afrika na wagonjwa wa virusi vya corona  katika mabara yote matano. “Katika miezi sita iliyopita, ulimwengu umekabiliwa na adui asiyeonekana, inasema tamko hilo, yaani ukweli wa sasa ni kama ukweli ambao hakujali tabaka la  kijamii, huku serikali za nchi tofauti za ulimwengu zikilazimishwa kuchukua hatua kali. Barani Afrika, karantini imeheshimiwa zaidi  au kidogo, lakini matokeo yamekuwa hasi hasa kwa watu wengi ambao kwa kawaida wanaishi kwa siku kutegemea na kipta cha kila siku. Katika ngazi ya  kiuchumi, hasa kushuka kwa uchumi ni dhahiri, kwa sababu janga limeweza kusimamishwa kwa shughuli, hususan katika sekta muhimu za uzalishaji, utalii, safari za ndege  na tasnia ya hoteli.

Madeni na ukosefu wa ajira kusababisha umaskini zaidi

Maaskofu wa Secam wanaogopa athari za kijamii katika nchi nyingi na hasa barani Afrika, ambao tayari wamejazwa na  mzigo wa madeni na viwango vya ukosefu wa ajira ambavyo vitasababisha kuongezeka kwa umaskini. Kwa maana hiyo watuhimiza kwamba “siyo kutazama kama vile janga ni adhabu ya Mungu badala yake, Mungu aliupenda ulimwengu hadi kumtoa Mwanaye wa Pekee  ambaye, alitoa maisha yake msalabani kwa ajili ya wanadamu”.Wanakumbusha. Kwa mujibu wa Maaskofu, kile ambacho mwanadamu anafanya uzoefu kinalingana na kile ambacho walifanya uzoefu wanafunzi wa Yesu baada ya kifo chake, ufufuko na kupaa, ambapo, walikatishwa tamaa na kuogopa, lakini baadaye wakabadilishwa kutokana na kushuka kwa nguvu ya  Roho Mtakatifu.

Janga la covid-19 lafunua mipaka ya utandawazi

Hatimye Maaskofu wa Secam wamedokeza juu ya, janga la Covid-19  kwamba limefunua mipaka ya utandawazi, inayolenga uchumi pekee yake na juu ya  kukuza utumiaji hovyo na ubinafsi, kwa kupotisha uadilifu na maadili ya kiroho. “Mfano wa madaktari na wahudumu wa afya, ambao wameonesha kujitoa katika taaluma yao, huku wakihatarisha maisha yao, imeleta ufahamu kuwa dunia, baada ya virusi vya corona haiwezi kuwa kama hapo awali. Usawa ni muhimu zaidi kuliko mashindano yasiyoisha ya kutaka kufanikiwa na faida”. Kwa njia hiyo maaskofu wahamasha  kwa kukumbusha juu ya “Mafundisho Jamii ya Kanisa Katoliki katika mapendekezo mazuri ya pamoja, mshikamano, heshima kwa hadhi ya binadamu, haki na maendeleo fungamani”.

02 June 2020, 13:36