UGANDA:Ujumbe wa Ask.mkuu Kizito:Hija ya Siku ya Wafiadini Uganda itafanyika kijimbo!
Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican
Mwaka huu maadhimisho ya Siku ya Wafia dini Uganda yataadhimishwa kwa ngazi ya kijimbo siku ambayo kwa kawaida ni tarehe 3 Juni ya kila mwaka. Kiutamaduni tukio hili limekuwa likiadhimisha kwa hija kuu katika Madhabahu ya Namugongo Kampala Uganda, lakini mwaka huu kwa sababu ya janga la virusi, tukio hilo limehairshwa. Amethibitisha hayo Askofu Mkuu Cyprian Kizito Lwanga, wa Jimbo Kuu Katoliki Kampala na ambaye katika ujumbe wake kwa waamini amefafanua kuwa maadhimisho ya tarehe 3 yatafanyika kwa ushiriki wa idadi ya watu wachache sana. Kwa wengine wate watakuwa na fursa ya kutazama kwa kuwa itatangazwa mubashara na televisheni na mitandao ya kijamii. Maandalizi ya sherehe hizo zimenza tarehe 24 Mei, katika Sikukuu ya Kupaa kwa Bwana kwa sala ya Novena kwa wafiadini wa uganda. Maelekezo na sala hata na mengine vinapatikana katika mtandao (e-book).
Katika ujumbe wake kwa mujibu wa habari katoliki (Cisa), Askofu Mkuu Kizito amewaalika waamini kuomba kwa siku hizi katika maombezi ya wafiadini wa Uganda kwa ajili ya wagonjwa na wanaokufa, kwa wale wanao wahudumia, kwa wale wote wanaofanya kazi ili kupunguza kasi ya Covid-19, kwa ajili ya waliolundikana kwa sababu ya mafuriko yaliyotokea katika sehemu mbali mbali za Nchi, kwa ajili ya wale wote waliopoteza mazao na chakula kutokana na uvamizi wa nzige kwa upande wa Kaskazini mashariki mwa Uganda na kwa ajili ya ulinzi wa Mungu dhidi ya hatari hizi zote.
Askofu Mkuu Kizito amesema “Imani yetu na maisha yamesimika mizizi katika damu ya wafiadini na ambao ni waombezi wetu kwa Mungu na mfano wa maisha ya kikristo. Katika kipindi hiki kigumu cha mateso kwa sababu ya janga la covid -19 , tukitazama katika sala na kubaki kidete katika imani, matumaini na upendo wa Mungu ambaye anaponya, anaingilia kati na kuokoa.”